Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kuchukua nafasi hii kipekee kabisa kukushukuru kwa kunipa fursa hii kuweza kuhitimisha hoja hii ya bajeti ya Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote takribani 65 ambao waliweza kuchangia, kwa kuongea walikuwa 26 na kati yao 39 waliweza kuchangia kwa maandishi. Kwa hakika kwa niaba ya Wizara ya Madini tunawashukuru sana kwa michango hiyo mizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kipekee kuchukua nafasi hii kumshukuru kwa mara nyingine tena Mheshimiwa Rais wetu mpendwa, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuendelea kuniamini na kwa kunipa nafasi hii ambayo kwa hakika ni heshima kwetu. Niendelee tu kumhakikishia mimi pamoja na Naibu Waziri wangu; Mheshimiwa Nyongo pamoja na Mheshimiwa Biteko kwamba hatutamwangusha na tutahakikisha kwamba tunatekeleza majukumu yetu kwa weledi na ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuwashukuru Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Nyongo na Mheshimiwa Biteko. Kwa hakika kama nilivyosema wakati nawasilisha hoja hii wamekuwa ni watu wa msaada sana kwangu. Nilieleza kwa takribani miezi mitatu sikuwepo, wamefanya kazi kubwa lakini pia wanaendelea kufanya kazi kubwa, kwa kweli ninajivunia kuwa nao kama Naibu Mawaziri wangu. Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki na niwahakikishie kwamba nitakuwa wazi kwao, tutaendelea kushirikiana wakati wowote watakapohitaji mwongozo wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nimshukuru Mheshimiwa Prof. Kabudi, tumekuwa tukishirikiana sana katika suala hili la usimamizi wa sekta hii ya madini hususani katika suala zima la majadiliano ya mikataba. Napenda kumshukuru pia Mheshimiwa Dkt. Kilangi kwa namna ambavyo anaendelea kutushauri kama Mwanasheria Mkuu wa Serikali na kutupatia Miongozo mbalimbali na tafsiri na fafanuzi katika masuala ya kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wahenga walisema tunahitaji mikono, jicho na mdomo wa kila mwanakijiji kuweza kumlea mtoto mmoja kwa mafanikio. Kwa hakika hivi ndivyo ilivyo kwa Wizara hii mpya ya Madini. Katika upya wetu tunahitaji sana mchango wa maoni, mapendekezo, ushauri wenu kukosolewa na kila Mheshimiwa Mbunge pale ambapo mtakapoona kuna haja ya kufanya hivyo. Sisi tunaamini kwa kufanya hivyo, hiyo hiyo ndiyo njia pekee ya kuweza kuimarisha Wizara yetu hii mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mwaka jana upande wa sekta ya madini wachangiaji hawakuwa wengi sana lakini nilikuwa nafurahi sana kila ambavyo nilikuwa naona Mbunge anasema mpaka tumefikisha Waheshimiwa 65 kwa maandishi na mdomo, tunawashukuru sana sana. Napenda kipekee kuwashukuru wote walioweza kuchangia hoja hizi, mmetuimarisha sana na napenda kutoa shukrani za dhati kwa michango mizuri ambayo mmetupatia. Niwahakikishie kwamba tumeipokea, tumefaidika sana na niwaahidi tu kwamba tutaifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajibu hoja chache lakini kwa zile ambazo nitaweza kuzijibu niwahakikishie kabla ya Bunge letu hili halijaweza kuhitimishwa tarehe 30 Juni tutaweza kuwasilisha majibu yote kwa maandishi kwa kila Mheshimiwa Mbunge kwa namna alivyochangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa ambacho kinanipa faraja mimi na wenzangu ni kwamba sisi na Waheshimiwa Wabunge wote tunazungumza lugha moja na sote tunavuta katika upande mmoja wa kutetea maslahi ya Watanzania wenzetu. Sote tunaamini kwamba sekta ya madini itakaposimamiwa vizuri, tutaweza kuvuna zaidi ya kiasi cha madini tunachokivuna hivisasa. Zaidi kwa ujumla wetu tunao, muafaka sote kwamba wananchi wetu ndiyo wenye kustahili kufaidika zaidi na rasilimali ya madini waliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu. Pia tunakubaliana kimsingi kwamba