Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja iliyoko mezani, lakini pia namshukuru Mungu kwa kunipa nafasi hii na wakati huo huo nawashukuru wapiga kura wa Urambo ambao wamekuwa wakinipa ushirikiano kila siku, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inanibidi nimshukuru Mheshimiwa Waziri Kamwelwe pamoja na Naibu Waziri Aweso pamoja na Katibu Mkuu Profesa Kitila Mkumbo, Wakurugenzi wote wa Wizara hii kwa jinsi ambavyo wanajitahidi kutatua tatizo hili kubwa tulilonalo nchini mwetu. Mheshimiwa Waziri ulikuja Urambo na ninakushukuru ulikuja kwa kituo, tukazunguka tukaona shida ya maji tuliyonayo Urambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwetu sisi Urambo changamoto ya kwanza ni maji na wewe mwenyewe ulishuhudia. Tulikwenda Usoke Mheshimiwa Waziri, ukaona jinsi ambavyo wanaume na wanawake wamezunguka kisima kimoja, wote wanasubiri maji yajae kwenye kisima na kisha wanatumia neno ambalo wewe mpaka leo Mheshimiwa Waziri unalijua, wakisema amsha popo, wote kwa pamoja wanashusha ndoo ndani ya kisima, Mheshimiwa Waziri uliona. Ni jambo lilikuhuzunisha wewe mwenyewe binafsi na mimi mwenyewe, hatukuaga kwa jinsi ya uchungu tulioupata. Tukaanza kuhangaika na wewe Mheshimiwa Waziri je, tupate maji kwenye Mto Ugala ikashindikana.

Mheshimiwa Spika, niko mbele yenu ninyi viongozi wa Wizara hii kwa uchungu uliouona Mheshimiwa Waziri nakusihi, nakuomba kwa niaba ya wapiga kura wa Urambo mtupatie maji ya kutoka Lake Victoria. Wewe mwenyewe umeona hakuna mbadala, visima tunavyochimba vitoe maji kama walivyoongea wenzangu kutoka Mkoa wa Tabora maji yako chini sana. Kwa hiyo, tunapokuomba visima ni ufumbuzi wa muda tu, lakini kwa ufumbuzi wa kudumu Mheshimiwa Waziri nakusihi kwa niaba ya wananchi wa Urambo tupate maji kutoka Lake Victoria. Naomba Mwenyezi Mungu akuongoze Mheshimiwa Waziri utakapokuwa unahitimisha angalau utamke neno la kuwapa matumaini watu wa Urambo, shida ya maji ni kubwa mno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika jitihada ya kupata suluhisho la muda tuliomba kuchimbiwa visima, tukapata Mkandarasi akatuchezea akili, tukarudi kwako wewe Mheshimiwa Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara yako wakatusaidia kutuunganisha na Wakala wa Uchimbaji Maji inayoitwa DDCA. Tunaomba Mheshimiwa Waziri utusaidie, kwa kupitia wizara yako ili huu wakala unaochimba maji uje uchimbe maji angalau kwenye vijiji 17 ambavyo vina shida sana ya maji.

Mheshimiwa Spika, naamini Mheshimiwa Waziri utaisukuma hii DDCA ili angalau ilete vyombo vyake tuone tuanze kupata matumaini, kwa sababu mpaka sasa hivi hawajafika na sisi tuna shida sana ya maji na hatuombi kwamba ishindikane fedha zirudi, zishindwe kutumika katika mwaka huu wa fedha. Tunakusihi sana Mheshimiwa Waziri utuangalie Urambo kwa jicho la huruma kutokana na shida ya maji tuliyonayo.

Mheshimiwa Spika, la pili Mheshimiwa Waziri tunaona kwamba katika kupata suluhisho la muda tukisubiri mradi huo mkubwa ambao naamini Mwenyezi Mungu atakusaidia tupate kutoka Lake Victoria, tunaomba tuchimbiwe bwawa. Kuna eneo zuri sana wataalam wetu walishaleta udongo Wizara ya Maji ili upimwe udongo ule kuona aina ya udongo ambayo unaweza kufaa kwa ku-retain maji yaani kwa kutunza maji. Eneo hilo zuri sana, bonde zuri sana ukija tena tutakupeleka Mheshimiwa ukaone, lakini tutafurahi kama wakija wataalam waone eneo ambao linaweza kuchimbwa bwawa zuri sana eneo la Kalemela.

