Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi. Nami niungane na wanachama wenzangu kutoa pole kwa viongozi wetu wa Chama Taifa, Wabunge, kwa wakati mgumu wanaopitia kipindi hiki, najua wako na kesi Mahakamani. Tunaendelea kuwaombea kwa Mungu awape ujasiri na dhahabu ili ing’ae ni lazima ipite kwenye moto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Jafo, kazi yako inaonekana. Nina mambo matatu. Kwanza nizungumzie issue ya Wakurugenzi, naiomba Wizara sasa ifanye tathmini kwa Wakurugenzi ambao wameteuliwa ili wale wenye sifa waweze kubaki na wale ambao hawana sifa tuweze kuwaondoa kwa sababu Wabunge wengi hapa wakichangia wameonesha mambo hayaendi kwenye Halmashauri zao. Wakurugenzi wengi waliteuliwa kisiasa. Wengi waliokosa kura za maoni walipewa kama zawadi na walioshindwa kwenye Uchaguzi Mkuu na hii imesababisha ugomvi mwingi kwenye Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko baadhi ya Halmashauri Wakurugenzi wanashindwa hata kuendesha vikao vya Mabaraza, wanaitisha vikao vya Mabaraza, lakini ikifika wakati wa vikao wanakaimisha Wakuu wa Idara na hii inasababisha maamuzi mengi kutokufikiwa kwa wakati na maendeleo ya Halmashauri hizo yanarudi nyuma. Kwa hiyo, niombe sana wafanye tathmini kwa hawa Wakurugenzi wenye sifa wabaki, wale ambao hawana sifa waondolewe. Pia tufuate utaratibu wa Utumishi wa Umma wanaotoka kwenye utumishi wa umma ndio waajiriwe katika nafasi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili nizungumzie miradi ya maendeleo kwenye halmashauri zetu; fedha hizi zimekuwa zinachelewa na hazifiki kwa wakati na kibaya zaidi Serikali Kuu ilichukua vyanzo vile vya mapato tena vyenye fedha nyingi wakiahidi kwamba wanakusanya ili waturudishie. Kibaya zaidi fedha hazirudi kwa wakati na zikirudi ni chache, niiombe Wizara sasa kwanza itupe tathmini wakati tulipokuwa tunakusanya wenyewe kama Halmashauri na wao walipoanza kukusanya yale malengo waliyojiwekea yamefikia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hayajafikia ni vizuri sasa vyanzo hivi vya mapato vikarudishwa kwenye Halmashauri zenyewe, ziendelee kukusanya ili kuweza kutekeleza ile miradi ya maendeleo tuliyojiwekea. Serikali Kuu kwa sababu wamechukua vile vyanzo lakini fedha hawazileti. Niishauri Serikali sasa ni wakati muafaka wa kubuni vyanzo vyao vya mapato na kuacha kuchukua vyanzo vya mapato vya Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni upungufu mkubwa wa Watendaji wa Vijiji; kumekuwa na upungufu mkubwa sana, unakuta vijiji viwili, vitatu vinakaimiwa na mtu mmoja. Hili limekuwa ni tatizo kubwa sana kwa wananchi wetu kupata huduma kwa wakati. Kwa hiyo, niiombe Wizara kuhakikisha kwamba Watendaji hawa wanaajiriwa ili wananchi wetu waweze kupata huduma hizi kwa haraka pale wanapofika kwenye hizo ofisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu ofisi za Watendaji hawa, hakuna, hata za kata baadhi ya vijiji hazina ofisi hizo kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la upungufu wa Walimu. Tumekuwa na upungufu mkubwa sana wa Walimu katika Mkoa wetu wa Kilimanjaro na Jimbo la Moshi Vijijini wa shule za msingi. Hii imetokana na kuwa Walimu wengi wamefikia umri wa kustaafu. Tunaomba sana suala la walimu ajira zao zipatikane kwa wakati, pia nyumba za Walimu bado ni tatizo kubwa sana kwa Walimu wetu tuhakikishe nyumba zinajengwa na ajira ipatikane kwa haraka kwa ajili ya watoto wetu hawa ili waweze kupata elimu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine pia yako matatizo kwa watumishi wetu, wamekuwa wakilalamika hawapati mafao yao kwa wakati, nimwombe Waziri tuhakikishe Walimu wetu tunajua wengi tumefika hapa kwa sababu ya Walimu, kwa hiyo tuhakikishe mafao yao yanapatikana kwa wakati.