wakati ndioyo sasa na sisi ndiyo wale historia imetukabidhi jukumu na wajibu wa kuliwezesha hili. Naamini, madamu tunakubaliana katika haya ya msingi basi hakuna kwa hakika litakaloharibika. Kwa lugha ya leo tunaweza kusema yajayo yanafurahisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano iko bega kwa bega na Bunge lako Tukufu katika kusimamia rasilimali ya madini ya nchi yetu. Ni kwa msingi huo Serikali ilifanya mabadiliko ya Sheria ya Madini ambayo Waheshimiwa Wabunge mliweza kuipitisha pamoja na Kanuni mpya nilizozitunga mwaka huu wa 2018. Niwahakikishie tena Waheshimiwa Wabunge tangu mabadiliko ya Sheria yalipofanyika, kampuni mbalimbali za madini za ndani na nje ya nchi zimeonyesha nia ya kuwekeza katika sekta ya madini nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa kufuatia kuundwa kwa Tume mpya ya Madini tunatarajia kwamba maombi ya leseni kwa ajili ya uwekezaji katika sekta ya madini yatashughulikiwa mapema ipasavyo. Vilevile kama Serikali tumeanza kutekeleza mpango wa kujenga uwezo wetu wa kuhakiki mitaji inayowekezwa na shughuli zinazofanywa na kampuni za madini. Nia yetu kubwa ni kuwa na uwezo wa kuhakiki taarifa za kampuni kuhusu uwekezaji wao na shughuli zao. Napenda kuwahakikishia kwamba sisi kwa upande wetu kama Wizara hatutalala, tutakuwa macho na tutaendelea kuchukua hatua kila mara itakapobidi. Nachoomba Waheshimiwa Wabunge kutoka kwenu ni mambo mawili. La kwanza, ni imani na ushirikiao wenu katika kutekeleza wajibu wetu huu mkubwa. Pili, niendelee kuwaomba kwa heshima na unyenyekevu mkubwa mtupitishie bajeti hii ambayo kwa hakika ndiyo itakayokuwa nyenzo muhimu kwetu ya kutuwezesha kutekeleza azma yetu hii. Haya yote mawili kwa hakika yamo ndani ya uwezo wenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo ya utangulizi, niruhusuni sasa nianze kujibu baadhi ya hoja kama zilivyotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, ilikuwepo hoja ya Mheshimiwa Kanyasu kuhusiana na Mzee wangu Felix Ngowi na wenzake ambao wana mgogoro na mgodi wa GGM. Kwa kweli ameeleza kwa hisia kubwa na mimi nimesikitika. Hukumu takribani sita zimeweza kutolewa kuhusiana na suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kumhakikishia Mheshimiwa Kanyasu pamoja na Mheshimiwa Musukuma na Wabunge wote wa Geita na wengine wote wenye mapenzi na wanyonge wetu katika Taifa hili kwamba suala hili nitalichukua kwa uzito wa pekee. Kwa kuwa na mimi mwenyewe ni mwanasheria, nitakaa na Mheshimiwa Jaji Mkuu kuweza kuliangalia suala hili limekaaje ili kuweza kulipatia ufumbuzi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja pia kuhusiana na GGM, wanapokuwa wanatoa mipango mbalimbali ya uwajibikaji katika jamii au CSR kwamba bei kubwa za vifaa zinakuwa inflated. Tulielezwa hapa, lori moja la mchanga mpaka takribani Sh.350,000. Napenda kusema tu kwamba hili halikubaliki, niendelee tu kuwaomba Waheshimiwa Madiwani wetu, kupitia kifungu cha 105(1)(2) na (4) cha Sheria yetu ya Madini ya 2010 kama ilivyorekebishwa mwaka 2017, kabla hawajaridhia mpango wa mwaka wa uwajibikaji kwa jamii wahakikishe kwamba wamejiridhisha kile kinachoahidiwa katika mpango huo wa mwaka basi kweli kinaendana na thamani halisi ya fedha. Napenda kumwambia Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote, tutafanya ukaguzi maalum kupitia Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) kuiangalia migodi yote mikubwa katika CSR zao ambazo wamekuwa wakizitoa katika jamii zao na kuona kwamba kweli zinaendana na kiasi halisi cha fedha inayoelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja kuhusiana na ruzuku, wapo wachimbaji wadogo ambao waliweza kunufaika lakini kwa bahati mbaya wapo takribani wanufaika tisa ambao hawakuweza kuwa waaminifu na walizitumia fedha zile vibaya kwa