Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa hii. Vilevile nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Madini pamoja na Manaibu wake na Katibu Mkuu kwa hotuba nzuri sana iliyosheheni maelezo ambayo kwa kweli ni mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kwa kuanza na suala zima la kumshukuru Rais kwa maono yake kuhusiana na rasilimali za Taifa letu. Amechukua uthubutu wa hali ya juu na amepata vipingamizi vingi lakini mwisho wake tunaona kwa nini alikuwa anaelekea huko. Kwa kweli lengo kubwa ni kuhakikisha kuwarasilimali tulizonazo zinatufaidisha kwanza wenyewe Watanzania kabla ya watu wengine. Hatua zilizochukuliwa kwa kweli tunaziona kuwa zitatuboreshea mikataba na utendaji mzima wa sekta hii muhimu ya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile nizungumzie suala zima la wachimbaji wadogowadogo. Wachimbaji wadogo kama ambavyo wachangiaji wengi wameeleza ni sehemu kubwa na ya muhimu sana katika sekta hii ya madini, lakini wanafanya kazi katika mazingira magumu sana na kwa kuwezeshwa na Serikali wanaweza wakajikwamua kiuchumi na wakachangia vikubwa zaidi katika Pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi ambayo wachimbaji wadogo wanafanyia kazi ni kama ya kubahatisha, ama wawe na leseni au wakiwa hawana lakini bado wanahamahama kwa kubahatisha kuwa labda hapa nitapata. Serikali iwaunganishe na wale wanaofanya geo- survey ili wanapopata leseni zile ziwe tayari zimeainisha madini yaliyoko ndani ni kiasi gani ili hata wao wenyewe wanapotia nguvu yao pale wawe na uhakika wa kupata mapato vilevile kuchimba kwa njia ambayo haiharibu mazingira yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala hilohilo la wachimbaji wadogo, wengi sana wanatumia nyenzo duni. Natambua sana hatua zilizochukuliwa na Serikali za kuwapa mitaji kwa njia ya ruzuku lakini kama ilivyo haitoshelezi. Wachimbaji wadogo wanaoomba leseni ni wengi na mahitaji yao ni makubwa. Kwa kupitia shirika zao zile mbalimbali, basi Serikali itafute njia ya kuhakikisha kuwa wanawaletea vifaa vinavyofaa, wanawapa mafunzo ya kutosha lakini maeneo wanayotengewa yawe ni maeneo yenye rutuba kwa maana ya madini ya kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za nyuma kulikuwa kuna utaratibu wa Benki Kuu kununua dhahabu, ule utaratibu wenyewe haukuwa mbaya isipokuwa uligubikwa tu na tatizo kidogo mwishoni. Nafikiri ni wakati mzuri sasa wa kuangalia jinsi gani tunaweza tukarudisha mfumo ule. Wachimbaji wadogo wengi sana walikuwa wananufaika na ule mfumo kwa sababu walikuwa na soko la uhakika la dhahabu yao na ilikuwa inawezekana kupimwa wakajua thamani yake na inawasaidia hata wao wenyewe kwenda kupata mikopo kwa sababu tayari wana dhahabu mkononi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda hilo suala liangaliwe kwa sababu nchi nyingi na benki nyingi za dunia wananunua dhahabu mpaka sasa hivi. Sasa hivi tunaweza tukaingia ubia na wawekezaji ambao wao kazi yao itakuwa kuthamini hiyo dhahabu, kuihakiki na Benki Kuu inakusanya pesa inayotokana na hiyo dhahabu lakini vilevile kuihifadhi. Hii itakuwa ni njia mojawapo ya kuthaminisha dhahabu yetu na kutuweka katika hali ambayo kama Taifa kuwa na pato la kutosha hata kukopesheka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la makaa ya mawe. Tuna makaa ya mawe mengi sana nchini, tukianzia Ileje au Songwe, Ludewa, Ruvuma, Njombe, kote huku tuna machimbo mengi ya makaa ya mawe, inasikitisha kuwa mpaka sasa hivi uendelezwaji wake umekuwa wa kusuasua. Hiki ni chanzo muhimu vilevile kwa masuala ya viwanda na uzalishaji wa nishati ya umeme. Kwa hiyo, napenda sasa hivi tufikie mahali ambapo Serikali inajikita kwa nguvu zaidi katika kuwekeza kuchimba makaa ya mawe ambayo ni muhimu sana tunapoelekea uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua vilevile kuhusiana na STAMICO. STAMICO imepigiwa kelele sana, imelalamikiwa sana lakini STAMICO kama mnavyojua Mashirika ya Umma mengi ambayo yalikuwa yamepewa majukumu ya kuendesha shughuli mbalimbali, ni mojawapo ya mashirika ambayo yamekuwa hayapati fedha ya kutosha kuendesha shughuli zake. Tutawalaumu bure STAMICO hapa wakati kumbe hatuwawezeshi. STAMICO ina wataalam wazuri sana, ina miradi ilikuwa mizuri sana, kama walishindwa ni kwa sababu hawajawezeshwa vya kutosha. Sasa hivi Serikali ihakikishe kuwa STAMICO inapewa fedha ya kutosha, inasimamia vizuri migodi na miradi ambayo iko chini yake ili ilete tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka kuzungumzia Mkoa wangu