Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kunijalia asubuhi hii afya na uzima nikaweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyojua Wizara ya Mambo ya Ndani ni miongoni mwa Wizara za Muungano. Kwa hiyo, taasisi zake zote zilizomo katika Wizara hii zinapaswa zifanye kazi katika maeneo yote ya Tanzania Bara pamoja na Tanzania Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumzia kuhusu Jeshi la Polisi ambalo kwa mujibu wa utaratibu ndiyo ambao wanalinda mali na raia wa nchi hii kwa ujumla. Pia tamko hilo liko supported na Ibara ya 15(2)(a) na (b) cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano. Nasema hivyo kwa sababu nataka kuelewa hili jukumu la kulinda raia na mali zake lipo kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar au kuna mpaka baina ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu inaonekana dhahiri chombo hiki kikija katika maeneo ya Zanzibar labda kuna vyombo vingine ambavyo vimepewa majukumu haya ya kufanya kinyume na ule utaratibu wa kuweza kulinda raia na mali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninao mfano hai wa siku ya Alhamisi, tarehe 5 Aprili, katika Kijiji cha Mitambuuni, Jimbo langu la Mtambwe, Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba, kama alivyosema Mheshimiwa Khatib jana vijana sita wadogo kabisa, innocent, wapo mbali kabisa na hata maendeleo ya teknolojia maana hakuna umeme, hawana television wala hawana habari yoyote, ambao wana umri kati ya miaka 16 na mkubwa wao ana miaka 30 wamekamatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamekwenda watu sijui tuite ambao hawajulikani wakiwa na magari manne yenye namba za private, namba ambazo baadhi ya majirani walizichukua, wakawagongea, wakawachukua vijana hawa, nyumba tofauti wakawafunga vitambaa vya uso, wakawasweka katika magari wakaenda nao mahali pasipojulikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana hao wakapelekwa katika nyumba, kwa sababu wamefungwa hawakujua wamekwenda wapi. Kulipokucha asubuhi wazee wao na jamaa zao wakaenda katika Kituo cha Polisi cha Wete ambapo ni Makao Makuu ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba kuuliza, kwa sababu tumezoea mambo haya lakini mara nyingi tunazoea Polisi wanawachukua watu wanakwenda nao vituoni, lakini walipofika pale wakaambiwa hapa hawapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakaenda Makao Makuu ya Polisi Mkoa wa Kusini Pemba, Chakechake napo wakaambiwa watu hao hawapo. Vijana hawa baada ya siku nne vijana watatu katika sita, majina ninayo hapa, alfajiri wakatupwa mahali mbali kabisa na makazi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walipokuja vijijini wakaeleza wakasema kwa kweli sisi tunashukuru hatukufanyiwa mateso lakini wenzetu ambao tumebagulia wapo katika vyumba tofauti wana mateso ya ajabu. Sasa just imagine hali ya wazee na jamaa itakuwaje watoto wao wameambiwa wapo katika mateso makubwa kama hayo. Wale vijana watatu wakakaa ndani kwa siku 11 kuanzia tarehe 5 mpaka Jumapili ya tarehe 15 na wao wakaenda wakatupwa mahali wakiwa wamefungwa mikono na vitambaa vya uso. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni msiba mkubwa nchi kama Tanzania ambayo tunajivunia ni kisiwa cha amani, miaka 54 ya Muungano leo wanakwenda maharamia kwenda kuwachukua vijana wadogo. Waliporudi tulipokwenda kuwaona kwa kweli hali zao haziridhishi, wakikueleza mateso waliyoyapata basi huwezi kustahamili, unaweza kutoa machozi. Kwa kweli hali ni mbaya, wamepigwa kila eneo la mwili wao. Kwa hiyo, unaweza kujiuliza nyuma ya Jeshi la Polisi kuna nani ambaye ni super power ana-organize uharamia huu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni uharamia ambao kwa kweli unasikitisha mno. Kamishna wa Zanzibar yupo hapa ampelekee shukrani zetu RPC wa Kaskazini, katupa ushirikiano siku zote tulipokuwa tunakwenda lakini yeye muda wote alikuwa na yeye anasikitika, mimi hawa watu sinao jamani nendeni mkakague katika maeneo yangu yote, lakini unamhisi kuna jambo ambalo limefichika nyuma yake, anajua baadhi ya mambo. Yeye anasema hanao lakini anatupa moyo baada ya siku mbili au baada ya siku ngapi mtawapata watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha zaidi tumepeleka hata namba za gari, hapo ndiyo mwanzo, kama ni upelelezi unaanzia hapo. Tungetarajia kwa kupitia namba za gari zile watu hawa wangekuwa traced na wakajulikana na tunasikia wamehojiwa lakini mpaka leo wanadunda, hakuna ambaye amepatikana na ameshtakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ndiyo maana tukauliza, je, wajibu na jukumu la Jeshi la Polisi hasa kule Zanzibar kuna watu mme-delegate powers kwao, wao ndiyo washughulikie usalama lakini wakati huo huo washughulikie mateso ya watu? Hapa ndipo ambapo tunapata shaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunamuuliza Waziri Inshallah akija hapa kutoa majumuisho, ni lini hawa watu ambao hawajulikani wataanza kujulikana na mateso haya yatakoma lini. Au kama hiyo haiwezekani basi atamke hapa leo akija Mheshimiwa Waziri kwamba sasa jukumu la kujilinda liwe lenu wenyewe wananchi. Tukishapata kauli hiyo tutajua namna gani ya kuweza kukaa kulinda wananchi, kujilinda wenyewe na mali zao, vinginevyo kwa kweli itakuwa hatuwafahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tungeomba kabisa nchi hii ni yetu sote, kama kuna mtu yeyote na kwa kawaida kila raia ni mtuhumiwa mtarajiwa. Mimi naweza kutuhumiwa leo lakini kuna utaratibu, niitwe polisi au popote pale nikahojiwe ikionekana labda kuna makosa nipelekwe katika vyombo vya haki (mahakama).

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani kwenda kumgongea mtu usiku ukamfunga kitambaa ukaenda ukamtesa bure. Mtakuja kuwaona wananchi ni wabaya kumbe wabaya wakati mwingine ni Jeshi la Polisi. Hii ni kwa sababu wao wameshindwa kuwalinda wananchi pamoja na mali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa niseme kwamba pamoja na yote hayo, tunaona kwamba polisi wana matatizo mengi katika maeneo yao ya kazi. Hata bajeti yao ya mafuta ni ndogo mno. Kwa mfano, hata tulipowaita wao kwenda katika site watu wale walipokuwa dumped kikwazo kilikuwa ni mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii.