Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nitoe mchango wangu katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri na hotuba ya Kamati yetu ya Bunge ya Bajeti kuhusiana na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tu kwanza kuipongeza Serikali, Mheshimiwa Waziri pamoja na Mawaziri wote na Watanzania wote kwa ujumla, kwa namna ambavyo wanaunga mkono Serikali ya Awamu ya Tano katika kuhakikisha kwamba Tanzania yetu inakwenda mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitabu cha Serikali chenye mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2019/2020, ukurasa wa 34 - 49, vimeelezwa vipaumbele mbalimbali ambavyo Serikali yetu tayari imeshaanza kuvitekeleza na vingine viko katika hatua nzuri na naamini kabisa kwamba vipaumbele hivi vitakapokuwa vimekamilika, vitaifanya Serikali na Taifa letu la Tanzania kuwa miongoni mwa mataifa ambayo kwa kweli yatakuwa yamepiga hatua kimaendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ujenzi wa mradi wa uzalishaji wa maji wa Rufiji wenye megawatt 2,100; ujenzi wa reli ya kati, maendeleo ya ujenzi tumeyaona na juzi Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuwa amekwenda kukagua utekelezaji na tukapata taarifa pia kwa Mkurugenzi wa Shirika la Reli, Bwana Kadogosa, alieleza mambo mengi. Tunaamini kabisa kama wale wa Shirika la Voda wanavyosema kwamba yajayo yanafurahisha, nami nina imani kabisa kwamba kwa kweli ndani ya Serikali ya Awamu ya Tano hakika yajayo yanafurahisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni nchi ambayo imejaaliwa kwa mambo mengi na naomba Watanzania wote tushikamane kwa pamoja kuhakikisha kwamba tunaiunga mkono Serikali yetu. Katika mambo yote ambayo Serikali yetu imejipanga kuyatekeleza, tushikamane pamoja na tuone kwamba miundombinu ambayo inajengwa na Serikali ni kwa ajili ya Watanzania wote. Ndege zinazonunuliwa, reli na treni zitakazokuwa zinahudumia Watanzania, zitakuwa ni kwa ajili yetu wote na kwa maslahi ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu kwamba tunayo mambo machache ambayo kimsingi tunatakiwa tuyazingatie na kupambana nayo hasa juu ya suala zima la hifadhi ya mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Bila kumung’unya maneno, nataka niseme tu kwamba uharibifu wa mazingira ni adui mkubwa ambaye anaweza akasababisha harakati zetu za kujikomboa na kutaka kulifanya Taifa letu liende mbele kukwama. Kwa ajili hiyo, napendekeza kwa kweli habari nzima ya utunzaji wa mzingira ipewe kipaumbele katika maeneo yetu ya utawala katika mikoa, vijiji, wilaya na kila sekta ijipambanue katika kuhakikisha kwamba tunahifadhi mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukataji wa miti ovyo, tumeziona athari zake katika Kanda ya Ziwa na hasa mikoa ya Shinyanga, Tabora hata kwetu Geita, athari zake tunaziona. Kwa maana hiyo, naomba kwa kweli Watanzania wenzangu ambao bado hawajapata athari ya ukataji wa miti, waje wajifunze Kanda ya Ziwa ili waweze kuona ni namna gani mvua haziwezi kupatikana kwa uhakika na kwa maana hiyo tunapata shida kweli kweli. Kwa hiyo, naomba Serikali yetu ijipange kuhakikisha kwamba tunakuwa na mkakati wa upandaji miti katika maeneo ambayo yameathirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuchangia ni eneo la mazingira wezeshi kwa wawekezaji, yaani yale mazingira ambayo yanaweza kusababisha uvutiaji wa wawekezaji kutoka nchi za nje kuja kuwekeza katika nchi yetu. Katika tafiti mbalimbali zimeonesha wazi kwamba Tanzania haina mazingira rafiki ya wawekezaji katika sekta mbalimbali. Wakati tunapojiandaa kutengeneza Tanzania ya viwanda, basi mazingira ambayo yanatuonesha kwamba sisi tunakuwa ranked wa namba za mwisho, tuyarekebishe ili kusudi kusababisha nchi yetu iweze kuwa ni eneo la kupendelewa na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kweli katika hatua mbalimbali ambazo imezifanya. Katika sekta ya afya ambayo kimsingi Taifa lolote ambalo linataka kuendelea lazima watu wake wawe na afya njema na Serikali yetu imewekeza vya kutosha katika sekta ya afya. Tumeona jinsi ambavyo vituo vya afya vimeboreshwa na hata upatikanaji wa dawa na wenyewe umekuwa wa kuridhisha. Kwa hiyo, naipongeza Serikali na naomba iendelee na moyo huo na ikiwezekana kwa kweli maeneo ambayo bado hayajapata huduma za Hospitali za Wilaya kama huko kwetu Mbogwe, basi Serikali ione uwezekano wa kutuingiza katika utaratibu ikiwezekana miaka ijayo tupatiwe Hospitali ya Wilaya ili kusudi wananchi wa kwetu huko nao waweze kupata huduma za afya katika ukamilifu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la viwanda. Napendelea kabisa Serikali yetu pia ilitupie macho suala zima la utengenezaji wa viwanda vya mbolea. Kama ambavyo tumeweza kufanikiwa katika sekta ya viwanda vya kutengeneza saruji, basi na utengenezaji wa mbolea Serikali ione uwezekano huo ili kusudi suala zima la sekta ya kilimo iweze kupata msukumo wa peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viwanda pia vya utengenezaji wa madawa ya binadamu na wanyama pamoja na viuadudu ni muhimu. Naomba viwanda hivi na vyenyewe vipewe kipaumbele ili kusudi Tanzania yenye watu asilimia zaidi ya 75 wanaotegemea kilimo, basi kilimo hiki kiwe na tija. Watu wetu watakapokuwa wamepata miundombinu ya madawa na viuadudu na vile visumbufu vya mimea, naamini kwamba uzalishaji wa mazao ya biashara na ya chakula utakuwa uko katika hali nzuri na matokeo yake Tanzania ya viwanda itakuwa imefikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwa mara nyingine kwamba naisifu Serikali kwa kazi zake nzuri ambazo imeendelea nazo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)