Mheshimiwa Spika, nimeona, mimi nina wivu wa maendeleo, nimeangalia kwa wenzangu wanachimbiwa mabwawa, naamini kwa jicho lako la huruma pia na sisi Urambo tutachimbiwa bwawa la maji katika eneo la Kalemela ili na sisi tuwe na chanzo kimojawapo cha kupata maji ya kutusaidia wakati tukisubiri maji kutoka kwenye mradi mkubwa ambao naamini kwa jicho la huruma utatuingiza na sisi katika huo mradi ambao unahusisha milioni kama 500 hivi za fedha za kigeni kutoka India.

Mheshimiwa Spika, mimi nachukua nafasi hii kuwaunga mkono Wabunge wenzangu wote waliotangulia kuzungumzia umuhimu wa kuwa na Mfuko wa Maji Vijijini. Tumeona jinsi ambavyo REA inafanya kazi vizuri, tunaamini tukianzisha Mfuko Maalum wa Maji Vijijini, hili suala la maji linaweza kupata ufumbuzi. Kwa hiyo, naunga mkono wenzangu waliotangulia walioongea kusema tupate angalau ushuru au jina lolote mtakalotumia wa shilingi 50 kutoka kwenye dizeli na petroli ili isaidie kuunda mfuko huo ambao tunaamini utasaidia upatikanaji wa maji vijijini.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kwa siku ya leo ni tatizo hili ambalo nadhani linahitaji si wizara moja tu, nadhani linahitaji Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wakati huo huo TAMISEMI na Wizara yako mkae pamoja muone jinsi gani ambavyo mtahakikisha kwamba tunathamini kuvuna maji ya mvua. Kwa kweli ukiangalia maji ya mvua yanavyopotea na shuleni watoto wa kike, wa kiume wote wanashindwa kupata hata maji ya kunawa mikono baada ya kwenda sehemu zile wanazokwenda. Kwa hiyo, mimi ningeomba kuwe na sheria fulani ya uvunaji wa maji ya mvua ili tuondokane na shida ya maji hasa katika maeneo ya taasisi zetu za shule na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, pengine Wizara ya Elimu inaweza ikaamua kwamba shule isifunguliwe mpaka kuwe na utaratibu wa kuvuna maji ya mvua. Kwa sababu ni jambo la kusikitisha mvua inavyonyesha hasa kwa mfano kama sasa hivi mvua inanyesha Dar es Salaam na wapi, lakini maji yanapotea, na wakati huo huo unakuta watoto hawana maji mashuleni na kwenye taasisi kama hizo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilikuwa nafikiri kuwe na kautaratibu fulani ka kulazimisha, wenzetu kwa mfano, kwa taarifa niliyonayo na nimeshuhudia nilikwenda Bamuda. Kwenye Kisiwa cha Bamuda wameweka utaratibu kwamba hujengi nyumba yako wewe ya kuishi kabla hujaonesha jinsi utakavyovuna maji ya mvua. Sasa na mimi nilikuwa nafikiri na sisi tungekuwa na utaratibu huo hasa hizi taasisi zetu isifunguliwe mpaka utaratibu wa kuvuna maji uwekwe. Wakati huo huo nichomekee na hapa hapo, maji na choo yaani kuwe na maji uvunaji wa maji na choo ndio taasisi iandikishwe. Nimechomekea hilo kwa sababu naona vinaenda karibu pamoja tu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi naomba kumalizia kwa kurudia tena kilio chetu sisi watu wa Urambo. Pamoja na shukrani zetu kwako wewe Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri ambaye pia alikuja akitokea Kigoma nawasihi mtuweke. Hata kama hamkututaja kwenye kitabu hiki muone jinsi ya kutuingiza sisi kama Urambo kwenye mradi wa kupata maji kutoka Lake Victoria kama ukombozi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru nawapongeza kwa kazi ngumu mnayoifanya lakini niko mbele yenu kuwaomba mtukumbuke Urambo, ahsante sana.