Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi hii, na nimshukuru Mwenyenzi mungu ambaye ameniwezesha afya njema na kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu bila kuwasahau wananchi wa Mtwara Vijijini ambao wameniwezesha kurudi kwa mara ya tatu katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa katika Bunge hili ambayo kwa kweli imegusa katika kila suala. Mimi kwa kifupi kama ambavyo umeshauri, ningependa nizungumzie maeneo machache.
Eneo la kwanza ningependa kuzungumzia suala la viwanda, ambalo Mheshimiwa Rais amesisitiza wakati wote kwamba Serikali yake itakuwa ni Serikali ya viwanda. Naunga mkona sana suala hilo, na napendekeza suala la wapi viwanda vijengwe, tuangalie vigezo vya kiuchumi zaidi. Mwenyenzi Mungu ameiumba nchi yetu kila eneo lipo zao au ipo rasilimali au malighafi ambazo amewajalia.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na Mkoa wangu ambao Mwenyenzi Mungu ameujalia gesi nyingi, ameujalia zao la korosho, bila kusahau bandari ambayo ni ya asili yenye kina kirefu. Kwa hiyo, naunga mkono Wizara ya Fedha na Uchumi ambayo kupitia Mpango wa Taifa wa miaka miwili, mapendekezo waliyoyatoa miaka mitano ijayo ambayo wamependekeza kuendeleza maeneo ya viwanda eneo la Mtwara likiwa ni mojawapo. Ningependekeza na ningeishauri Serikali kwamba suala la uendelezaji wa viwanda liende sambamba na uendelezaji wa miundombinu ambayo itawezesha viwanda vile kufanya kazi kwa ufanisi, ikiwemo reli ya kutoka Mtwara hadi Songea kwenda Liganga na Mchuchuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, reli ile itawezesha sana kubeba malighafi kutoka Liganga na Mchuchuma kuja Mtwara na vilevile kusafirisha bidhaa ambazo zitazalishwa katika viwanda ambavyo vitakuwepo kule Mtwara. Mtwara imejaliwa gesi na sasa hivi bomba la gesi limejengwa hadi Dar es salaam, lakini bei ya gesi ni sawa Mtwara na Dar es Salaam. Wakati ukiangalia bei ya mafuta ni tofauti, Dar es Salaam tofauti na Mtwara, tofauti na Kigoma na tofauti na eneo lingine. Kwa kuweka bei ya gesi sawa Mtwara na Dar es Salaam au Mikoa mingine ndiyo kusema unataka kuua uwekezaji wa Mkoa wa Mtwara. Kwa sababu hakutakuwa na motisha yeyote mtu kwenda kuweka kiwanda Mtwara wakati bei ya gesi popote anapohitaji ataipata kwa bei ile ile. Kwa hiyo, nimuombe Waziri wa Nishati aliangalie suala hilo la bei ya gesi.
Mheshimiwa Naibu Waziri, suala lingine ambalo nataka pia nilizungumzie ni suala zima la uendelezaji wa bandari ya Mtwara na uwanja wa ndege wa Mtwara. Uchimbaji mkubwa wa gesi unafanyika baharini na wafanyakazi wanapelekwa kule kwa helkopta na kurudishwa kwa helkopta na wakati mwingine kama ilivyo katika eneo lolote la kazi wakati mwingine zinatokea ajali kule. Sasa ikitokea usiku ni suala gumu sana kuwaleta wale majeruhi huku nchi kavu kwa sababu uwanja wa ndege wa Mtwara hauna taa. Ukiachia taa ule uwanja ulijengwa mwaka1965, hata mzungumzaji nikiwa sijazaliwa, lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza hakuna ukarabati wa maana uliyofanyika katika uwanja ule, kwa hiyo, niombe Serikali iufanyie ukarabati uwanja ule uendane na uwekezaji ambao uko kule.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia suala zima la viwanda vya korosho na suala zima la ukamilishaji wa hospitali ya Rufaa katika Mkoa ule. Pia suala la maji, viwanda vyote vinahitaji maji, wananchi wanahitaji maji, lakini shughuli za binadamu nyingi zinahitaji maji. Ningependa kurudia tena kwamba suala la uwekezaji wa viwanda uende sambamba na uwekezaji wa miundombinu ambayo inabeba au inawezesha viwanda vile kufanya kazi ikiwemo umeme, barabara, reli, bandari, hospitali kwa sababu wafanyakazi pia wanahitaji kuwa na afya ili waweze kutumika vyema.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hotuba ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)