Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii ili nami nitoe mchango wangu katika bajeti hii ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Niwapongeze sana Waheshimiwa Mawaziri hawa wawili, Waziri Lukuvi na Naibu wake, dada yangu Mabula, wanafanya kazi kubwa sana kwa sisi wataalam kwa kweli wanatufurahisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizo, nina maombi mawili/matatu. Ombi la kwanza nianze na Wilaya yangu ya Manyoni. Nimejaribu kupekua kitabu hiki cha bajeti cha Mheshimiwa Waziri, nimefurahishwa sana na mipango hii kabambe ya uendelezaji wa miji na naziona juhudi katika wilaya nyingine. Hata hivyo, mara nyingine nimekuwa nikiimba sana na kuomba na kulia kwamba hebu itazameni na Manyoni katika mipango hii kabambe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalia kwa sababu Manyoni naitazama iko karibu na Dodoma, Manyoni pale ni kama hub ya mkakati wa maendeleo. Dodoma itakapojaa, mahali pazuri pa kupumulia ni pale Manyoni na si mahali pengine; kwa nini wanakuwa wanairukaruka? Nimechambua sana na naona Manyoni iko sidelined. Naomba sana wajaribu ku- concentrate Manyoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Manyoni pale tukiweka mipango kabambe tuna nafasi za viwanda, nimehangaika katika juhudi zangu binafsi, nimewasiliana na Walimu wa Morogoro, tumepatiwa wanafunzi pale, tunahangaika sana kuwalisha, kuwatunza kidogo angalau kwa bei nafuu, lakini bado tunazidiwa na juzi walikuwepo pale wameondoka jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba mkono wa Serikali basi, hebu tuipange Manyoni, kwani kuna shida gani Manyoni? Naona wanaruka tu, wakienda wanapita Manyoni kama vile hawaioni, wakati ile ni hub nzuri kwa maendeleo wapange ule mji, utatusaidia sana utasaidia maendeleo ya Dodoma hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naliongea kwa uchungu kwa sababu nimekuwa nikifuatilia kwa muda mrefu na mimi ni mtaalam; sasa ninapoona maeneo mengine yanapewa huduma lakini Manyoni inarukwa na iko karibu na ni strategic position Manyoni pale, inaniumiza na inawaumiza watu wa Manyoni. Mheshimiwa Lukuvi, naomba hebu aikumbuke Manyoni, please.


Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nalo niseme, nimeona katika ukurasa wa 45 Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi, tumeona TANAPA walivyojitoa sasa kusaidia vijiji. Nikiona namba ya vijiji vile 392, sijajua, hakuna mchanganuo, sijui kama Manyoni pia ipo kwa sababu TANAPA inasaidia hivi vijiji ambavyo vimepakana na hifadhi za misitu, wanyama. Manyoni inavyo vijiji 12, sasa sijui kama Manyoni na vijiji ndani ya Manyoni ni miongoni mwa hivi vijiji 392.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, tafadhali, kama havipo hebu wavitazame waviweke, wasiipitepite Manyoni hivi hivi, Manyoni ni Mji mzuri mno, tunauita Ghana ndogo ile. Manyoni kwa wanahistoria ndiyo wilaya ya kwanza kuwa na Mkuu wa Wilaya Mwafrika, tuikumbuke Manyoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia katika Mpango huo huo ukurasa wa 45, hawa wenzetu wa misitu, pia nao wanasaidia katika upangaji wa matumizi bora ya ardhi. Naomba pia katika vijiji 50, sijajua kama Manyoni pia ipo, watusaidie kuipanga Manyoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho niombe tu kwa ujumla kama ambavyo katika hotuba zote za bajeti za mwaka jana, mwaka juzi, mwaka huu, wanazungumza maneno mazuri sana, kwamba kupangwe matumizi bora ya ardhi katika nchi hii ili kupunguza migogoro; hebu wapunguze maneno sasa twende kwenye vitendo. Mimi napenda sana vitendo kuliko maneno, ndiyo maana huwa siongei sana, napenda sana kutenda, wakatende.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ndiyo mafupi ambayo nilikuwa nataka kuchangia. Nashukuru sana kwa nafasi hii.