wa Songwe, hususani Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira. Kumekuwa na sintofahamu ya muda mrefu sana kuhusiana na Kiwira, mara mwekezaji anakuja, mara wanasema hatoshi, mara inakuwa hivi mara vile. Sasa hivi tunaambiwa tangu Aprili mwaka uliopita STAMICO wameanza kufanya majaribio ya kuchimba makaa ya mawe na wameanza kuyauza. Napenda kujua sasa kama hiyo itakuwa ni mwendelezo na mikataba gani imeingiwa kati ya STAMICO na Wilaya yangu ya Ileje na Mkoa wetu wa Songwe kwa ujumla na nini tutegemee katika suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nitoe ombi kwa Wizara, tuna daraja dogo sana pale linalounganisha Mgodi wa Kiwira na Wilaya ya Ileje ambalo lingetoa fursa ya mkaa ule kusafirishwa lakini halifanyi kazi kwa sababu limekatika. Je, Serikali kwa kupitia Wizara hii wanaweza wakahakikisha kuwa wanatengeneza hilo daraja la kilometa 7 tu ambalo litawezesha sasa kupitika na makaa ya mawe yaweze kupita pale badala ya kuzungukia Kyela ambako ni mwendo mrefu zaidi na hasa tukiangalia kuwa mkaa huu unapelekwa Mbeya Cement ambako ni rahisi zaidi kupitia upande wetu wa Ileje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kujua ubora wa makaa haya. Mara tunaambiwa hayafai, mara tunaambiwa yanafaa, mara tunaambiwa yana ubora zaidi kuliko hata yale ya Afrika Kusini mara tunaambiwa sijui yakoje. Naomba tupate takwimu sahihi kujua kama kweli yana ubora gani na hatua zinazotegemewa kuchukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie sasa suala zima la watoto wadogo wanaofanya kazi katika migodi nchi nzima. Kwa kweli hili ni janga na hizi ajira za watoto kwenye migodi zinaathiri sana watoto kiafya vilevile kielimu. Watoto hawa hawaendi shule kwa sababu wanatumika kwenye migodi na sehemu wanazofanyia kazi watoto hawa ni hatarishi sana. Mashimo tu ambayo hayana kinga aina yoyote wanadumbukizwa kule kwa sababu wao kwa udogo wao ni rahisi kupenya matokeo yake wanaathirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya yote wanaathirika na zebaki wanayotumia kuchenjua ile dhahabu. Wengi sasa wamegundua kama wakienda kuchezacheza na ule udongo wakatia zebaki kidogo wanaweza wakaambulia vijiwe vya mawe ya dhahabu kwa hiyo wanafanya hivyo, lakini hii ina madhara makubwa sana kwao. Napenda Serikali kwa umoja wao kwa mfano, Wizara ya Madini, Wizara ya Elimu, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, wote washirikiane kuona jinsi gani watahakikisha kuwa watoto wadogo hawafanyi kazi katika migodi ili waendelee na masomo kama kawaida na watakapokuwa wakubwa basi wataingia katika kazi hizi za migodini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusiana na wanawake. Wanawake wengi wamependa na wao kujiingiza katika shughuli za migodi lakini mazingira siyo rafiki kwao na vilevile na wao wanapata matatizo kama yale ya wachimbaji wadogo kwa vifaa duni na mitaji ni midogo. Kwa hiyo, wao pia kama kundi maalum la wazalishaji wangesaidiwa kwa sababu wana umoja wao tayari ambao unawawezesha na wao kuhusika katika biashara hii ya migodi. Tungependa kuona hilo likifanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zaidi ya yote tunaomba sana data tupate kujua mawe ya aina gani, yana thamani gani, tunayo mengi kiasi gani na vito vya aina gani, vina thamani kiasi gani, tunayo kiasi gani. Hii kwanza moja kwa moja itatusaidia kama Taifa kujua utajiri wetu na kutuwezesha kuwa na ulinganisho mzuri duniani hata katika masuala ya mikopo na masuala mengine ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo napenda sana tuwe na takwimu za kutosheleza kuhusiana na rasilimali tulizonazo nchini. Kwa sasa hivi tunazungumzia madini lakini naamini ni kwa rasilimali zote ambazo Tanzania tunazo na ambazo kwa kweli Mungu ametupendelea na kutupatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni yangu yalikuwa ni hayo, nilikuwa nataka tu kuhimiza suala zima la rasilimali hizi zianze kusaidia Watanzania kwanza na kama ni suala la sera kila mtu alielewe vizuri na ionekane pale ambapo kuna mapungufu basi turekebishe ili mwisho wa yote madini yetu yabakie nchini na yaweze kusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kuyeyusha (smelting). Tumeambiwa kuwa tunajitahidi kwa kadri iwezekanavyo madini yasipelekwe nje yakiwa ghafi, lakini bado hatuna smelters za kutosha kuweza kuhakikisha kuwa hilo linafanyika. Tungependa Serikali ifanye makusudi kabisa kuwekeza katika suala hili kwa sababu hiyo ndiyo itakuwa njia pekee ya kuzuia madini kutoroshwa nje kwa njia ya magendo.