Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia juu ya hoja iliyowekwa mbele yenu na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kuhusu mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Kazi kubwa inafanyika lakini kweli kwamba katika mambo yote ya kufanya kazi changamoto hazikosekani, hata sisi wenyewe kule majimboni tunafanya kazi nzuri lakini bado changamoto zimeendelea kuwepo. Mimi naamini kwamba tukipeana muda tukapeana mawazo yaliyo sahihi tutafika katika malengo makubwa tunayoyataka.

Mheshimiwa Waziri katika kitabu chako cha hotuba yako ya juu ya mipango yako mambo ya msingi ambayo mimi nimeyaona na ninataka niyagusie hapa, lakini katika eneo litakuwa ni kuongeza juu ya yale mambo mazuri ambayo mmeyasemea nataka nianze na jambo la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la kilimo nimeona kwamba shughuli kubwa inayofanyika ya kujenga maghala, lakini Mheshimiwa Waziri ni ukweli kabisa kwamba bado sijaona ile nia ya dhati kabisa Serikali yetu kukifanya kilimo chetu kikawa cha kibiashara. Nimeona maeneo mengi mmezungumza lakini mimi nataka nizungumzie hasa katika kilimo cha mpunga.

Mheshimiwa Waziri kama unakumbuka vizuri wakati wa hotuba ya bajeti tulichangia na kueleza kwa wazi kabisa juu ya ambavyo mabonde yetu makubwa Tanzania kwa mfano kama lile la Ruvu pale linavyoweza kuwa chanzo kizuri cha kuzalisha chakula cha kutosha lakini katika hotuba yako Mheshimiwa Waziri nimeona mmezungumzia sana jambo la eneo la Kilombero kwa maana ya bonde lile la Morogoro, lakini Mheshimiwa Waziri kiukweli kabisa Tanzania inayo mabonde mengi sana ambayo kama yatatumika vizuri kilio cha watu kulia njaa kukosekana kwa chakula kitakwisha kabisa na hata itaweza kufika sehemu kwamba tuna uwezo wa ku-supply chakula kwa nchi za nje na kuuza kwa ajili ya kupata fedha za kigeni.

