Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri wake kwa kuwasilisha taarifa yao ya mapato na matumizi kwa kipindi hiki cha 2018/2019. Pia nichukue nafasi hii kuwapongeza Mawaziri hao kwa sababu wanafanya kazi kama timu na nimeshuhudia katika kipindi kifupi tu kazi ambazo zinafanyika za usimamizi wa rasilimali hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kwa dhati kabisa nimpongeze Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa anayoifanya ya kusimamia rasilimali hii ya madini, kwa kweli anastahili pongezi zote. Kwa kila namna tuendelee kumuombea dua njema Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya nzuri, afya njema ili aweze kusimamia majukumu yake ambayo yanaleta faida katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze pia Wizara ya Madini kwa usimamizi, kwa muda mfupi wameweza kuongeza mapato kwa zaidi ya asilimia 120. Hii ni kazi nzuri na wameweza kusimamia vizuri na kwa mabadiliko haya ya sheria ambazo tumezipitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie Mkoa wa Lindi. Katika Mkoa wa Lindi tumebahatika kuwa na madini mbalimbali. Tunayo ruby, sapphire, graphite, gypsum, chokaa, chumvi na dhahabu lakini niseme Serikali bado haijafanya maamuzi ya kuweka mazingira wezeshi ya kusimamia rasilimali hizi za madini ambazo zipo katika Mkoa wa Lindi ili ziweze kunufaisha Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali wameweza kutoa leseni kwa wawekezaji hawa wa graphite ambao wako Ruangwa. Tunategemea sasa waanze mara moja uchimbaji huu wa madini ili wananchi wa Ruangwa waweze kupata ajira lakini uchumi wetu pia uweze kukua katika Mkoa wetu wa Lindi na hatimaye Serikali yetu iweze kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo gypsum ambayo ipo Kilwa katika eneo la Kiranjeranje, Hoteli Tatu na maeneo mengine. Hii gypsum ina ubora wa kidunia, ni suala la kujivunia kwamba tuna rasilimali ambayo ipo katika soko la dunia lakini bado Serikali haijatilia mkazo katika usimamizi wake na kuweka mazingira wezeshi kuifanya Serikali yetu iweze kupata mapato. Sasa hivi kuna uchimbaji tu ambao upo kiholela, kwa hiyo, tunapoteza mapato mengi sana kupitia madini haya ya gypsum. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali kusimamia uwekezaji huu wa gypsum ili Serikali iweze kupata mapato lakini pia wananchi wa Mkoa wa Lindi tuweze na sisi kukuza uchumi wetu kupitia hii gypsum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna wazalishaji wengi wa chumvi nchini Tanzania lakini na kwetu Lindi tuna wazalishaji hao wa chumvi lakini tuna changamoto mbalimbali katika eneo hili la chumvi. Wadau hao wa chumvi mara nyingi wamekuja kuleta kilio chao kwa Serikali lakini bado hatujapata nafasi ya kuwasaidia. Naiomba sana Serikali kuwatazama kwa macho mawili ili wazalishaji wa chumvi nao waingie katika ushindani wa soko na tuweze kuwa na viwanda vya chumvi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa chumvi kuna tozo mbalimbali. Ziko tozo ambazo zinatozwa kupitia halmashauri kati ya asilimia 5 - 10 lakini bado utakuta wanunuzi wa chumvi wanaposafirisha njiani tena wanakumbana na tozo zingine mbalimbali. Pia kuna ushuru wa mikoko ambao unatozwa na Wizara hii ya Maliasili na Utalii lakini cha kusikitisha tozo hii inatozwa eneo lote la mikoko. Kwa hiyo, mimi naishauri Serikali tozo hii wangeelekeza katika eneo lile ambalo linazalisha chumvi kuliko kutoza katika eneo zima la mikoko. Tozo hii inatozwa katika kila ekari mbili na nusu Sh.130,000, kwa hiyo bado tunaona wazalishaji wa chumvi wana mzigo mkubwa ukiangalia mlolongo wote wa tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna tozo ya kuandikisha mashamba na inatozwa kila mwaka Sh.320,000 na kuna leseni wanalipia kila mwaka. Kwa hiyo, tunaona mzigo ambao upo kwa wazalishaji wa chumvi na kusababisha chumvi yetu ya Tanzania kuuzwa bei ya juu kuliko chumvi ile ambayo inaingizwa kutoka nje ya nchi. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali kuangalia baadhi ya tozo hizi ambazo zinaleta kero kwa wazalishaji wa chumvi na kufanya chumvi iwe bei ya juu basi tuweze kufanya mabadiliko ya sheria ili tuweze kuwasaidia wenzetu wazalishaji wa chumvi na tuweze kuwa na viwanda vya chumvi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao wachimbaji wa madini wanawake. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, siyo kwa kuwa yeye ni mwanamke tu lakini kuwatazama hawa wachimbaji wa madini wanawake ili Serikali sasa iwape mafunzo na iwawezeshe kwa kuwapa vitendea kazi na wao waweze kuingia katika fursa hii ambayo ipo ya madini na kupata leseni za kuwaruhusu kuingia katika uchimbaji huu wa madini. Kwa hiyo, hili ni suala muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine tunalo hili Shirika letu la STAMICO, hili shirika bado halina miguu. Naiomba Serikali kulisaidia shirika hili kama ambavyo tumeweza kuwasaidia ATC, Kampuni ya Simu, TANESCO, basi na hawa STAMICO tuone umuhimu wa kuwasaidia ili na wao waweze kupata miguu wasonge mbele. Wanayo mipango na mikakati mizuri lakini wanashindwa kutekeleza kwa sababu tu ya kukosa fedha. Kwa hiyo, hilo ni suala muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Spika wetu kwa kuteua Kamati Maalum iliyoenda kusimamia masuala mazima ya madini. Kwa kweli wamefanya kazi nzuri na tumeona mazao ya kazi ile. Bahati njema tumepata faida katika Kamati ile tumepata Mawaziri. Kwa hiyo, tuna imani kabisa na wao, nasi tunawaunga mkono katika shughuli zao mbalimbali katika kumsaidia Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, naiomba Wizara izingatie maoni na ushauri wa Kamati ya Madini. Tumeshauri mambo mengi sana na kwa bahati njema baadhi ya mambo wameyafanyia kazi, tumeyaona katika kitabu chao. Niwatakie kila la kheri katika bajeti hii, Serikali iweze kutoa fedha kwa sababu Wizara ni mpya inataka kujipanga vizuri katika kuhakikisha inasimamia rasilimali za nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.