Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuchangia kidogo kwenye Wizara hii muhimu kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipouliza swali mara kadhaa hapa Bungeni kuhusu ni lini Serikali itajenga daraja muhimu la Mto Ruhembe lililopo kwenye Kata ya Ruhembe Jimboni Mikumi, aliyekuwa Naibu Waziri wa TAMISEMI ambaye sasa ni Waziri aliahidi kututengea Sh.700,000,000/= kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo kwa kuwa wanatambua umuhimu wake na vifo vingi vinavyosababishwa na maji mengi ya mto huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kusikitisha mpaka leo bado hakuna kinachoendelea maana mpaka sasa hata yale machuma ya daraja yaliyoletwa kutoka Chekeleni yamewekwa chini na hakuna kinachoendelea na madhumuni yake yalikuwa yaletwe ili lijengwe daraja la muda wakati tunasubiri kuletewa fedha za ujenzi wa daraja hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujibu aweze kutujibu ni lini pesa hizo Sh.700,000,000/= zitaletwa na je, vyuma vya daraja la muda ni lini vitaweza kuunganishwa na kusaidia wananchi kwa muda muafaka maana vinapokaa pale kwa muda mrefu vinasababisha hali ya wananchi kuwa mbaya na pia watu wenye nia mbaya wanaweza kuviiba na kuitia hasara kubwa sana Serikali na wananchi wa Jimbo la Mikumi kwa ujumla. Tunaomba sana tupate majibu ni lini Serikali italijenga daraja hili muhimu la Ruhembe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali imekuwa ikiahidi mara kwa mara kumalizia ujenzi wa barabara ya lami kuanzia Dumila – Kilosa mpaka Mikumi ambayo imekuwa ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne na Rais wa Awamu ya Tano kuwa barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho Mji Mdogo wa Mikumi unakua kwa kasi sana na ni mji wa kitalii, je ni lini Serikali itajenga kituo cha afya kwenye Mji Mdogo wa Mikumi? Maana Zahanati ya Mikumi ni chakavu sana na imezidiwa kabisa uwezo na idadi kubwa sana ya watu wengi pale Mikumi na vitongoji vyake, hivyo tunahitaji sana kuwe na kituo cha afya ili kiweze kuhudumia wananchi na watalii na wanaotumia barabara ya Tanzania - Zambia ambapo kuna ajali nyingi sana maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.