Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili nitoe mchango wangu katika Wizara hii muhimu ya Maji. Nichukue nafasi hii kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa afya na uzima tumekutana jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Spika, hakuna ziada mbaya na mimi niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara Profesa Kitila pamoja na watumishi wote wa Serikali katika Wizara hii kwa juhudi kubwa ambazo wanazifanya kwa kuwaletea maji wananchi wa Tanzania. Wote ni mashahidi tumeona kwamba wanachapa kazi na wanatembelea sehemu mbalimbali kujua changamoto za Watanzania lakini changamoto kubwa ni upatikanaji wa fedha kutoka Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niishukuru Serikali kwa miradi mbalimbali inayoendelea katika jimbo langu katika vijiji vichache. Pia nimeona humu nia ya Serikali kulijenga Bwawa la Kidunda, niipongeze sana na nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kutimiza ndoto za Mwalimu Nyerere za miaka ya 1960 ambazo anazitekeleza sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Serikali, Kidunda siyo mara ya kwanza kuiona kwenye vitabu, nimeiona mwaka juzi wakati nikiwa mwaka wa kwanza hapa Bungeni, nimeona mwaka jana nikiwa mwaka wa pili hapa Bungeni na mwaka huu pia nimeiona, lakini utekelezaji wake haufanani na kinachoandikwa. Niwaombe sana mwaka twende tukatekeleze mradi huo, ni mradi wa miaka mingi na una manufaa makubwa sana katika nchi yetu hasa kwa upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam, Pwani na Morogoro hasa kwa hivi viwanda vyetu kuwa na uhakika wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni mipango ya muda mrefu ya Mwalimu Nyerere, nikikumbuka pale Morogoro alivyotujengea viwanda zaidi ya 11 kutoka msaada wa World Bank alijenga na Bwawa lile la Mindu kwa ajili ya ku-supply maji. Kwa hiyo, tunafuata nyendo zake hata huko aliko anafurahia namna gani Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli anatimiza ndoto zake alizoziacha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi na shukrani hizo, nianze kuomba maombi ya kwenye jimbo langu. Kama nilivyosema kuna miradi michache inatekelezwa lakini kuna mambo mbalimbali niwaombe. Kuna Mradi wa Chalinze III, ni mradi wa kabla mimi sijakuwa Mbunge tangu 2009, tulipata vijiji saba, miundombinu yote ilijengwa tangu 2009 lakini mpaka leo hiyo miundombinu imeshakuwa chakavu na imeanza kubomoka hatujaweza kupata maji. Mheshimiwa Waziri unapokuja kufunga hoja yako tunataka majibu ya Chalinze III maji yatatoka lini? Mwaka jana ulisema kuna mambo mnayafanya mchakato unafikika mwisho lakini tumebakiza miezi miwili kumaliza hii bajeti bado hatuna matumaini Chalinze III itaanza kutoa maji lini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika Chalinze III hiyohiyo kuna vijiji vitatu ambavyo vilisahaulika kujengewa miundombinu yake ambavyo ni Gwata, Masewe na Lubongo. Tunaomba sana hizo hela tukamalizie hiyo miundombinu ili ikianza kutoa maji Chalinze III na sisi pale tupate maji.

Mheshimiwa Spika, pia katika Tarafa ya Ngerengere karibu kata zote hatuna maji safi na salama. Niombe wataalam wa Wizara na Halmashauri waje wafanye utafiti wa kupata maji ardhini ili tuweze kupatiwa visima katika zile kata ambazo haziwezi kufikiwa na vyanzo vya maji vya mserereko ambavyo tunavyo kule Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi kuungana na wenzangu wengi waliopendekeza kwamba tuongeze shilingi 50 katika tozo ya mafuta kwa ajili ya kuongezea Mfuko wa Maji ili tuweze kusambaza vizuri maji huko vijijini. La pili niungane na wenzangu pia waliopendekeza kwamba Wakala wa Maji Vijijini ianzishwe.

T A A R I F A . . .

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, namheshimu sana ndugu yangu, lakini nikuombe wewe muda wangu uutunze ili na mimi niweze kutoa mawazo yangu kwenye Wizara hii. Suala la export levy tutakuja kulijibu Wizara ya Kilimo ikija hapa, lakini sasa tunazungumzia masuala ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema nikubaliane na wenzangu ambao wanataka tuanzishe Wakala wa Maji Vijijini, lakini naomba nitofautiane kidogo au nitoe mawazo yangu kidogo. Tukianzisha wakala huu sasa hivi kabla hatujajua miradi ya maji imekwama wapi tutarithisha matatizo kutoka katika Mamlaka za Maji zilizoko sasa hivi na kupeleka kwenye huo wakala mpya.

