Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo kuchangia hoja ya TAMISEMI pamoja na Utawala Bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza nitaenda moja kwa moja kwenye suala la mgao wa wilaya. Halmashauri yetu ya Wilaya ya Tunduru ni kubwa sana na kilio chetu kimekuwa cha muda mrefu. Pamoja na kwamba Rais amesema hatutakuwa na mgao lakini hali yetu ya kiutawala ni ngumu kutokana na ukubwa wa eneo letu tulilokuwa nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Tunduru imeanzishwa tangu mwaka 1905 lakini mpaka leo haijawa na wilaya nyingine na ukubwa wake ni zaidi ya Mkoa wa Mtwara ambao sasa una wilaya zaidi ya sita (6). Kwa hiyo, utakuta kimaendeleo kuhudumia wananchi wetu inakuwa ni ngumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba kulingana na idadi ya watu tuliokuwa nao, ukubwa wa eneo uliokuwepo na umbali wa makao makuu kuhudumia maeneo mengine yaliyokuwepo tunaomba sana mtufikirie kwa hali na mali ili tuweze kupata wilaya nyingine kwa ajili ya kuwahudumia watu wetu vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nitalizungumzia ni suala la elimu. Kama nilivyozungumza juzi tunashukuru sana elimu bure lakini tuna changamoto nyingi sana upande wa Tunduru ambazo kwa kweli ni aibu, mpaka leo tuna madarasa ya nyasi katika maeneo mengi ya shule zetu za msingi. Pamoja na madarasa ya nyasi lakini bado hata vyoo hatuna. Kulingana na idadi ya watoto ilivyokuwa utakuta shule ina watoto 840 matundu ya vyoo ni saba, kumi ambayo hayaendani na hali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi kwenye nyumba za Walimu ndiyo usiseme, walimu ni wachache kupita kiasi hata nyumba zao hazipo. Kwenye eneo langu nimetembea karibu jimbo zima na shule zote za msingi nimezitembelea, shule ina watoto 840, Walimu watano, sita au watatu. Asilimia 60 ya shule za msingi zilizopo kwenye jimbo langu zina Walimu chini ya watatu, jambo ambalo ni gumu hata tukifikiria namna wanavyofundisha na kufaulisha Walimu wale wanastahili pongezi kubwa sana kwa sababu Walimu ni wachache na madarasa yamekuwa mengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili nimeliona miaka hii kunakuwa na session katika madarasa ya kwanza mpaka darasa la saba. Kwa kweli wale watu wanastahili kupewa hata overtime kwa sababu wanafunzi ni wengi, madarasa ni mengi lakini wanafundisha Walimu wachache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nitazungumzia juu ya ujenzi wa vituo vya afya. Naishukuru kwa mara nyingine Serikali kwa kutupatia Kituo cha Afya Nkasale lakini eneo la Tunduru kwa maana ya halmashauri yote tuna kata 35. Katika kata 35 tuna vituo vya afya vitano (5) tu na hivyo kwenye jimbo langu kuna vituo vya afya vitatu (3).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Kituo cha Afya Nalasi, Rais wa Awamu ya Nne Rais Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alitoa ahadi ya kujenga kituo hiki. Nalasi ni mji mkubwa una zaidi ya wakazi 30,000 ambao wako kwenye kata mbili katika kijiji hicho hicho kimoja. Kwa hiyo, alivyokuja kwa mara ya mwisho aliahidi kwamba angeweza kujenga kituo cha afya katika kata ile na aliahidi kutoa gari la wagonjwa lakini ile ahadi mpaka leo haijatekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013/2014 kwenye bajeti waliweka shilingi milioni 80, wananchi walifyatua tofali za kujenga boma. Bahati nzuri shilingi milioni 80 ilipatikana wakaanza ujenzi ule lakini tofali zile sasa zimekuwa kichuguu, tangu umejengwa huo msingi kwa maana ya foundation mpaka leo ahadi ile haijatekelezeka na halmashauri imejitahidi kila mwaka kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa halmashauri yetu ni kubwa kama nilivyozungumza tuna kata 35, tuna Madiwani 52, tukijumlisha sisi Madiwani kwa maana Wabunge halmashauri yetu ina Madiwani 55 yaani ni darasa kubwa ambalo hata kusikilizana inakuwa ni ngumu. Kwa hiyo, bajeti ya afya haitoshi na ya elimu inakuwa haitoshi kwa sababu mapato yetu hayawezi kukidhi kuweza kuhudumia vituo vya afya vyote kwa maana ya kupata fedha za majengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nilizungumzie ni suala la maji. Tuna miradi mingi sana ambayo inasimamiwa na halmashauri yetu kwa maana ya maji. Tunayo miradi ya muda mrefu, Mradi wa Mtina mpaka leo haujakwisha. Juzi bahati mbaya halmashauri imesitisha mkataba na mkandarasi yule lakini naomba waende wakaangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimetembelea ule mradi kwa macho yangu na kwa scope ya kazi niliyoona inaonekana mradi ule umefikia zaidi ya asilimia 80, lakini kwa matakwa ya watendaji wetu naweza kusema kwa maslahi binafsi wameweza kusitisha ule mkataba tangu Desemba mwaka jana mpaka leo mkandarasi mwingine hajapatikana, wakati wangeweza kumuachia ndani ya mwezi mmoja kama alivyoomba mradi ule ungekuwa umeweza kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na tabia nchi ya ukame katika maeneo mengi, Tunduru tulikuwa na mito mingi lakini bahati mbaya mito hii imeendelea kukauka. Kwa hiyo, tunahitaji miradi ya maji mingi kwenye vijiji vyetu kwa ajili ya visima vifupi na virefu ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ningependa kuchangia juu ya watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru. Halmashauri yetu kama nilivyozungumza ni kongwe na ni imezeeka lakini ina watumishi wachache sana. Watumishi waliokuwepo ni wachache mno ukizingatia na namna ambavyo kazi zile zinafanyika. Mbaya zaidi kuna watumishi wanazeeka na halmashauri ile, wana zaidi ya umri wa miaka 20 kwenye halmashauri moja, kwa hiyo, wanafanya kazi kwa mazoea kiasi kwamba kila wanachokifanya wanafanya kwa namna ambavyo wao wanaona siyo kwa matakwa ya masharti ya kazi kama ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba basi ikiwezekana watusaidie angalau kufanya internal transfer kwa maana ya kutoka halmashauri moja au nyingine ili wale waliokaa muda mrefu ambao sasa imekuwa ni mazoea kufanya kazi zao ikiwezekana na wao waweze kupelekwa sehemu nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna jambo linanisikitisha kwenye halmashauri yetu. Tumekuwa na tabia sisi ya kusomesha wataalam wetu katika halmashauri...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)