Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia kwenye hoja zilizoko mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amezidi kutupa baraka zake na hatimaye tunaweza kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza kwenye mambo matatu. Nitajielekeza kwenye suala la elimu, afya na lishe. Nitumie fursa hii kuishukuru sana Serikali kwa kutupatia fedha za kujenga mabweni na madarasa kwa Sekondari zetu mbili za Maramba na Mkinga ambazo zimekuwa high school, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizo bado sekondari hizi ambazo zimekuwa high school zina changamoto nyingi kwani kuna uhaba mkubwa wa nyumba za Walimu. Sekondari ya Mkingaleo hakuna nyumba za Walimu na high school ile inachukua wasichana, kwa hiyo, unaweza kuona hatari iliyopo. Nawasihi sana Serikali tuchukue hatua za haraka kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Sekondari ya Maramba, sekondari ile tulipoianzisha tulichukua majengo ya yaliyokuwa mashamba ya mkonge. Kwa hiyo, nyumba wanazotumia Walimu ni nyumba zile za wafanyakazi wa mkonge, za chini kabisa. Kwa hiyo, unaweza kuona picha Walimu wetu tunawaweka katika mazingira gani. Nawasihi sana, tumezipandisha hadhi shule hizi, basi tuziboreshe na kuzipa hadhi inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile shule hizi zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa Walimu, taarifa tumekwishapeleka naomba waziangalie. Pia shule hizi zinakabiliwa na tatizo la maji, naomba waangalie. Wingi ule wa wanafunzi katika shule zile halafu shule hazina maji ni changamoto kubwa kwelikweli. Vilevile lipo lingine, shule hizi hazina usafiri, tumewaweka vijana wetu pale, lakini shule hizi hazina usafiri ni changamoto kubwa kwelikweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunayo madai ya Walimu. Tuna Walimu takribani 271 wanadai madai mbalimbali, ukiacha mishahara, wanadai takribani shilingi milioni 312. Hata orodha ile ya malipo ilipotoka kwa Wilaya ya Mkinga walikuwa ni wafanyakazi wawili tu, naomba waliangalie vizuri jambo hili, halitupi hali nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ndugu yangu Mheshimiwa Waziri atakumbuka niliwahi kuja na timu ya Madiwani kutoka Mkinga, wanastahili posho zao baada ya kumaliza muhula uliopita wa Bunge. Mpaka leo madai yao bado hayajatimia, naomba tuwalipe fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni kwenye afya. Hapa naomba vilevile niipongeze na niishukuru sana Serikali, imetupatia shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga kituo cha afya. Kituo kile kimekamilika, tunaomba zile shilingi milioni 200 zilizobaki ili kufika shilingi milioni 700 kwa ajili ya vifaa tiba, naomba watupatie ili tuweze kukamilisha kituo kile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado ombi langu liko palepale la kuhakikisha Wilaya ya Mkinga tunapatiwa fedha za kujenga hospitali ya wilaya. Wilaya ile tuna kata 22, sasa hivi tuna vituo vya afya vitatu. Kwa hiyo, unaweza kupata picha kwa wilaya yenye kata 22, haina hospitali ya wilaya ina vituo vya afya vitatu, unaweza kujua ukubwa wa tatizo ni kiasi gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikilisema hili muda mrefu, naomba ifike mahali sasa Serikali isikie. Tunawashukuru World Vision kwa kutusaidia kujenga jengo la kisasa la upasuaji katika Kituo cha Afya cha Mkingaleo, tunaomba na wahisani wengine waige mfano huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna upungufu mkubwa kwenye sekta ya afya, tuna mahitaji ya watumishi 395 waliopo ni 183, tuna uhaba wa karibu asilimia 58 ya watumishi. Maombi haya tumekwishayapeleka muda mrefu, tunaomba wayafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nihamie kwenye lishe. Hapa nataka ku-declare interest kwamba mimi ni Mwenyekiti wa Kikundi cha Ma-champion wa Lishe katika Bunge letu. Niishukuru Serikali juzi imetoa commitment ya kutoa semina kwa Wabunge wote juu ya tatizo tulilonalo la lishe katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwamba kwa ukubwa wa tatizo tulilonalo katika nchi yetu ingekuwa busara sana kama Wabunge wote mngeona umuhimu wa kujiunga na kikundi hiki cha lishe. Mwaka jana tulifanya jambo kubwa, tulipitisha hapa shilingi bilioni 11 ziende kwenye halmashauri kwa ajili ya kutatua tatizo la lishe. Lilikuwa ni jambo kubwa kweli kweli lakini cha kushangaza na imenisikitisha kidogo kwamba nimeisikia hotuba ya Waziri Mkuu sikusikia chochote kuhusu lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeisikiliza hotuba ya ndugu yangu Mheshimiwa Jafo hakuna sehemu imetajwa lishe. Ndugu zangu tuna tatizo kubwa kwenye lishe, wala
tusimumunye maneno, tuna tatizo kubwa. Haiwezekani kwamba takribani asilimia 45 ya vifo vya watoto katika nchi hii vinahusishwa na utapiamlo, haiwezekani asilimia 57 ya watoto katika nchi hii wana upungufu wa damu, haiwezekani asilimia 34 ya watoto wetu wamekuwa stunt halafu hotuba zetuhazigusii jambo hili, si sahihi, si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jafo yeye alikuwa miongoni mwa Wabunge tulioanzisha kikundi cha lishe, najua passion yake kwenye jambo hili, Waziri wa Fedha najua passion aliyonayo kwenye jambo hili, hebu tuchukue hatua. Taarifa zilizopo ni kwamba katika shilingi bilioni 11 tulizoidhinisha it’s only eight percent ya fedha hizo ndiyo zimekwenda. Taarifa hii ni ya mwezi wa Pili. Katika shilingi bilioni 11 tumepeleka shilingi milioni 888, hii haiwezi kuwa sawa. Nawasihi sana tuchukue hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua changamoto tuliyonayo ni kwa sababu fedha hizi tunazipitishia kwenye Health Basket Fund, fedha hizi tunataka zitoke kwenye own source, fedha hizi tunataka zitoke kwenye OC. Njia hii haitatufikisha, tuangalie uwezekano wa kutumia njia ya ku- ring-fence fedha hizi, kuzi-page kwenye GDP asilimia fulani ili tuhakikishe fedha hizi zinakwenda moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukitumia bajeti za halmashauri kule tukategemea tutaenda kutatua tatizo kubwa kama hili tunajidanganya. Tumekubaliana kwenye vision 2020-2025 kwamba tutaweka kipaumbele kwenye kuboresha human capital na productivity haya hayawezi kupatikana kama hatutahakikisha tunaondokana na tatizo la lishe duni na lishe iliyopitiliza.

T A A R I F A . . .

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa lakini hali ni mbaya zaidi ya hapo. Tathmini inaonesha kwamba kama hali ikiendelea hivi ikifika mwaka 2025 Taifa litakuwa limepoteza nguvukazi ya shilingi trilioni 28.8, this is very serious. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri atakapokuwa anahitimisha taarifa yake atueleze, tulikubaliana kwamba tutaajiri Maafisa Lishe 600, nini kimetokea mpaka sasa hatujaweza kuajiri? Vilevile mpaka kufikia kipindi hiki ni fedha kiasi gani tunazipeleka kwenye lishe? Nawasihi sana tunapofanya mabadiliko ya miundo katika Wizara tujitahidi Kitengo cha Lishe kisije kikamezwa tukahatarisha jitihada hizi tulizozianza.