Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri kwa asilimia mia moja. Nampongeza Mheshimiwa Waziri na Manaibu wake kwa kazi nzuri wanazofanya, ni nzuri na zinaonekana. Niwapongeze pia Makatibu Wakuu wa Wizara kwa kuendesha vyema Wizara. Naomba changamoto zifuatazo tuzifanyie kazi:-

Ujenzi wa barabara ya Nzasa-Kilungule-Buza; barabara hii ni muhimu sana, Serikali imelipa fidia kwa wananchi kwa lengo la kuingia mradi wa DMDP, lakini mradi huo inasemekana hauwezi kuingia katika DMDP. Je, zile fedha za fidia si tungeweza kujenga barabara angalau kwa nusu kilomita? Je, nini hatima ya barabara hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweka maslahi wazi, mimi nilikuwa Mwalimu; Walimu kuwahamisha kutoka msingi kwenda sekondari ni jambo jema, lakini halijazoeleka katika nchi yetu. Zamani ukirudishwa msingi kutoka sekondari ni demotion. Je, Serikali imewapa elimu Walimu watambue Mwalimu anaweza kufanya kazi msingi au sekondari kwa ngazi ya mshahara ule ule? Je, Serikali imejipanga vipi kuweka Counselors katika Halmashauri zetu kwa kutoa ushauri nasaha kwa makundi mbalimbali yanayofanyiwa mabadiliko ya kimfumo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa vibali vya ujenzi katika Halmashauri zetu; kweli Serikali imefanya vizuri kwa kufupisha muda wa kupata kibali cha ujenzi, lakini kibali kinachotoka Halmashauri hakipewi heshima kama kimepitishwa na wataalam mbalimbali matokeo yake wanakuja wahindi na Ma-architect kutoka maeneo mengine kuvitengua na kudai malipo upya. Kwa nini hawa wanataka kupitia wasiungane na Halmashauri, mwananchi akipata kibali aendelee na ujenzi badala ya kusimamishwa kila mara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabasi yaendayo kazi; napongeza Serikali kwa mradi huu ni mzuri na unasaidia. Naomba sasa angalau uanze ujenzi wa mwendokasi Mbagala kwa kuwa hatua iliyobaki ni ulipaji wa fidia ya stendi ya Mbagala Rangitatu. Naomba sasa tuanze ujenzi wa barabara huku tukiendelea na zoezi la stendi, ni jambo jema, nalitakia heri lifanikiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napongeza juhudi za Serikali kwa maboresho ya barabara za Mitaa ya Kariakoo, Gerezani na Upanga kwa kweli inapendeza na kazi ni nzuri kwani maeneo hayo yalikuwa na barabara mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nawapongeza viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mkuu wa Mkoa na Katibu Tawala, Wakurugenzi wa Halmashauri zangu zote za Mkoa wa Dar es Salaam na Wakuu wa Wilaya wote, Ma-DAS wote kwa ushirikiano mkubwa wanaonipa na kuweza kutekeleza majukumu yangu bila kikwazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA waongezewe nyezo za kufanyia kazi kama magreda, makatapira na vifaa vingine vya ujenzi. Kwa kuwategemea wakandarasi wa kukodishwa linapotokea tatizo, hakuna wa kuli-solve haraka sana. TARURA pia waangalie wakandarasi wa kuwapa kazi, kuna tofauti kubwa kati ya barabara za TANROADS na TARURA kwa zile za changarawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za wanawake na vijana, benki wanazitoza riba lakini halmashauri wana Wahasibu. Kwa nini utaratibu usifanyike fedha zikatolewa katika Halmashauri zetu na kama ni benki kusiwe na riba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, bajeti ipite, maendeleo yafanyike, tupate matokeo ya haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.