Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia hotuba hii muhimu. Niwapongeze sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, Waziri wa Mambo ya Ndani, Naibu wake na Watendaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani kwa kazi kubwa na muhimu ya kulinda usalama wa raia na mali zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuanza kuchangia kwa kuzungumzia masuala ya Wilaya za pembezoni kama vile Ileje ambako tuna changamoto nyingi za kiusalama kwa sababu tuko mpakani na Malawi na Zambia, pia, kuna mwingiliano mkubwa wa wageni toka Somalia, DRC Congo, Zambia na Zimbabwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zetu ni kuwa Ileje yenye ukubwa wa kilometa za mraba 1,906 na yenye jiografia ngumu ya milima na mabonde na raia wake ambao wako mbalimbali sana na kwenye umbali mrefu kati ya kata na kata, kijiji na kijiji, ina kituo kimoja tu cha Polisi miaka takribani 44 ya Wilaya hii kongwe. Hiki ni kikwazo kikubwa kwa utoaji huduma, Kituo Kidogo cha Polisi cha Isoko wananchi wametumia nguvu zao kukijenga na kupaua. Tunaomba Serikali iwaunge mkono kukimalizia na kujenga nyumba za watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Ileje ina upungufu mkubwa wa Askari, Wilaya nzima tuna Askari 58, karibu ratio ya 1:5,000 askari kwa wananchi kwa projection ya mwaka jana, hivyo kuhatarisha ulinzi na usalama. Kituo chetu kimechakaa mno kwa sababu ni cha miaka mingi mno. Tathmini tuliyofanya tunahitaji milioni 38 kufanya ukarabati wa kituo pekee kilichopo Ileje. Tuna nyumba 10 za Askari ambazo zinahitaji ukarabati mkubwa na hazitoshi kwa mahitaji ya makazi ya Askari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Polisi cha Ileje kina upungufu mkubwa wa vitendea kazi, mafuta, spea tairi za magari na hata magari ya kufanyia kazi na hiki ni kikwazo kikubwa kwa utendaji wa Askari wetu ambao wanafanya kazi katika mazingira magumu mno. Maslahi na vyeo vya Askari wa Ileje bado ni duni sana na kwa kuzingatia ugumu wa maisha ya Ileje wanahitaji kuhamasishwa na kupewa stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vyetu havipokei fedha ya kutosha kuendesha ofisi na hii inasababisha askari kuomba msaada wa Mbunge mara kwa mara ili waweze kufanya kazi. Tumeshawapatia mashine ya kudurusu ya kisasa, laptop, printer na scanner, vilevile nimechangia ma-box ya rim za karatasi, nimechangia matairi ya gari na kukarabati gari la Polisi, pia, nimechangia matengenezo mengine. Hii haipaswi kuwa kazi ya Mbunge, lakini kwa kuzingatia umuhimu wa usalama wa wananchi na mali zao imebidi iwe hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye masuala ya Jeshi la Zimamoto kuna haja ya kuhakikisha kuwa, kila jengo la biashara linajengwa liwe na ngazi ya dharura nje ya jengo kila ghorofa. Nyumba nyingi kwa sasa hazizingatii hili, tunataka Waziri atoe tamko kuhusu hitaji hili muhimu kwa usalama wa watu na mali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunamwomba Mheshimiwa Waziri aje kutoa tamko la kuagiza kila jengo, hasa la kibiashara, kuwa na vitambuzi Moshi (smoke detectors) ili itoe taarifa ya awali kung’amua dalili za moto ndani ya nyumba, vilevile kuhakikisha vifaa vya kuzimia moto vinaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Traffic Police bado ni tatizo kubwa, kuna haja ya kuweka vifaa barabarani na kupunguza askari hawa ambao muda mwingi wanajali kuchukua rushwa badala ya kuelekeza watumiaji wa barabara kuzingatia usalama na kuwachukulia hatua madhubuti. Bado magari yasiyo na ubora wa kutumika yanaendeshwa, ilhali Askari Usalama wamejazana barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Wizara itafute Mwekezaji wa kuja kuwekeza kwenye vifaa vya ukaguzi wa magari kabla ya kuyapa leseni; vilevile waweke kamera barabarani na kutumia teknolojia ya kuwezesha kutambua magari yanayoendeshwa ili kutoa udhibiti na adhabu husika. Umefika wakati sasa ukaguzi ufanywe kidigitali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado Polisi wetu hawajaweza kushughulikia ipasavyo matukio ya ubakaji na udhalilishaji wa kijinsia ambayo yanaongezeka hata kuathiri watoto wachanga. Tunamwomba Waziri aoneshe kuguswa kwakwe na hili ili wananchi hasa wanawake wapate faraja kuwa mateso wanayopata mikononi mwa wanaume wao na watoto wao yatashughulikiwa kwa haki na usawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.