Sasa Mheshimiwa Waziri nikuombe utakaposimama utuambie juu ya mpango mkakati mlionao wa kuendelea kutumia mabonde haya kwa ajili ya faida ya Watanzania hasa hasa mimi nazungumzia hapa Bonde la Ruvu ambalo tunalo kwa sisi wenyeji wa Pwani hasa maeneo ya Chalinze na Bagamoyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo Mheshimiwa Waziri nikupongeze, nimeona katika taarifa nilizozisoma juu ya benki yetu ya kilimo jinsi ambavyo imeweza kuwasaidia AMCOS zinazolima pamba kwa kutoa vifaa vyenye thamani ya shilingi bilioni 1.5 kusaidia kuweza kuvuna pamba na kuiweka katika maeneo mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikuombe sana kwamba kilimo kipo cha namna nyingi lakini pesa hizi naamini kwamba zipo na mahitaji ni makubwa sana. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri muendelee kuangalia maeneo mengineyo pia, kilimo sio pamba tu peke yake, tunacho kilimo cha korosho, kahawa, alizeti na mazao mengineyo ambayo Waheshimiwa Wabunge wameeleza hapa kama walivyotangulia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia Mheshimiwa Waziri nimtoe wasiwasi ndugu yangu Mbunge wa Sumve amezungumzia juu ya pamba kukosa maeneo na kwamba pamba nyingi inasafirishwa nje. Sasa hivi pale Chalinze tunajenga kiwanda kikubwa sana ambacho kinakuja kutengeneza vitambaa na material zote zinazotokana na pamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana aende akawahamasishe wananchi wake wa Sumve na maeneo yote ya wakulima wa pamba kwamba sasa pamba ile itakuwa haifiki Dar es Salaam bandarini isipokuwa itakuwa inaishia Chalinze pale kwa ajili ya kuchakatwa na kutengenezwa material ambazo zinakwenda kuwa sehemu kubwa ya kutatua tatizo kubwa la kupatikana kwa vitambaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo, nizungumzie kidogo katika eneo la mifugo. Nimeona kazi kubwa na nzuri sana ambayo inafanywa na Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na wizara yake kwa ujumla lakini bado tumekuwa na tatizo kubwa sana la kuchunga au kugeuza nchi nzima kuwa ni sehemu ya machungio. Mheshimiwa Waziri kiukweli kabisa nyama nzuri haiwezi kupatikana kwa ng’ombe kutembea kutoka Sumve huko Mwanza mpaka Chalinze. Ng’ombe mwenye nyama nzuri anapatikana kwa kutunzwa, kulishwa vizuri na matunzo yakawa yenye kutengeneza ubora huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nimeona hapa mmezungumza jinsi ambavyo mnataka kuhakikisha kwamba ng’ombe wetu wanakuwa wana uwezo wa kuzalisha maziwa yenye ubora zaidi. Mheshimiwa Waziri nataka nikukumbushe kama vyombo havitosimamia ile Sheria ya Usafirishaji wa Mifugo kilio hiki na matatizo haya yataendelea katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana wewe na Mheshimiwa Waziri wa Mifugo, namuona ndugu yangu, Mwenyekiti wangu Bwana Ulega anafanya kazi nzuri sana lakini kama hatutoweza kusimamia sheria hizi hatuwezi kupata nyama iliyo bora au maziwa yaliyo bora. Itaishia kila siku ng’ombe ambao unatarajia watoe lita 12 mpaka 14 watakuwa wanatoa lita mbili au lita moja kwa sababu ya kuchoka kwa kutembea umbali mrefu na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote hayo nizungumzie pia jambo la afya, ni kweli kwamba fedha nyingi sana zinapelekwa katika afya. Mimi binafsi nawashukuru sana mmeendelea kutuangalia watu wa Chalinze kwa jicho la huruma zaidi, kituo changu cha afya cha Kibindu sasa kinakamilika na Lugoba kule mambo ni mazuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia wameeleza waliotangulia juu ya ufinyu wa watoa huduma za afya. Mimi nikuombe sana hili jambo ni jambo sensitive sana, tunaweza tukawa na majengo mazuri sana lakini kama majengo yale hayafanani na huduma zinazotolewa itakuwa ni jambo ambalo kwa kweli mwisho wa siku wananchi hawatotuelewa. Nikuombe sana tuendelee kuliangalia jambo hili na kulipa kipaumbele chake kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nikushauri Mheshimiwa Waziri pamoja na Serikali yangu katika eneo la bima ya afya. Sasa hivi kwa bima kubwa kabisa kwa mfano tunalipa shilingi 1,500,000, hii shilingi 1,500,000 kwa mwananchi wangu anayetoka kule Talawanda kusema kwamba akalipe kwa kweli ni ngumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana kama tutaamua kuja na mkakati wa kuwawezesha wananchi kulipa kiwango hiki cha shilingi 1,500,000 ambacho kinatakiwa kulipwa kwa mwaka kikalipwa katika installments za kila mwezi. Kwa maana sasa kwa kila mwezi mwananchi akawa analipa at least shilingi 125,000. Hili jambo wanaliweza na wananchi pia wapo tayari kufanya hivyo. Leo hii unaweza kukuta mama ana tatizo labda ana uvimbe tumboni, anatakiwa alipe shilingi 3,000,000 ili aweze kupata matibabu, lakini mtu huyu kama angeweza kulipa shilingi 1,500,000 maana yake angeweza kupata matibabu hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukaja na mkakati mzuri ambao unaweza ukasaidia kupunguza matatizo na machungu kwa wananchi wanyonge ambao tuliwaahidi kwamba tutaendelea kuwaangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa ambalo limetokea jana Mheshimiwa Waziri hasa Waziri wa Afya nikupe tu taarifa kwamba Kituo chetu cha Afya cha Msata kimepata nyota nne na kimekuwa cha kwanza Mkoa wa Pwani kwa ubora. Haya ni mambo ambayo yanaendelea kufanyika katika Halmashauri ya Chalinze na sisi tunaendelea kusimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipekee kabisa niwashukuru sana wenzangu ambao wanafanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha kwamba mambo haya yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la viwanda kwa kipekee kabisa nimpongeze sana Mkuu wangu wa mkoa Engineer Evarist Ndikilo kwa jinsi ambavyo anaendelea kufanya kazi kubwa ya kusimamia kuhakikisha mapinduzi ya viwanda kwa Chalinze yanakuwa ni kweli lakini kwa Mkoa wa Pwani kwa ujumla wake.

Ninachokuomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha muendelee kuhakikisha kwamba yale maeneo tengefu ambayo tumeyatenga mnayapelekea fedha ili zile fidia ambazo zimeahidiwa kulipwa wananchi zilipwe, lakini pia yale maeneo ambayo tumetenga kwa ajili ya viwanda nayo pia mnaendelea kuweka msisitizo na msukumo kuhakikisha kwamba viwanda vile vinakamilika mapema iwezekanavyo na Serikali iweze kufikia malengo yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la Hydro- Electric Power Rufiji; Mheshimiwa Waziri nikuhakikishie wananchi wa Chalinze wanasubiri kwa hamu kubwa sana mradi huu wa umeme. Mradi huu wa umeme unakuja kutatua kero ambayo sasa tumeanza kuipata ndani ya Chalinze, umeme hauji vizuri kwa sababu wananchi wanagawana umeme na viwanda. Viwanda vimekuwa vingi, Serikali yetu imesisitiza juu ya viwanda na sisi Chalinze tunatimiza kwa vitendo, lakini kwa kweli adha hii inayoanza leo tunaogopa isijekuwa ngumu halafu baadaye wananchi wakaja kuuliza kwamba sasa viwanda hivi mlivileta ili vitusaidie nini kama sio kuja kutuongezea tabu katika maisha yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru na naunga mkono hoja, ahsante sana.