Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Waziri Mheshimiwa Mwigulu pamoja na timu yake yote kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Polisi Lushoto kilijengwa toka mwaka 1890 na kimejengwa na mkoloni. Mpaka sasa hakijafanyiwa hata ukarabati lakini DC anayeitwa Majidi Mwanga alipata pesa kupitia wafadhili na kujengwa jengo moja la utawala ambalo limejengwa mpaka kufikia usawa wa lenta. Mpaka sasa ni miaka minne imepita bado jengo liko vile vile na linazidi kunyeshewa na mvua. Kwa hiyo, niiombe Serikali ipeleke pesa za kumalizia jengo lile ili lisije likaangushwa na mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, kuna shida kubwa sana ya nyumba za watumishi. Nyumba zile za polisi ni za tangu mkoloni, zimechoka mno hazistahili kuishi askari wetu. Pamoja na hilo, askari wameamua kujenga nyumba za mabanzi ili waweze kuishi humo lakini kiuhalisia nyumba hizo za mabanzi hazistahili kuishi askari wetu ambao wanafanya kazi ngumu mno. Hivyo basi, niiombe Serikali angalau askari wetu wapate hata nyumba tano.

eshi la Magereza nalo gereza lao ni la muda mrefu pamoja na nyumba wanazoishi askari wetu siyo nzuri kabisa na hata nikisema hazistahili kuishi askari namaanisha. Hivyo basi, niiombe Serikali yangu Tukufu iiangalie Lushoto kwa jicho la huruma ili tuweze kuokoa maisha ya askari wetu. Kwani kwa maisha wanayoishi askari wetu wanaweza kupata magonjwa na kuhatarisha maisha yao ukizingatia nyumba zile walizojenga hazina hata sehemu ya kuchimbia choo kwa ujumla nyumba zile hazina vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jiografia ya Lushoto inajulikana kuwa ni ya milima na mabonde na wilaya nzima ina wakazi zaidi ya milioni moja lakini Jeshi la Polisi pamoja na Jeshi la Magereza hawana vitendea kazi. Hivyo basi, niiombe Serikali yangu ipeleke magari kwa ajili ya askari polisi na askari magereza. Hasa hawa magereza hawana kabisa magari wanapata tabu sana hasa katika utafutaji wa kuni. Hii imepelekea wafungwa kutembea umbali mrefu kufuata kuni na hii ni hatari kwa askari wetu wanaweza kutorokwa na wafugwa. Kwa hiyo, Serikali ituangalie Lushoto kwa jicho la huruma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tabia ya askari wetu wasio waaminifu kuwanyanyasa raia wetu kwa kuwalazimisha wawape rushwa. Wakikataa au kama hawana ndiyo wanaanza kuwabambikia kesi au kuwapiga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, askari wetu hawa hasa hawa askari trafiki wanawanyanyasa vijana wa bodaboda na vijana wanaoendesha Noah. Imefikia hatua hata kama dereva amepaki gari askari hutoa plate namba za gari tena kwa kuitoa kwa nguvu hadi ikatike na kusababisha uharibifu wa plate namba hiyo. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu ikemee kitendo hiki kinachofanywa na askari wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali yangu Tukufu itujengee vituo vidogo vya polisi katika maeneo ya Makanya – Kwemakame na Gare, kwani maeneo haya yana watu wengi sana na pia ndiyo maeneo ambayo yana matukio mengi ya kihalifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali yangu Tukufu, hizi pesa zinazokusanywa vituo vyetu vya polisi zote zisiende Serikali Kuu. Angalau zibaki hata 30% ili vituo vyetu viweze kukidhi mahitaji yao madogo madogo kama mafuta ya magari na kununua stationary.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vitambulisho vya Taifa, kazi hii inasuasua sana na huku wananchi wetu wanatuuliza kila siku. Hivyo basi, niiombe Serikali yangu ihimize mamlaka hii inayoshughulika na vitambulisho hivyo iongeze kasi hasa katika maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.