Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Wizara hii nyeti sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri wote wawili pamoja na Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii sekta ya madini mimi nilitarajia ingechangia kiasi kikubwa sana cha pato la Taifa lakini nasikitika kwamba inachangia 4.8% tu wakati madini tunayo mengi sana hapa nchini. Mheshimiwa Waziri itabidi alieleze Bunge hili kwa nini sekta ya madini inachangia kidogo sana katika pato la Taifa? Nadhani madini mengi yanatoroshwa na ndiyo maana sekta hii inachangia kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nashauri kwamba maeneo yote ambayo wanachimba madini basi wale wananchi wanufaike, angalau watengenezewe barabara, wajengewe shule, zahanati, lakini hawanufaiki na jambo lolote wanaachiwa mashimo tu. Wilaya ya Mpwapwa ina madini, kuna rubi eneo la Winza, copper eneo la Kata ya Mlembule na Kata ya Matomondo, Vijiji vya Tambi, Mlembule Nnana, Majami, Mwenzele wanachimba sana copper. Ukienda kwenye vijiji vile hakuna chochote, barabara haitengenezwi wala hawawasaidii wananchi kwenye suala zima la shule.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri vilevile hawa wachimbaji wadogo wadogo hebu tuwaangalie, tuwape vifaa vya kisasa, tuwape mikopo ili waweze kuboresha uchimbaji wao kwa sababu wanafanya kazi katika mazingira magumu sana. Kwa hiyo, nakuomba Mheshimiwa Waziri, wapewe mikopo ili waweze kununua vifaa vya kisasa na si kuchimba kwa kutumia sululu na majembe waweze kuchimba na mitambo ya kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa umenipa dakika tano, nakushukuru sana, huo ndiyo mchango wangu. Naunga mkono hoja hii kwa asilimia 100, ahsante sana.