kukiuka mkataba. Napenda tu kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge suala hili tumelipaleka TAKUKURU na tayari uchunguzi wake umefanyika na tunaamini wataweza kuchukuliwa hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja nyingine kuhusiana na suala zima la madini ya bati kwa upande wa Kyerwa. Wote tunafahamu tunao Mkataba wa ICGLR ambapo kupitia mkataba huo, hatuwezi kuuza madini yetu nje ya mipaka yetu bila kusaini Itifaki ile ya Illegal Exploitation pamoja na mkataba ule wa ICGLR kuhusuiana na usalama na ulinzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kumhakikishia Mheshimiwa Bilakwate ameeleza suala hili kwa uchungu mkubwa, tunaona hoja hii kwa msingi wake. Kama Serikali tumeshaanza kulifanyiakazi na tuko katika hatua ya mwisho ili kuhakikisha kwamba tunaleta mkataba huu Bungeni ili uweze kuridhiwa na kuruhusu biashara ya bati kuuzwa katika soko la kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja kuhusiana na mgodi wetu wa Buckreef, kwa muda mrefu wabia wetu au wabia wenza wa STAMICO wamekuwa wakishikilia mgodi ule lakini wamekuwa hawatimizi kama ambavyo mikataba imewataka. Napenda kuwahakikishia tayari tumeshafikisha suala hili katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na tunaamini tutaweza kupata tafsiri na miongozo ya namna gani ya kuweza kuachana na mikataba huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja nyingine kuhusiana na kukamilisha ujenzi wa smelter; Mheshimiwa Mama Nagu, Mheshimiwa mama Mbene, Mheshimiwa Kapufi na wengine wengi wameweza kulizungumzia hili kwa uzito mkubwa. Kama nilivyowaeleza awali, niwahakikishie kwamba tayari tumeshapata waombaji takribani 27 na tunachokifanya hivi sasa ni kuhakikisha kwamba tunayachambua na kuweza kufanya uchunguzi au due dilligence ili kuhakikisha kwamba tunampata mwekezaji ambaye kweli anavyo vigezo na ni mahiri katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja za Mheshimiwa Catherine Magige kuhusiana na utoroshwaji wa madini ya tanzanite lakini zaidi alitupa ushauri tuweze kuimarisha mipaka yetu ya Namanga, Horohoro pamoja na mipaka mingine. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kufuatilia mnyororo mzima wa uchimbaji, uendeshaji wa biashara hii ya tanzanite pamoja na mauzo nje ili kudhibiti utoroshaji. Pia napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kama Wizara hivi sasa tunaandaa utaratibu imara wa kuweza kuwapatia motisha wananchi watakaoweza kutoa taarifa au whistleblowers juu ya watoroshaji wa madini ya tanzanite pamoja na madini mengine. Pia tunaandaa simu maalum au hotline maalum ambayo tutaitumia katika kupokelea taarifa kuhusiana na masuala ya utoroshaji na biashara nzima hii ya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja za Mheshimiwa Ndassa ambaye kimsingi aliweza kutushauri tuweze kuonyesha ni namna gani tunaweza kuwasomesha wathamini wetu wa madini ambao hivi sasa tunao wathamini wachache. Napenda kumshukuru kaka yangu Mheshimiwa Ndassa na nimhakikishie tu kwamba tunalipa suala hili la uthamini wa madini uzito wa kipekee. Tayari tumeshaainisha au tumeshawatambua watumishi 10 ambao tutawapeleka kwenye mafunzo katika nchi ya Thailand pamoja na India ili waweze kupata mafunzo maalum ya gemology kwa ajili ya kuweza kutambua madini ili waweze kutambua na kufanya uthamini ili tusiweze kuibiwa na kuweza kupata fedha stahiki au mirabaha stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja kuhusiana na kufunga security system katika ukuta wetu wa Mererani. Nimshukuru kaka yangu Mheshimiwa Bulembo kwa kuweza kuona umuhimu wa suala hili. Nimhakikishie kwamba ni suala ambalo kwa kweli tunalipa upekee mzito. Ameeleza hapa masuala ya mitobozano na masuala mengine. Nisingependa kueleza masuala mengi ya kiusalama lakini nimhakikishie