Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa TAMISEMI pamoja na Manaibu Mawaziri wake. Wananchi wengi wamejenga maboma mengi ya zahanati, shule, nyumba za Walimu pamoja na vituo vya afya na maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, maboma haya yamekaa muda mrefu bila kuendelezwa na kama Serikali inavyosema kuwa wananchi wanapojenga maboma na wakafikia kwenye mtambaa wa panya (lenta) Serikali inaendeleza, lakini mpaka leo kuna maboma mengine yanakuwa magofu. Kwa hiyo niiombe Serikali ipeleke fedha za kutosha ili kumalizia maboma haya ili wananchi waweze kupata huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kuna vituo vya afya viwili vinavyojengwa kwa nguvu za wananchi, vituo hivyo ni Kituo cha Gare na Gwelo. Kituo cha Gare tayari kimeshajengwa maboma manne ambayo yako kwenye hatua tofauti. Jengo la kwanza ni OPD hili limeshapigwa bati, ward mbili nazo zimeshapigwa bati na ward nyingine mbili zipo kwenye kujengwa msingi. Kituo cha Afya Nawelo hiki kina jengo moja la OPD ambalo lipo kwenye mtambaa wa panya (lenta). Kwa hiyo niiombe Serikali itupatie fedha kama vinavyopatiwa vituo vya afya vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lushoto lina kituo cha afya kimoja tu ambacho kipo Mlola na niishukuru Serikali yangu tukufu kwa kutupatia shilingi milioni 700 kwa ajili ya kupanua kituo pamoja na kupata vifaa tiba. Hata hivyo, kituo cha afya kile kina changamoto ya gari la wagonjwa na ukizingatia kituo cha afya kile kina zaidi ya kilomita 53 kufika katika hospitali ya wilaya. Kwa hiyo gari hii itakuwa ni muhimu ili kuokoa vifo vya akinamama na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ni kawaida kabisa kwa halmashauri kutotenga 10%. Kwa hiyo niiombe Serikali ihakikishe halmashauri zinasimamiwa ipasavyo kwa suala zima la kutoa 10%. Kwani halmashauri nyingi hazitengi pesa hizi kwa viburi walivyokuwanavyo watendaji wachache wasiolitakia Taifa letu mema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa zilizotengwa kwenda TARURA 30% ni ndogo sana wakati mahitaji ya barabara ni makubwa hasa kwa vijijini. Kama unavyojua uchumi mkubwa wa wananchi unatoka kwa wakulima ambao wapo vijijini kwa hiyo wananchi hawa wanatakiwa waboreshewe miundombinu. Serikali iongeze ifike 50% ili angalau barabara zetu ziwe zinatengenezwa kwa wakati muafaka na kwa wingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali 20% kikamilifu kwa ruzuku inayotengwa kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya mamlaka za chini yaani vijiji na Serikali za Mitaa. Kwani hii pesa ikitengwa itasaidia kuwalipa Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa. Niishauri Serikali ianzishe Bodi ya TARURA ili Bodi hii isimamie kuanzishwa kwa Mfuko wa TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niombe Serikali iwezeshe halmashauri fedha ili ziweze kununua magreda kwa ajili ya kutengeneza barabara zetu za vijiji hasa kukiwa na dharura kuharibika kwa barabara hasa vijijini. Niiombe Serikali pamoja na kuishauri ifanye haraka iunde haraka mamlaka ya maji vijijini, kwani kuna uovu mkubwa sana unaofanywa na watendaji wetu na ndio maana miradi hii ya maji haimaliziki kwa wakati na mingine haifiki hata kwa robo kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni takribani miaka saba sasa toka iundwe Mamlaka ya Mji Mdogo wa Lushoto, lakini cha kushangaza mamlaka ile haijapewa mamlaka ya kujiendesha mpaka leo. Niiombe Serikali itoe kauli ili mamlaka ile iweze kupewa madaraka yake.