Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia hizi Wizara mbili ambazo ziko chini ya Ofisi ya Rais. Kwa kuanza kabisa, naomba niwaombe Waheshimiwa Wabunge pamoja na kusimamia na kushauri Serikali ni muhimu sana kuchangia kwa busara na bila ugomvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Rais wangu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutoa agizo na Mheshimiwa Waziri Mkuu kufuatilia kwa karibu sana na kikamilifu nia ya Mheshimiwa DC wangu kutaka kuniweka ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kuwashukuru sana Wabunge wa Mkoa wa Manyara, Wabunge wote ambao wamefuatilia suala langu hususani Mheshimiwa Abuu kuona kuna nini kumbe nataka kuwekwa ndani kwa sababu niko karibu sana na wananchi wa Wilaya ya Hanang. Nawashukuru sana kwa uvumilivu wao nilivyowaomba wasiandamane kuja kule hawakufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba waendelee kushirikiana na mimi, ushirikiano ambao unawapa hofu watu ambao wanataka kuvamia wilaya yangu, napenda niendelee kushirikiana nao na Mungu awabariki sana. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei taarifa kwa sababu ni kweli sijawekwa ndani na nimemshukuru Rais kwa agizo lake. Kama walikuwa wanataka niwekwe ndani sijawekwa ndani na ni wao ndiyo chimbuko la matatizo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza sana na kumshukuru Waziri Jafo, wakati nia hiyo ikitaka kutekelezwa yeye vilevile alisaidia sana kuisimamia vizuri TAMISEMI ili wanaofanya kazi chini yake wafanye kazi vizuri. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora) kwa sababu kwa kweli wanajaribu sana kusimamia utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye mambo ya wilaya yangu. Napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuona kwamba agizo lake la elimu msingi bure linatekelezwa vizuri ambalo limezaa uandikishaji wa watoto mara mbili ya uandikishaji wa awali kabla ya agizo hilo. Pamoja na agizo hili zuri nataka niwaambie kwamba sasa watoto walioandikishwa wameongezeka, madarasa yanatakiwa zaidi na vilevile nyumba za Walimu zinatakiwa zaidi na zaidi ya yote tunahitaji walimu wengi zaidi kwa sababu watoto wameongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mfano tu wa Wilaya yangu ya Hanang kwamba kabla ya agizo lake tulikuwa tunaandikisha watoto laki moja na elfu kumi lakini mwaka huu wa 2018 waliandikishwa elfu kumi na mbili na mia nne themanini na sita. Utaona jinsi watoto walivyoongezeka, kwa hivyo, madarasa mengi yatahitajika, Walimu wengi watahitajika na nyumba nyingi za Walimu zitahitajika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri wananchi wa Hanang wameliona hilo na wanamuunga mkono Rais wao kwa kujenga madarasa mengine lakini naomba tushirikiane nao. Kwa mfano, mahitaji ya madarasa kwa shule za msingi ni mia saba sabini na mbili na sekondari ni sitini na nne, kwa hiyo, wao wako tayari kushirikiana na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuwe na utaratibu mzuri, nyumba zinazohitajika sasa hivi ni mia nane ishirini na tano kwa shule za msingi, mia tatu sabini na saba kwa shule za sekondari na madawati mia tisa kumi na mbili kwa shule za msingi na mia tano tisini na tisa kwa shule za sekondari. Haya yote yametokana na kuandikisha watoto wengi zaidi. Wananchi wako tayari kusaidiana na kuunga mkono Serikali yao, wanachoomba utaratibu mzuri wanapoona kwamba wananchi wamejenga mpaka kwenye lenta basi mimi Mbunge wao nipo lakini Serikali za Mitaa pamoja na Serikali Kuu tuone ni namna gani tunawaunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu afya, Serikali ina utaratibu mzuri kama kusaidia wananchi katika ujenzi wa vituo vya afya. Hanang wanajitahidi sana, wana vituo kama saba walijitolea wao wenyewe kuvijenga na napenda kuishukuru TAMISEMI kupangia na kutoa shilingi milioni mia tano kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Simbai ambacho kipo kwenye kata ambayo iko pembezoni na kitasaidia watu wengi sana hata wale wa Kondoa watakuja kwenye kile kituo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tuendelee kuungana na wananchi kwa sababu afya ni muhimu sana. Watu wanaokwenda kwenye kilimo, wanaokwenda katika ufugaji, wanaofanya biashara ni wale wenye afya. Kama hatuna misingi mizuri ya afya itakuwa ngumu sana kutekeleza hata ilani yetu na kuleta maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara za vijijini, naishukuru na kuipongeza Serikali kuunda TARURA kwani itasaidia barabara za vijijini. Tujue kwamba barabara kuu na za mikoa hazitafanya kazi kubwa kama vijijini hakuna barabara. Naomba sana ugawaji wa fedha za Mfuko wa Barabara uwe hamsini kwa hamsini na ikiwezekana tutilie mkazo vyanzo vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia REA, Serikali imefanya kazi kubwa kwani wananchi wa vijijini walikuwa hawategemei umeme lakini sasa umeme umefika vijijini, naipongeza sana Wizara. Hata hivyo, kuna upungufu mwingi ambao na kwa hakika usipofanya jambo upungufu hautaonekana, naomba Waziri aweze kufanya tathmini kila wakati ili aondoe upungufu ule kama kuruka taasisi au vijiji njiani wanapopeleka kwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda nichukue nafasi hii kwa sababu mwaka 2004 nikiwa Waziri wa Utumishi ndiyo tuliotoa ule Waraka kwamba wale watendaji waliomaliza darasa la saba kabla ya muda huo waendelee. Nimeishukuru sana Serikali kuchukua hatua hiyo, nampongeza sana Waziri Mkuchika kuweza kuelewa Waraka ule na kuwaelekeza watendaji waone kwamba ule Waraka unasimamiwa vizuri na watu wasionewe ila pale ambapo wamegushi hatuwezi kusema neno lolote. Napenda kuwashauri watendaji wa Serikali wasipende kughushi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie hakuna mahali ambapo panatakiwa job security kama Serikalini kwa sababu ndiyo uamuzi ambao unahusu maisha ya watu unapotoka. Watumishi wa Serikali wanapaswa wajisikie salama, wanapaswa wajisikie kwamba wanaaminika ili waweze kutenda haki ambayo inaweza ikasaidia maendeleo ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana Wizara ya Utumishi iweze kusimamia sana usalama wa kazi kazini kwa sababu kwa kweli wasipokuwa salama hawatakuwa na uhakika katika kufanya uamuzi na mambo mengi yatasimama…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono hotuba ya Mawaziri wote wawili, naiunga mkono Ofisi ya Rais kwa kazi nzuri inayofanyika.