Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Karatu ina mashamba ya mikataba 42 na mengine yamekuwa hayajaendelezwa ipasavyo na kugeuka kuwa mapori ya kuishi wanyama. Mashamba ya Tembo Tembo na ACACIA yaliyo Kijiji cha Mangola juu yameendelezwa kwa chini ya asilimia 40 na yanakosa sifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili lilishapelekwa Wizarani na hata wananchi walimsimamisha kwa mabango Waziri Mkuu alipotembelea Karatu. Tunaomba Serikali iwarudishie wananchi wa Mang’ola juu sehemu na mashamba hayo hapo juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmiliki wa shamba la ACACIA amekataa kutoa njia ya wananchi wa Mang’ola Juu kwenda Kijiji cha jirani cha Makhomba. Huu ni ukatili wa hali ya juu na kuwanyima wananchi haki ya kutembeleana; mmiliki huyo haitambui Serikali. Tunaomba Waziri awasaidie wananchi wa Mangola Juu kupata njia hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Karatu ambayo iligawanyika kutoka Wilaya ya Mbulu ya zamani ina utata wa mpaka kati yake na Wilaya ya Ngorongoro. Kihistoria eneo la msitu wa kutoka gate la Ngorongoro hadi View Point lilikuwa eneo la Wilaya ya Mbulu. Tunaomba Serikali isaidie kupata ukweli wa mpaka sahihi kati ya Wilaya ya Karatu na Wilaya ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabaraza ya Ardhi ya Kata yanafanya kazi kubwa na muhimu sana ya kusimamia haki. Bahati mbaya Mabaraza haya ya Kata bado yanafanya kazi katika mazingira magumu sana. Suala la posho zao, nauli pindi wanapokuwa kazini bado ni shida kubwa sana. Tunaomba Serikali iweke mpango wa wajumbe hao kuwa na posho ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka kati ya Wilaya ya Karatu na Wilaya ya Ngorongoro uhakikiwe. Mpaka kati ya Wilaya ya Karatu na Wilaya ya Mbulu eneo la Maseda nao uhakikiwe.