Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili na mimi nitoe mchango wangu kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ametupa uhai na tunaweza kuwatumikia Watanzania. Namuomba anipe uwezo wa kuchangia vyema, nichangie nikiwa sober katika suala hili muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa ziara yake aliyoifanya Jimboni kwangu Mkinga, kuja kujionea mwenyewe changamoto kubwa ya maji katika Wilaya ya Mkinga. Ulijionea mwenyewe kwamba Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga hatuna maji, lakini uliona vilevile miradi inayoendelea na changamoto zake. Mheshimiwa Waziri nikukumbushe tu ziko hati tatu mezani kwako, Hati ya Mradi wa Doda shilingi milioni 166, hati ya Mradi wa Bwagamacho shilingi milioni 54, Hati ya Mradi wa Mbuta shilingi milioni 227. Tunaomba fedha hizi zilipwe ili kazi ya miradi ya vijijini iendelee. Mheshimiwa Waziri utakumbuka pale Parungu Kasero ulipokuja tulikumbana na changamoto ya kupeleka umeme mwezi wa 11 ulipokuja ukaahidi kutoa shilingi milioni 49 fedha zile hazijafika, tunaomba sana utusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mara kadhaa tumesikia kwamba maji ni uhai, tumekua tukisikia kauli hiyo kwamba maji ni uhai lakini kitabu hiki cha Mheshimiwa Waziri kinatuambia takribani asilimia 41 ya wananchi wakioko vijijini hawapati maji, maana yake hakuna uhai.

Mheshimiwa Spika, Umoja wa Mataifa mwaka 2010 kwa kutambua changamoto hii ikasema maji safi na salama ni haki ya msingi kwa maisha ya binadamu na kwamba ikifika mwaka 2015 tuwe tumetatua tatizo la maji vijijini kwa asilimia 50. Sasa ukiangalia Human Development Report ya recent na ukiangalia machapisho ya wenzentu wa ESRF wanatuambia nguvu yetu kwenda kutatua tatizo la maji inakwenda taratibu mno. Kutoka asilimia 45 mwaka 2004/2005 mpaka leo tunazungumzia asilimia 58 tunakwenda taratibu mno. Wakati hali ikiwa hivyo, leo hii tunazungumzia cases 5,800 za kipindupindu zinaripotiwa kila mwaka nchini. Wakati hali ikiwa hivyo tunapoteza vijana wetu wa chini ya miaka mitano vinapatikana vifo vya watoto 18,500 na katika hao asilimia 90 vinasababishwa na kukosekana kwa maji safi na salama. Kama Taifa tutaendelea kuiachia hali hii mpaka lini? Mpaka lini tutakubali kupoteza nguvu kazi hii.

Mheshimiwa Spika, takwimu hizi zinaonesha kwamba kila mwaka kwa kutopeleka maji safi na salama tunapoteza bilioni 301mpaka lini kama Taifa tutakubali udhaifu huu. Nimesoma ripoti ya Kamati wanasema tumepeleka kwa asilimia 22 tu za fedha zile. Kwenye umwagiliaji ndiyo usiseme, hapa tunasema kilimo kitukwamue kutoka kwenye umaskini wetu, kilimo cha kisasa cha umwagiliaji hatupeleki fedha, tunakusudia nini. Nawasihi sana tupeleke fedha hizi.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana nilisema hapa kwamba tulipoamua kupeleka umeme vijijini tulipoamua kuweka tozo Serikali walikuwa wagumu kukubali tozo ile lakini leo hii tozo ile ndiyo inatusaidia kupeleka umeme vijijini. Nikashauri hapa mwaka jana kwamba hii tozo inayopigiwa kelele na Wabunge kwenye mfuko wa maji tuiongeze tufikie shilingi 100; hatukuongeza. Lakini leo kinachotuondoa aibu ni Mfuko wa Maji kupitia tozo ile. Nawaomba sana Serikali muwe wasikivu tunaposhauri mambo haya tuongeze tozo lile ili twende tukaondoe tatizo la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado narudia kusema Makao Makuu ya Mkinga hatuna maji nimeona kwenye vitabu mmetupangia shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuanza usanifu kwa Miji kama mitano hivi ya Mkoa wa Tanga. Nawashukuru kwa gesture hii, lakini nikumbushe tu mwaka jana mlifanya hivi na fedha hazikwenda. Tunaomba safari hii fedha hizi zitoke ili usanifu ule uweze kufanyika.

Mheshimiwa Spika, nimeona mmetupangia shilingi milioni 500 pale Horohoro lakini mkumbuke wakati mkitupa shilingi milioni 500 mradi ule wa kupeleka maji Horohoro lakini mkumbuke wakati mkitupa shilingi milioni 500 mradi ule wa kupeleka maji Horohoro unazungumzia bilioni sita ni mradi unaoenda ku-save kile kituo chetu pale cha one stop boarder center, tuondoleeni aibu ya watu wetu kwenda kuchota maji Kenya. Haipendezi sana kila siku tukisema maneno haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi ule wa kupeleka maji kutoka Mto Zigi ni muhimu sana. Ni mradi ambao utatusaidia kupeleka maji kwenye viwanda vile 10 ambavyo tunakusudia kuvijenga, uwekezaji wa trilioni 7.6 hautaweza kufanikiwa kama hatutapeleka maji kwenye eneo lile, tunawasihi sana muone umuhimu wa kupeleka maji kwenye eneo lile.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya naunga mkono hoja, ahsante sana.