Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Ahmed Juma Ngwali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ziwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AHMED JUMA NGWALI: Mheshimiwa Spika, mimi jina langu naitwa Ahmed Juma Ngwali, siitwi Ahmed Ali Ngwali.
Mheshimiwa Spika, sihitaji makofi wala sihitaji vijembe. Nimekuja hapa na nimesimama hapa nina jambo langu ambalo naiomba Serikali inisikilize kwa umakini. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna Sheria ya Wakfu, (Commission Ordinance) ya mwaka 1953, Sheria hiyo ikafanyiwa marekebisho mwaka 1956. Ilikuwa Sheria namba 7 na ikafanyiwa marekebisho ikawa Sheria Namba 9. Jambo la kushangaza, sheria hiyo mpaka leo ipo, Sheria hiyo inahusu Wakfu ya Waislamu. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Kwanza Mwalimu Nyerere akaiacha hiyo commission hakuwahi kuiunda pia Mheshimiwa Rais Mwinyi akapita hiyo commission haikuundwa, akapita Rais wa Tatu Mheshimiwa Benjamin Mkapa pia hiyo commission haikuundwa na Rais wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Jakaya Kikwete commission haijawahi kuundwa.
Mheshimiwa Spika, kwa hivyo mali za waislamu zimekuwa zikiibiwa. Hiyo commission ni muhimu sana kwa ajili ya maslahi ya waislamu na mali zao.
Kuna Sheria ya Mirathi ambayo ndani ya Sheria ya Mirathi sasa imeingizwa sehemu ya Sheria ya Wakfu ambayo imeeleza mambo mengi. Inashangaza sana! Sheria ya Wakfu ipo halafu ikatiwa ndani ya Sheria ya Mirathi.
Mheshimiwa Spika, mirathi na wakfu ni mambo mawili tofauti, hayafanani!
SPIKA: Mheshimiwa Ngwali, neno moja dogo tu….
MHE. AHMED JUMA NGWALI: Naam.
SPIKA: Umesema mali za waislam zinaibiwa tukashtuka, ni kitu gani? Unaweza ukafafanua kidogo?
MHE. AHMED JUMA NGWALI: Tunakwenda, tulia…
SPIKA: Ni jambo kubwa hilo!
MHE. AHMED JUMA NGWALI: Mheshimiwa Spika, tulia!
Mheshimiwa Spika, nirudi hapo ambapo unapotaka sasa, kwasababu tu hii commission ya kusimamia mali za waislamu….
MHE. DKT. SULEIMAN ALLY YUSSUF: Mheshimiwa Spika, Taarifa!
SPIKA: Mheshimwa Ngwali pokea Taarifa.
TAARIFA....
MHE. AHMED JUMA NGWALI: Mheshimiwa Spika nimepokea vizuri na muda wangu nilindie.
Mheshimiwa Spika, tunachosema sasa ni kuiomba Serikali, hii commission ya Wakfu ianze kufanya kazi, kwa sababu sheria tayari ipo na kila kitu kipo, waislamu wengi wanapata shida na kuchelewa kwa Serikali kuanzisha wakfu hii kumesababisha mali za wakfu zilizowekwa waislamu hawajui ni kiasi gani zilikuwepo, kiasi gani zilizopo sasa, zilizouzwa na zilizofanyiwa mambo mengine. Kuna waislamu wengi wanataka kuweka mali lakini kwa sababu commission bado haijaundwa ni shida sana wanaogopa mali zao kupotea, hata mimi nataka kuweka wakfu.
Mheshimiwa Spika, katika hili tunaiomba Serikali kwa nia njema kwa sababu Serikali ina nia njema, hii sheria ipo, hawajaifuta, siyo tu kwamba hawajaifuta, wameitengenezea utaratibu mwingine mzuri ili kupitia katika Sheria ya Mirathi waislamu waweze kufaidika na hiyo Sheria ya Mirathi.
Mheshimiwa Spika, ikiwa Wakoloni mwaka 1953 walikuwa na sheria hii, wala jambo hili siyo la dini, jambo hili ni la kisheria. Wakoloni ndiyo waliokuja na dini, wao ndiyo waliokuwa na dini, kwa nini waliweka utaratibu kwamba watu hawa waisalmu waishi hivi na watu hawa wa dini nyingine waishi hivi, hivyo tunaiomba Serikali kwamba kama Rais hajateua au kama kateua atuambie hao watu aliowateua katika hiyo commission ni akina nani na kwa mujibu wa ile sheria Rais anayo mamlaka ya kuchagua siyo chini ya watu nane na katika hao watu watano watakuwa waislamu, pia Rais atachagua Mwenyekiti atateua na Katibu. Vilevile Rais atachagua kwa mapenzi yake anayoyaona na Tume ile inaweza kukaa kwa muda ambao Rais atapenda. Katika hali hiyo tunaiomba Serikali hii Tume ianzishwe.
Mheshimiwa Spika, suala la pili, nataka kuzungumzia Sheria ya Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo. Sheria hii inafanya kazi vizuri sana kwa upande wa Tanzania Bara lakini kwa upande wa Zanzibar hii sheria ni tatizo.
Kwa mfano, fedha zikitoka Hazina ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinakwenda katika Ofisi ya Makamu wa Rais, zikitoka Ofisi ya Makamu wa Rais zinakwenda Hazina Zanzibar, zikitoka Hazina Zanzibar zinakwenda kwa Makamu wa Pili wa Rais, zikitoka kwa Makamu wa Pili wa Rais zinakwenda kwenye ofisi ya Haji Omar Kheir, Tawala za Mikoa na Vikosi vya SMZ, zikitoka hapo ndiyo ziingie katika Halmashauri za Majimbo. Sasa hii inashangaza sana, huo mlolongo hata hizo fedha zikifika inakuwa ni muda mrefu sana.
Mheshimiwa Spika, jambo lingine baya zaidi ni kwamba pesa zile hazikaguliwi kwa sababu Mdhibiti na Mkaguzi wa Mahesabu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano hawezi ku-cross over akaenda kukagua Hazina ya Zanzibar. Kwa hiyo, kwa miaka mitano fedha zile au kama ushahidi kuna mtu alete ushahidi kama upo, miaka mitano fedha zile hazijakaguliwa! Mwisho wa siku wanakuja watu kutoka katika Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais na karatasi zao eti wanakagua fedha ambazo zinatoka katika Hazina ya Jamhuri ya Mungano na ni fedha za Muungano. Wala sheria haijasema mahali popote kwamba mwenye mamlaka ya kwenda kukagua zile fedha ni mtu fulani kwa hivyo zile fedha za Serikali zinapotea, Serikali yenyewe ipo na haina habari! Naomba Serikali kwenye jambo hilo walitazame vizuri na sisi tutaweka input zetu katika kuleta maerekebisho ya sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo lingine nataka kuuliza ambalo ni dogo tu, ile Mahakama ya Kadhi imefikia wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Serikali tunataka mtuambie tu kwamba ile Mahakama ya Kadhi imeshindikana, haipo ama vipi kwa sababu ile mimi naithamini sana kwa sababu iliahidiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2010-2015 ikasema kwamba ile ni moja katika mkakati wa Chama cha Mapinduzi kuhakikisha kwamba Mahakama ya Kadhi inasimama.
Mheshimiwa Spika, nashukuru.