Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi katika maeneo ya pembezoni, mazingira yao ni magumu. Kutokana na jiografia ya Ukerewe ambapo ina visiwa (38) Watumishi wengi wanakuja kuripoti na kuondoka, hali ambayo inasababisha upungufu mkubwa wa watumishi hasa katika maeneo ya afya na elimu. Zahanati zetu, vituo vya afya pamoja na shule zina upungufu mkubwa wa watumishi katika Visiwa vya Ukerewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi au ushauri wangu ni kwamba, moja; pamoja na Halmashauri zetu kuwa na mipango mbalimbali ya motisha kwa watumishi wanaopangwa kwenye Halmashauri zetu, Serikali iwe na mpango maalum wa kuhakikisha kuwa watumishi wanaofanya kazi katika maeneo kama ya Ukerewe wapate package fulani ya mazingira magumu ili wasijione kama watu waliopewa adhabu na hivyo kutafuta kila njia kuondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili; kutokana na changamoto ya watumishi kuripoti na kuondoka katika maeneo kama Ukerewe, katika mgao wa watumishi Visiwa vya Ukerewe viangaliwe kwa mtazamo wa pekee na hivyo kupewa idadi ya kutosha ya wataalam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, malipo ya Wenyeviti wa Vijiji/Mitaa na Vitongoji; wananchi ndiyo injini kubwa ya maendeleo kwenye Halmashauri zetu lakini wanaweza kuwa na tija pale wanaporatibiwa na kusimamiwa na viongozi wetu wa ngazi za chini, mfano, Wenyeviti wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji lakini viongozi hawa wamekuwa na mfumo mbovu na malipo duni wakati wanafanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza au nashauri kuwa, mfumo wa malipo kwa viongozi hawa ubadilishwe ikiwezekana basi Serikali Kuu iweze kuwalipa moja kwa moja badala ya kupitia Halmashauri kwa sababu nyingi zimekuwa haziwalipi viongozi hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwango kinacholipwa kwa viongozi hawa kiongezwe ili kiendane na hali halisi ya maisha ikizingatiwa kwamba wanatumia muda wao mwingi kuhamasisha na kusimamia shughuli za maendeleo, muda ambao wangetumia katika shughuli zao binafsi za uzalishaji.