Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu Subhanahu-wataala kwa kutujalia kufika siku ya leo na kutoa mchango wetu Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, nimpe pole Mheshimiwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, wananchi wa Buyungu, wanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na familia ya Mheshimiwa Mwalimu Kasuku Bilago kwa kuondokewa na mpendwa wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma taarifa ya Kamati ya Nishati na Madini humu ndani kuna tatizo kubwa la STAMICO (Shirika letu la Madini la Taifa). STAMICO haina mtaji, imekabidhiwa jukumu kubwa sana la kusimamia madini katika nchi hii lakini Serikali haijawahi kuipa STAMICO mtaji wa kutosha wa kufanya shughuli zake. Matokeo yake nchi imekuwa kichaka cha watu kupora madini yetu kwa sababu hatujaijengea uwezo mkubwa STAMICO wa kusimamia rasilimali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, shirika hili la umma ambalo ndiyo lilikuwa linatarajiwa kubeba dhamana kwa makampuni yote yanayokuja kuwekeza kwenye madini kwenye nchi hii, angalau shirika hili liwe ndiyo shirika kiongozi, lakini limetupwa na limeachwa yatima. Jambo ambalo limesababisha sasa kuzaliwa kwa makampuni mengi feki na kuchukua rasilimali za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hii ilianzisha Kampuni inaitwa Meremeta ambayo siku za nyuma aliyekuwa Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Kayaza Pinda aliliambia Bunge mwaka 2008 kwamba Kampuni hii ni ya Usalama wa Taifa na Kampuni hii inamilikiwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania, akakataa kutoa taarifa ya Kampuni ndani ya Bunge hili. Kampuni ya Meremeta ilithibitika kwamba asilimia 50 ya wanahisa wake ni watu kutoka nje na kwa hiyo kwa vyovyote vile haiwezi ikawa Kampuni ya Jeshi la Wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Wananchi lilishajiondoa tokea mwaka 2002 baada ya Kampuni ya Meremeta kurudishwa Hazina kwa Msajili wa Hazina. Hadi kufikia Juni, 2008 kampuni ya Meremeta ilikuwa na Dola za Marekani zaidi milioni 80 katika akaunti yake iliyofunguliwa Benki ya NBC kule Musoma, karibu zaidi ya bilioni 200. Fedha ambazo ni za walipa kodi wa nchi hii na hazijulikani zilivyotumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato wa makampuni ya nje kujiingiza katika biashara ya ndani bila kuisaidia STAMICO kusimamia miradi ya madini nchini hatutaweza kufika popote. Kila mwaka tutakuwa tunaibiwa, kila mwaka tutakuwa tunapiga kelele lakini njia pekee ya kusaidia Taifa hili ni kuimarisha STAMICO. Njia pekee ya kuondoka hapa tulipo ni kuimarisha STAMICO.

Mheshimiwa Naibu Spika, wageni wanakuja hapa wanachimba madini yetu wanaondoka, wanaacha mashimo, wanaacha uharibifu wa mazingira hakuna mtu nyuma anayeweza kusimamia. Kama STAMICO ingekuwa ndiyo shirika letu umma, linamiliki zaidi ya asilimia 50 ya hisa kwa makampuni ambayo yanakuja kuchimba, maana yake kwamba jukumu hili angekabidhiwa STAMICO. Leo ukienda kule Nzega kuna kampuni imechimba madini imeondoka imeacha mashimo, imeacha uharibifu wa mazingira, wananchi wanateseka, leo mzigo unabebwa na Serikali na kampuni haikulipa kodi imeondoka, mambo kama haya nchi hii haiwezi kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma ripoti ya Kamati, kuna mgodi mmoja uko Mara umetajwa humu, Jeshi la Wananchi limezuia ile kampuni iliyopewa kazi ya kuchimba madini isifike kwenye mgodi. Mimi nilipongeze Jeshi kwa hatua hiyo, nchi yetu Jeshi letu limetumiwa kama kichaka cha watu kuja kuchukua fedha zetu. Kwa hiyo, ni lazima uchunguzi ufanyike kama Jeshi limefunga mkataba na kampuni fulani, huo mkataba uonekane, maslahi ya Taifa letu yaangaliwe kwanza kabla ya kitu chochote kile. Tusije tukatumia Jeshi tukaonekana tunaficha baadhi ya vitu kutumia Jeshi ili vitu hivyo viweze kuondoka kiurahisi kwa sababu Bunge hili au Wabunge hawa hawana mamlaka ya kuingilia mambo ya ndani ya Jeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni jambo la kusikitisha sana kwamba katika kitabu kizima cha Waziri na Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, hakuna mahala popote palipozungumzwa makinikia kwa ufasaha wake. Tulitegemea Bunge letu lipewe taarifa ya kina ya mazungumzo yanayoendelea kati ya Serikali na makampuni ya Accacia na mengine ambayo yaliambiwa na TRA hayakulipa kodi ya zaidi ya shilingi trilioni 424. Dola za Marekani bilioni 190 ambazo tuliambiwa nchi hii ingepata kutokana na makinikia, bajeti nzima ya Serikali iliyokuja haizungumzii mahali popote jambo hilo na katika ripoti ya Waziri hakuna mahali popote ambapo amezungumzia jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mmoja wa Wajumbe au Mwenyekiti wa hiyo Kamati yumo humu ndani Profesa Kabudi atuambie makinikia yamefikia wapi. Mchanga ambao ulizuiwa bandari umeondoka? Kama bado upo, upo mpaka lini? Je, leo migodi inasafirisha mchanga kwenda nje ya nchi? Kiwanda cha kuchakachua ule mchanga kinajengwa lini ili Watanzania ambao walikuwa na matumaini ya kupata elimu bure, kila Mtanzania aendeshe Noah yake mwenyewe kwa fedha hizi, kila Mtanzania apate matibabu bure kwa fedha hizi, kila Mtanzania aweze kuishi maisha mazuri kama ambavyo nchi nyingine zinaishi kwa fedha hizi, fedha hizi shilingi trilioni 424 zinapatikana lini? Bajeti ambayo ni zaidi ya miaka 10 ya bajeti ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili ni muhimu sana tukaelezwa Watanzania makinikia yako wapi. Mazungumzo yamefikia wapi, fedha hizi zinapatikana lini ili sisi tupate kuwaambia wapiga kura wetu kwamba kila Wilaya, kila Kata itapata Kituo cha Afya kwa sababu kuna shilingi trilioni 424 bajeti ya miaka 10 ijayo ya Serikali hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizi ni nyingi sana na kama tumeibiwa kwa kiasi hiki ni lazima Serikali ijiangalie vizuri. Mimi niwashauri njia pekee tusipige danadana, tuimarishe Shirika la Taifa la Madini (STAMICO), tulipe mtaji...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.