kwamba hoja na ushauri wake utazingatiwa na tutahakikisha kwamba tutakuwa na mfumo wa ulinzi ambao kwa kweli hapatakuwa na utoroshaji hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja ya ndugu yangu Mheshimiwa Bobali kuhusiana na tozo nyingi katika chumvi pamoja na masuala mengine lakini pia Mheshimiwa Hamida, Mheshimiwa Ngombale na Waheshimiwa wengine, niwashukuru kwa hoja hii. Kipekee kabisa napenda kuwaeleza kwamba nilipata hoja hii kutoka kwa Taasisi yetu ya TASPA ya wazalishaji wa chumvi. Nasi kama Wizara kwa kweli tuliliona kwa uzito mkubwa. Ukiangalia gharama inayotumika katika uzalishaji wa chumvi wanapata faida kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni takribani Sh.150 peke yake katika kilo 50, Sh.3 kwa kila kilo ni fedha ndogo sana. Hii inatokana na tozo zilizopo katika biashara nzima, wana tozo zaidi ya 16. Tayari kama Serikali, tumeanza mashauriano, tumewasilisha Wizara ya Fedha, kwa upande wetu kama Wizara ya Madini na Wizara ya Viwanda kuona ni namna gani suala hili linaweza likaangaliwa kwa mapana yake ili kuweza kuhamasisha uzalishaji wa chumvi ya Tanzania. Maana yake hivi sasa Tanzania tunayo chumvi nyingi na ukiangalia sekta hii ya chumvi imekuwa ikiajiri akina mama wengi sana lakini tumegeuzwa kuwa soko la nchi nyingine, tunanunua chumvi ya nchi zingine kwa sababu tu gharama za uzalishaji zimekuwa kubwa. Napenda tu kusema kwamba tunaomba muweze kutuvumilia katika suala hili, Serikali yetu sikivu, tunaamini suala hili litaweza kupatiwa ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na pendekezo la Mheshimiwa Bilakwate kuhusiana na suala zima la uongozi wa STAMICO. Napenda tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, tumeanza kufanya mageuzi kwa ajili ya uongozi wa Shirika hili la STAMICO. Tayari tumeshambadilisha Mkurugenzi Mtendaji, tumeshaanza kubadilisha baadhi ya Wakurugenzi na tutafanya hivyo kila mara itakapoonekana inahitajika. Hoja hiyo pia ilielezwa na kaka yangu Mheshimiwa Bobali pamoja na Waheshimiwa wa Bunge wengine. (Makofi)

Mheshimiwa n aibu Spika, ilijitokeza pia hoja ya Mheshimiwa Rashid Shangazi kuhusiana na madini ya bauxite kule Lushoto lakini pia alinialika niweze kutembelea eneo hilo. Nimueleze kwamba mimi natoka Same na anajua Same ni jirani na Lushoto, kwa hiyo, kwa hakika kila nikitembelea Same nitahakikisha pia nakwenda Lushoto ili kuweza kujionea maeneo yale ya Makanya, Magamba, Soni pamoja na Malindi lakini zaidi kuwaunganisha wananchi wa Lushoto wale ambao wanayo reserve ya bauxite na wawekezaji ambao watakuwa tayari kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna hoja ya Ndugu yangu Mheshimiwa Issaay ambaye naye aliweza kutualika. Pia alitoa ushauri wa kuendelea kutoa ruzuku kwa wachimbaji wetu wadogo. Nimhakikishie tu kwamba suala hili tunaliangalia ili kuweza kupata utaratibu mzuri ambao utaweza kuwanufaisha wachimbaji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja nyingine ambapo Waheshimiwa Wabunge walishauri STAMICO iachie maeneo ambayo haiendelezi. Napenda tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, tayari kwa upande ule wa mgodi wa Buckreef tumeshaainisha mgodi ule au eneo la Lwamgasa South II pamoja na Nyamalimbe II na Lwamgasa West na hayo tutaendelea kuyatambua na kuweza kuwatengea wachimbaji wetu wadogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja pia ya Mheshimiwa Ngalawa ambaye alipendekeza GST wajengewe uwezo iliwaweze kufanya utafiti zaidi katika suala hili la uchimbaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa pia kuna hoja ya Mheshimiwa Mussa Mbarouk kuhusiana na Chuo cha Madini kuongeza idadi ya wanafunzi ili kuweza kupata wataalam zaidi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mussa Mbarouk kwa mwaka huu wa fedha tumepata wanafunzi 542 lakini kuanzia Julai tutakuwa na wanafunzi 850 na lengo letu ni kuhakikisha kwamba ifikapo 2019/2020 tunakuwa na wanafunzi 1,350.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zaidi tumeanza mashauriano na Bodi yetu ya Mikopo ili kuona ni namna gani sasa wanafunzi wale wanaosomea cheti na diploma katika sekta ya madini katika Chuo chetu cha Madini na wenyewe waweze kunufaika na mkopo huu wa elimu hiyo. Naenda kuwaalika Waheshimiwa Wabunge, ndugu zenu lakini zaidi wapiga kura wenu waweze kukaribia katika Chuo chetu cha Madini ili kuweza kujifunza katika sekta hii ya madini ikiwemo jiolojia na masuala mengine ya uhandisi na uchenjuaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja kuhusiana na usimamizi wa ufuatiliaji wa walipa kodi katika sekta ya madini. Napenda tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, tutafanya hivyo na tutashirikiana na taasisi zingine ili kuhakikisha kwamba Serikali inapata kodi zake stahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Alhaj Bulembo pia aliweza kutupa ushauri kwa Tume yetu mpya ya Madini ili iweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu na zaidi itahitaji ushirikiano mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja ya Mheshimiwa Seif Gulamali kuhusiana na usafirishaji wa carbon kutoka Geita ambapo yeye alitolea mfano carbon ambayo ilikuwa ikienda Mwanza. Nitaomba Waheshimiwa Wabunge kwenye eneo hili mnisikilize kikamilifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mabadiliko ya teknolojia ya uchenjuaji katika miaka ya 2000, wachimbaji na wachenjuaji wadogo wengi nchini wamekuwa wakitumia kemikali ya cyanate kwa ajili ya kuchenjua madini ya dhahabu. Ni kwa kutumia teknolojia hii ya kemikali hii ya cyanate waliweza kuchenjua madini ya dhahabu ambayo imekuwa ikihusisha utumiaji wa vat leaching pamoja na activated carbon.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi nisingependa kwenda kwenye utaratibu mzima wa namna ambavyo vat leaching hii na carbon inafyonza dhahabu lakini napenda tu kusema kwamba, katika suala zima la usafirishaji wa carbon kutoka katika maeneo mbalimbali hususani Geita, Singida pamoja na maeneo mengine wamekuwa wakienda katika mkoa jirani au katika mkoa mwingine wa pili kwa ajili ya kufanya uchenjuaji. Napenda tu kusema, kuanzia leo tarehe 1 Juni, 2018 itakuwa ni kosa kwa mtu yeyote kusafirisha carbon kutoka katika mkoa ambapo mchanga au carbon inazalishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona katika televisheni wale wenye viwanda vya uchenjuaji Mwanza na sehemu zingine wakieleza na mpaka humu ndani wameandika barua yao kwamba suala hili litawakosesha ajira. Kama Serikali napenda kusema kwamba Sheria ya Madini iko wazi na kuanzia leo niombe vyombo vya ulinzi na usalama yeyote atakayekutwa anasafirisha carbon kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine achukuliwe hatua kazi za kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa suala la ajira, nitolee mfano wa eneo la Geita, miundombinu ipo, barabara zipo, umeme upo na kila kitu kipo, haingii akilini nini kishindikane wachenjuaji wale wenye viwanda vya uchenjuaji kuweka viwanda vyao vya uchenjuaji Geita, Singida, Tanga na maeneo mengine? Ni marufuku kuanzia leo tarehe 1 Juni, 2018, yeyote atakayekamatwa anasafirisha carbon hiyo kutoka katika eneo moja kwenda lingine hasa mkoa mmoja kwenda mwingine itakuwa ni kosa la jinai. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona nisisitize hili, lengo hapa ni kuhakikisha tunalinda ajira katika mkoa husika unaozalisha carbon ile pamoja na mchanga ule wa madini hususani madini ya dhahabu na mengineyo. Lengo kubwa ni kuhakikisha kwamba tunaongeza mzunguko wa fedha na tunadhibiti utoroshwaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wengi wamekuwa wakitoa dhahabu Geita, Singida kwenda Mwanza na maeneo mengine lakini unashangaa katika record zetu Wizara ya Madini huoni record za mauzo yale ya madini, huoni record za vibali tunavyovitoa vya mauzo ya madini yale nje, huoni record ya malipo ya mirabaha na kwa kweli tumekuwa tukipoteza fedha nyingi katika eneo hili. Niombe sana vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vihakikishe vinalisimamia suala hili ili kupiga marufuku na kuhakikisha suala hili linafika mwisho na ni imani yangu tutapeana ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zaidi niwaombe TRA pamoja na Ofisi zetu za Madini kufanya ukaguzi wa kina na forensic audit kwa wote ambao walikuwa wakifanya uchenjuaji au walikuwa wana viwanda hivyo vya uchenjuaji na kufuatilia minyororo mizima ya biashara yao hiyo katika viwanda vya uchenjuaji ili kuhakikisha kwamba Serikali inapata fedha na malipo yake stahiki. Lengo letu kubwa ni kuhakikisha kwamba tunachochea ukuaji wa uchumi katika maeneo husika ambako michanga hiyo na carbon zinazalishwa katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka tuone mabenki katika maeneo hayo, huduma zingine zipo, malazi yapo, bidhaa zipo sasa unajiuliza, iweje mtu atoe carbon Geita aipeleke Mwanza, iweje mtu atoe carbon Tanga aipeleke Mwanza? Kwa nini asiichenjue pale au kwa nini asiwezekeze pale? Endapo atashindwa kuwekeza wako wengine ambao wako tayari kuwekeza na wameonyesha nia hiyo. Kwa hiyo, napenda sana kusisitiza eneo hili na ni imani yangu Ofisi zetu za Madini pamoja na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vitalisimamia agizo hili kikamilifu ili kuhakikisha kwamba tunaweza kuona tija na ufanisi katika susla zima la uchenjuaji na sekta hii ya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuwahamasisha wachimbaji wote na wawekezaji watakaoguswa na agizo hili, waweze kujenga mitambo na miundombinu ya uchenjuaji katika mikoa ambayo wanazalisha hiyo carbon pamoja na michanga ili kuweza kutekeleza agizo hili ipasavyo. Pia nizitake Ofisi za Madini zishirikishe kikamilifu vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ili kuweza kusimamia shughuli za uzalishaji wa madini kwenye maeneo husika. Nipige marufuku kuanzia leo kwa Ofisi zetu za Madini kutoa kibali cha usafirishaji wa carbon pamoja na michanga hiyo kutoka katika mkoa mmoja kwenda katika mkoa mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja hapa kuhusiana na ruzuku katika awamu yetu ya I na ya II ya SMMRP. Wapo ambao walitaka kujua ni Mikoa mingapi imeweza kunufaika na mikopo hiyo. Napenda tu kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge, ni mikoa takribani 24 yenye wanufaika takribani 115 ndiyo walioweza kunufaika na mkopo wetu wa SMMRP.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshukuru Mheshimiwa Mwambalaswa kwa ushauri wake mzuri ambao ameendelea kutupatia kuhusiana na namna ya kusimamia sekta yetu ya madini katika Wilaya yake ya Chunya na katika eneo lake la Itumbi. Kipekee tunamshukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa mapendekezo yao mazuri pamoja na ushauri. Niwahakikishie mimi pamoja na wenzangu tutayafanyia kazi na wakati wote tutaweza kutii maelekezo yenu na ushauri na tutakapoona tuna changamoto tutaweza kurudi kwenu na tutaomba basi muweze kutuwezesha ili kufanikisha yale tunayoyahitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niliona kwa leo nieweze kuyasema hayo. Kwa wale ambao tutakuwa hatujaweza kuwajibu vizuri, tutaomba tuweze kuwajibu kwa maandishi kwa siku za usoni. Kwa kipekee kabisa tuwaombe waweze kutupitishia bajeti yetu hii ili tuweze kuwa na nguvu kuweza kutekeleza na kusimamia sekta hii nzito ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, kipekee kabisa, naomba kutoa hoja.