Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi nzuri sana ikiwa ni pamoja na miongozo ambayo imetoa dira katika kuboresha utendaji Serikalini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Seleman Jafo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, na Mheshimiwa Joseph Kakunda na Mheshimiwa Josephat Kandege, Naibu Mawaziri, TAMISEMI pamoja na Watendaji wote wa TAMISEMI kwa kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ziara za Waziri alipotembelea Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya alishuhudia changamoto za mtandao wa barabara ambazo kwa kiasi kikubwa hazipitiki kipindi chote. Pia alishuhudia daraja la Mto Idiwili katika Kata ya Isuto ambalo lilijengwa chini ya kiwango kupelekea kuvunjika mpaka leo hakuna mawasiliano ya hiyo barabara ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa Tarafa ya Isangati na Wilaya nzima ya Mbeya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri kupitia TAMISEMI warekebishe hilo daraja la Idiwili, pia barabara nyingi ziko katika hali mbaya sana ikiwemo barabara ya Mjele – Ikukwa, Ilembo – Mwala na Daraja la Izyira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ufinyu wa bajeti ya TARURA, napendekeza uongezwe mgao kutoka mfuko wa barabara kutoka asilimia 30 na kuwa asilimia 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ikamilishe ahadi ya Rais ya kumalizia ujenzi wa stendi ya Mbalizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu miradi ya maji haikukamilika kutokana na usimamizi usioridhisha ikiwemo ubadhirifu. Napenda kupongeza ziara za Mheshimiwa Kakunda, Naibu Waziri wa TAMISEMI na pia Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu Waziri wa Maji, ziara zao zimeleta tija kubwa na sasa miradi ya maji imeanza kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Wizara ikamilishe kuunganisha Mamlaka ya Maji Jiji la Mbeya na Mamlaka ya Maji Mji Mdogo wa Mbalizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza pia Wizara iweke mkakati wa kupeleka maji katika vituo vya afya, zahanati na shule zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Serikali na kwa kipekee Wizara ya TAMISEMI kwa ujenzi wa Vituo vya Afya vya Ikukwa, Sautilya na Ilembo. Pia napenda kushukuru kwa kutenga bajeti ya shilingi bilioni 1.5, kwa ajili ya hospitali ya Wilaya ya Mbeya DC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuomba Serikali kuunga mkono ujenzi wa zahanati zaidi ya 40 na Vituo vya Afya vya Kata ya Ilungu na Isuto ambavyo wananchi wamejenga kwa nguvu zao na vipo katika hatua mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Wizara iweke mkakati wa ujenzi wa mabweni katika shule za kata. Kipekee kuna ujenzi kwa nguvu ya wananchi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Galijembe na Sasyaka (Masoko), ambazo kwa sasa napendekeza Wizara iunge mkono nguvu ya wananchi kumalizia shule hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Wizara iweke mkakati wa haraka, wa mpango miji kwa Mji wa Mbalizi na Miji Mdogo inayokuwa kwa haraka kama vile, Inyala, Ilembo, Isuto, Igoma na Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Serikali iridhie/ maombi ya Halmashauri ya Mbeya DC ya kubadili matumizi ya shamba ya iliyokuwa Tanganyika Packers ili litumike katika kupanga Mji Mdogo wa Mbalizi, ikiwemo maeneo ya ujenzi wa viwanda, hospitali, mashule na makazi ya wananchi na halmashauri imetenga eneo mbadala katika Kijiji cha Mjele kubadilishana na eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, inajenga machinjio ya kisasa kwa soko la ndani na nje ya nchi na vifaa vimetolewa na UNIDO. Kwa sasa kunahitajika bajeti ya Serikali kumaliza ujenzi wa kiwanda hiki cha nyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mbeya Vijijini lina ukubwa wa kilomita za mraba 2,432, tarafa tatu na vijiji 152, lakini Tarafa ya Tembela haiungani na tarafa zingine na utokana na idadi kubwa ya wananchi, Serikali ya Mkoa (RCC) waliomba kugawanywa kwa jimbo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Serikali iridhie kugawa Jimbo la Mbeya Vijijini na naunga mkono hoja.