Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kutoa mchango wangu katika hoja hii ya bajeti ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kutumia pia fursa hii kumpongeza Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya na kuipongeza timu yake ya Baraza la Mawaziri, na Watendaji Wakuu wa Serikali kwa sababu kazi ya Serikali ya Awamu ya Tano inaonekana na inasikika, mwenye macho haambiwi tazama, mwenye masikio pia haambiwi sikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana kazi kubwa aliyofanya Waziri kuandaa hotuba hii. Napishana na walisema kwamba hotuba hii ni kubwa na haina kitu, hotuba hii ni nzuri ina vielelezo vya kutosheleza, ina details za kutosha kwa wale wanaopenda details na wengine kwa sababu ya haiba zao wanapenda tu kuangalia facts, ina facts za kutosha nimeona viambatanisho ambavyo sijaona katika hotuba nyingine zilizotangulia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kugusia haya maoni ya Kamati na kwa kweli ninaiunga mkono asilimia mia moja hasa kwenye mapendekezo matatu ambayo bila hayo nafikiri bado tutasuasua sana kama Taifa linalotaka kujenga Taifa lenye uendelevu wa viwanda. Walipotoa maoni kwamba, sekta ya umwagiliaji iongezewe pesa waweze kukuza kilimo cha umwagiliaji hawajakosea, tuzingatie kwamba sasa hivi tuko katika zama za mabadiliko ya tabianchi, mabadiliko ya hali ya hewa, bila kukuza kilimo cha umwagiliaji hatutatoka katika umaskini na upungufu wa chakula katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono 100 kwa 100 kwamba, hiyo sekta ya umwagiliaji iongezewe pesa, tena ipewe nyingi kwa sababu japo kule Longido hatuna mito mingi ya kumwagilia, lakini kuna mto mmoja ambao unatiririsha maji hadi kwetu Ngarenanyuki na nitaongelea katika muda huu wa dakika chache nilizonazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika maoni haya ya kamati ninaunga mkono hili suala la tozo, hizi tozo kwenye mafuta kwa lita ya petroli na dizeli kuelekezwa katika kusaidia kufikisha maji katika vijiji vingi katika nchi yetu ambavyo bado havina maji ni suala lenye tija. Ninaunga mkono na ninaomba hili lizingatiwe ili tuone kama tutapunguza kero ya maji katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, vilevile ninaunga mkono mapendekezo ya kamati katika suala la kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini. Kama vile ambavyo Wakala wa Barabara za Vijijini (TARURA) imeanzishwa tena hivi karibuni, naomba hili nalo lipewe kipaumbele tuone kama tutatoboa katika kupunguza kero ya maji katika vijiji vyetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo basi naomba nidonoe vipengele vichache katika taarifa hii ya hotuba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji. Kwanza napenda kuendelea kuishukuru Serikali kwa mradi mkubwa wa maji ya Mto Simba kuja katika Mji wa Longido ambao unajengwa kwa zaidi ya shilingi bilioni 15. Mradi huu ambao uligawanywa katika sehemu nne na Waziri amebainisha vizuri katika hotuba yake hii, ulikuwa na hivyo vipengele vinne; ujenzi wa chanzo, ambao kwa masikitiko makubwa nashangaa kuona kwamba umeshatimizwa kwa asilimia 40 tu na muda unazidi kwenda, ulazaji wa mabomba umekamilika kwa asilimia 42 tu, ujenzi wa tenki kwa asilimia 90 na ninashangaa hili tanki likimalizika na maji hayajafika matokeo yake ni nini kama sio kukauka na kupasuka kwa kukosa maji na pia mfumo wa usambazaji wa mabomba ambao umekamilika kwa asilimia 75. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nasikitika kwamba juzi nilipita Jimboni kwa haraka nikaona kwamba katika huu mfumo wa usambazaji kuna mitaro ilichimbwa ikaachwa wazi maji yakaja yakafukia na sasa hivi pia kwa sababu labda wameshituka tunajadili hii bajeti, nimeona wanaanza kuchimbua na kutoa pipes nyingine kule chini, inawezekana waliweka ambazo ziko chini ya kiwango. Naomba sana wakandarasi wa mradi huu wafuatiliwe kwa makini na Serikali ijaribu kuukaribia huu mradi maana wananchi watakata tamaa kama ahadi ya kupelekewa maji ndani ya mwaka huu tena ilikuwa ni ndani ya mwezi huu haitatimia kwa muda mfupi iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, pia, nashukuru kwa sababu nimeona kuna fungu la shilingi bilioni sita limetengwa ili kukamilisha mradi huu. Basi naomba Serikali iweke mkono uende kwa kasi zaidi kuliko ilivyo kwa sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, pia ninapenda kujulisha Bunge lako tukufu kwamba maji haya yakifika Longido tu na Orbomba na Engikahet ambapo inakisiwa kwamba itawanufaisha watu takribani 16,712 isije ikachukuliwa kwamba Longido kero ya maji imemalizika. Longido ina vijiji 49 na kutakuwa bado maana hivi ni kama vijiji vitatu tu maji yanafikia hayatakuwa hata yamesambazwa, kuna zaidi ya vijiji 45 bado vina kero kubwa ya maji na hivyo Serikali katika bajeti hii sijaona kama wametupatia kipaumbele katika kuendeleza miradi ya maji, hasa maji ya visima virefu sehemu ambapo hakuna mito ya kupeleka maji karibu vikiweko vijiji vya Wosiwosi, vijiji vya Magadini kule ambako hata sasa hivi nasikitika kusema kwamba baada ya mvua kubwa kunyesha na mafuriko kutokea kumezuka ugonjwa wa kuhara na kutapika ambao dalili zake hazipishani sana na kipindupindu, lakini sina taarifa rasmi niweze kutamka hivyo, ila kuna watu wamepoteza maisha na tusipopeleka maji kwa haraka katika ukanda huo wa Ziwa Natron kuna hatari mara mbili, kuna hiyo milipuko na pia kuna hatari kubwa ya watu kuendelea kuumia mifupa kama alivyosema dada yangu Mheshimiwa Mollel na ninamuunga mkono jana kwa upande wa Arumeru, maji ya Lake Natron nayo ni hatari sana yanapinda hata mpaka miguu ya wanyama wanaokunywa maji yale na watu wale wanaishi tu kama kilometa nane kutoka Mlima Gelai ambako maji ya bomba yangeweza kufikishwa kule tena ni maji masafi kutoka chemchemi, hiyo kero ingeweza kuondoka.

Mheshimiwa Spika, pia nipende kugusia kwa sababu ya muda kwamba katika huu Mpango Kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji pale Longido hatuna mto, lakini Arumeru ndugu zetu wana maji ya Mto Engarenanyuki. Ule mto ni mkubwa, unapeleka maji mengi tu mpaka kule bondeni katika eneo la Wilaya ya Longido hasa katika Kata ya Tingatinga, lakini wakulima wa Kiholela wanaolima nyanya na ni zao kubwa la biashara wametumia mifumo isiyo ya kisasa, maji mengi yanapotea, maji yanaelekea katika mashamba kwa mifereji.

Mheshimiwa Spika, naomba mto huu ujumuishwe kati ya mito ambayo imebainishwa katika hotuba hii ambayo itafanyiwa usanifu ili kilimo cha kisasa kiweze kutekelezwa, matenki makubwa yajengwe na mabomba yaunganishwe watu walioko Tingatinga hasa vijiji vya Ngereiyani nao waweze kufaidika na kilimo cha nyanya maana maji haya yana floride na chloride kwa wingi kiasi kwamba hayafai kwa matumizi ya binadamu lakini ni maji mazuri sana kwa kilimo cha nyanya.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda ninaomba pia nisiache kusemea kidogo suala la Wakala wa Uchimbaji wa Visima (DDCA). Nimeona kwamba katika bajeti hii hatujaguswa kabisa katika visima ambavyo vitachimbwa, sijaona popote kwamba Longido watachimbiwa visima vya maji ukizingatia kwamba kero ya maji katika zaidi ya vijiji 45 iko palepale na Wilaya ya Longido ni moja ya Wilaya kame sana katika nchi yetu. Tena niombe DDCA pia wapeleke wataalam, wafanye survey ya maji katika vijiji vyote nchi hii ili tuwe tayari tunajua kwamba maji yako wapi, pesa zinapopatikana hasa mkitutengea hizi za mafuta tuweze kuchimba visima na kuondoa kero ya maji.

Mheshimiwa Spika, pia ninapenda kusema kwamba katika huu mradi wa kujenga mabwawa, hatuna bwawa hata moja ambalo limebainishwa. Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba katika mvua za mwaka huu ambazo zimekuja kwa kasi kubwa baada ya kiangazi cha miaka mingi, tumebomokewa na mabwawa mawili makubwa yaliyokuwa yanasaidia maisha ya wananchi wa Longido. Bwawa la Kimokouwa limepasuka, Bwawa la Emuriatata limepasuka na Bwawa la Sinoniki lilishapasuka tangu mwaka juzi na ningeomba sana katika bajeti hii Mheshimiwa Waziri hebu angalia jinsi ya kutusaidia hayo mabwawa yaweze kufanyiwa ukarabati kwa sababu, ndiyo yanayosaidia maisha ya watu wa Longido.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna mabwawa yaliyojaa udongo, bwawa la Tingale Sing’ita ambalo huwa halikauki kabisa na linasaidia maisha ya watu wa Kata mbili na Tarafa mbili, Tarafa ya Longido, Tarafa ya Ngaranaibo, ninaomba hili bwawa pia liangaliwe ili liweze kufukuliwa na tuna lingine ambalo liko katika Kijiji cha Ngoswe linaitwa Ngweseiya, pia limejaa udongo.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nihitimishe hoja yangu kwa kusema kwamba sambamba na harakati za Serikali za kutuletea maji safi, pia kuna ahadi mbili zilishatolewa na Mawaziri hapa, Waziri wa Mifugo na Waziri wa Maji pia kwamba watatuchimbia mabwawa katika Kata ya Tingatinga na katika Kata ya Gilai Lumbwa upande wa Wosiwosi. Ni maeneo ambayo yana kero kubwa ya maji na upimaji ulishafanyika, survey imefanyika, usanifu umefanyika na sijaona kama kuna mradi umewekwa katika bajeti hii ili tupate maji hayo.

Mheshimiwa Spika, mwisho tuna kero kubwa moja ili niweze kumalizia kwa sababu ya muda. Kwamba, katika hii miradi inayotekelezwa Longido, hasa ule wa World Bank uliochukua miaka saba na bado haujakamilika wananchi wanaanza kupoteza matumaini maana miundombinu mingine ilijengwa, kulaza mabomba, kuweka visima sehemu za kunywa watu maji…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja, lakini tusisahaulike katika suala moja la msingi kwamba maji ya World Bank yakafanyiwe uchunguzi na siyo hiyo tu ningeomba pia wananchi hawa wa Longido washirikishwe Halmashauri ishirikishwe katika huu mradi wa maji ya mto Simba maana Halmashauri haihusiki imetoka Wizarani ikaenda Mkoani.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa muda.