Mheshimiwa Spika, pendekezo langu, kabla ya kuanzisha wakala huo, ni vizuri ama Serikali au wewe au CAG afanye ukaguzi maalum katika miradi yote ya maji nchi nzima ili tubaini tatizo la miradi hii kutekelezwa chini ya kiwango au miradi hewa ni nini? Baada ya hapo wakija na majibu na mapendekezo ndiyo Serikali ichukue na sisi Wabunge tutakuwa na uelewa mpana wa kuishauri Serikali kutoka hapa kwenye mkwamo twende wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema hivyo? Miradi mingi ambayo ilikuwa inaanzishwa na kandarasi nyingi watu walikuwa wanapeana kiujanjaujanja. Wakandarasi waliokuwa wanapewa hawana sifa wala vigezo, kwa sababu ni mtoto wa mjomba au mtu kwa sababu ana fursa hiyo iko pale anaanzisha kampuni yake, anamwambia ndugu yake weka hapa tender anashinda, uwezo hana, vifaa hana na ndiyo maana mpaka sasa hivi tuna miradi hewa na miradi mingine huko maji hayatoki.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kabla hatujaunda huu Wakala wa Maji ni vizuri kabisa kwanza tukabaini matatizo ni nini, nani alihusika na majina yao bila kujali vyeo vyao, yawe wazi ili tuisaidie Serikali tuondoke kwenye mkwamo huu wa maji tuliokwama.

T A A R I F A . . .

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Hiyo taarifa kwa sababu haina ushahidi wala uhakika nikiichukua atanirushia kesi ambayo haihusiki hapa, twende kwenye kuchangia maji tu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kuhusu washauri elekezi wa miradi ya maji, hiki ni kichaka kingine cha kutafuna fedha. Utakuta mradi wa maji wa kisima kimoja mshauri elekezi anatoka Arusha, Dar es Salaam ndiyo anakuja kusimamia kwenye halmashauri. Ushauri wangu kwa Serikali kwa sababu wana wataalam wao ndani ya Halmashauri na mkoa hata kwenye Mamlaka ya Maji, kwenye miradi hii midogo midogo ni vizuri washauri elekezi wakatumiwa hao watumishi wa Serikali ili kuokoa fedha nyingi na hawa washauri elekezi wakatumika kwenye miradi mikubwa tu kama Kidunda, Chalinze III na mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, tunalumbana hapa tatizo ni sababu ya pesa kidogo na niipongeze sana Serikali kwa kuja na mikakati ya kujiongezea pesa. Tunafahamu biashara ni uwekezaji na katika uwekezaji huo inayotuingizia mapato mengi kuliko yote ni kilimo asilimia zaidi ya 25 lakini ya pili ni utalii, watalii wanaongezeka namna gani? Lazima tupate watalii wengi na ndiyo maana Serikali imekuja na jibu la kuongeza mapato kwa kununua ndege ili watalii hawa wawe wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tulikuwa kwenye semina na wanasema watalii wengi tunaopata ni wazee, huwezi kumsafirisha mtalii mzee kwa gari kutoka Arusha kama unakuja Selous, haiwezekani, lazima atumie ndege. Niishauri Serikali siyo hizi kubwa tu wanunue hata ndege ndogo, tunaona hata wakati wa uchaguzi kuna vyama CCM na vingine tunakodisha ndege kutoka Kenya maana yake tunahamisha uchumi kuwatajirisha Kenya, ni bora zinunuliwe ndege nyingi ndogo hapa nchini tunakodisha na uchumi huo utaendelea kubaki ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wale wanaobeza suala la ununuzi wa ndege jambo hili ni la kwenda kuimarisha mapato ya Serikali kwa sababu miongoni mwa kinachochangia mapato makubwa Serikalini ni utalii kwa zaidi ya asilimia 17.6. Kwa hiyo, kwa kununua ndege hizo tuna uhakika watalii wetu wataongezeka. Tuipongeze Serikali kwa ununuzi huu wa ndege na kwa ubunifu huu wa kuongeza mapato badala ya kuwabeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.