Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia bajeti ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri kwa kazi kubwa ambayo wameifanya hasa katika kuandaa bajeti hii muhimu ya Kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nichukue nafasi hii kupongeza kwa dhati kwa kuondoa kodi kwenye taulo za kike ambayo ilikuwa ni kero ya muda mrefu. Tuna imani kubwa huu ni mwanzo mzuri na kwamba wananchi sasa hasa akina mama na watoto wa kike wataweza kunufaika kwa kuondolewa kodi katika taulo za kike kwa ajili ya kujihifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nichukue nafasi hii kupongeza sana kwa jinsi ambavyo wameweka kipaumbele cha kwanza kabisa kwenye suala la kilimo ikifuatiwa na suala la viwanda, hatimaye kwenye huduma za jamii na mwisho kabisa kwenye miundombinu muhimu wezeshi kwa ajili ya uchumi kukua. Nikianza kwenye sekta ya kilimo, ni muhimu sana kwa sababu asilimia kubwa ya Watanzania wanajishughulisha na kilimo. Kwa sababu hiyo Serikali ikiangalia suala la kilimo hasa ambavyo imezungumza kwamba itawezesha kuanzisha skimu za umwagiliaji, nipongeze sana kwa ajili ya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa tunalo Ziwa Viktoria na mikoa mingine kwa mfano Ziwa Tanganyika na maziwa mengine, tukianzisha skimu za umwagiliaji nina uhakika kwamba wananchi wataweza kunufaika, tutapata mazao ya uhakika mwaka mzima. Kwa hiyo, nipongeze tu na niombe sasa utekelezaji uwe ni wa kweli katika jambo hili, lisije tu kuonekana kwenye karatasi lakini kwenye vitendo halisi lisionekane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika suala la kilimo ni muhimu sana Serikali iangalie namna sasa ile Benki yetu ya Kilimo (TADB) ambayo tumeianzisha inavyoweza kufanya kazi. Hii benki kweli ipo lakini inapatikana mjini tu. Kwa mfano, kwenye Kanda yetu ya Ziwa Benki ya TADB inapatikana Mkoani Mwanza. Sasa mkulima wa kawaida siyo jambo rahisi kutoka Geita avuke kote kule mpaka Mwanza kwenda kuchukua mkopo kwenye Benki ya TADB. Kwa hiyo, Serikali iangalie sasa kujenga mazingira mazuri kuwezesha benki HII iweze kuwafikia wananchi hasa wakulima vijijini ili waweze kunufaika katika suala zima la kupata mikopo nafuu ili kujikimu na kujiendeleza katika shughuli mbalimbali za kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo pia, suala la wataalam katika sekta ya kilimo ni muhimu. Nasema hivyo kwa sababu mara nyingi katika vijiji vyetu siku hizi hakuna wataalam kabisa wa kilimo. Unakuta mtaalam mmoja anapatikana kwenye makao makuu tu ya kata ambapo wakulima wanapatikana vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa sasa Serikali imeweka kipaumbele kuboresha suala la kilimo, tuangalie uwezekano wa kuwa na wataalam wa kutosha kwenye vijiji na kata. Kikubwa zaidi wataalam hawa wafanye kazi zao vizuri kuwaelimisha wakulima badala ya kilimo tulichokizoea ambacho hakina tija, tuweze kubadilika kuwa na kilimo chenye tija na hatimaye tuweze kukuza uchumi wa Taifa letu.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika viwanda, nipongeze sana kwamba Serikali imejikita kujenga mazingira wezeshi ili wawekezaji wengi waweze kuingia ndani ya Tanzania na kuwekeza, pia hata wawekezaji wa ndani. Naomba sasa katika suala la uwekezaji na viwanda muwaangalie wafanyabiashara ambao kwa muda mrefu wafanyabiashara wengi wamekuwa na changamoto nyingi sana. Mimi natokea kwenye eneo ambapo kuna sehemu kuna biashara kubwa kwa mfano katika center moja ya Katoro, wafanyabiashara wana changamoto nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Serikali kwa ujumla iangalie namna ya kutatua kero na changamoto mbalimbali za wafanyabiashara ili waweze kuendelea kuwekeza zaidi kwenye viwanda kwa sababu bila kuwalea hawa wafanyabiashara wadogo ambao wapo sasa haiwezekani wakaweza kuwa wafanyabiashara wakubwa. Naomba katika fedha hizi ikiwezekana kuwepo na fedha kwa ajili ya kuwaelimisha zaidi wafanyabiashara wadogowadogo, kikubwa zaidi mazingira yao ya utendaji wa kazi yaweze kuwa mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kutokana na kwamba mara nyingi unakuta TRA wana-harass sana wafanyabiashara vijijini, wanakwenda pale mtu anarundikiwa kodi hapa na pale, kunakuwa na mazungumzo ambayo siyo mazuri. Nashukuru kwenye bajeti hii Waziri ametoa kauli kwamba kuwepo na urafiki kati ya TRA na wafanyabiashara. Napongeza sana statement hiyo, niombe sasa walioko kule kwenye wilaya na mikoa wahakikishe wanafanyia kazi jambo hili ili kuwezesha wafanyabiashara wadogo waweze kufanya biashara zao vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la huduma za kijamii ikiwemo sekta ya afya, naishukuru sana Serikali kwa sababu imewekeza sana kwenye afya. Nilikuwa najaribu kusoma katika mpango huu, sijaona mpango wa Serikali kuajiri watumishi wa sekta ya afya. Natoa msisitizo kwamba katika bajeti ya mwaka huu tuangalie namna ya kuajiri watumishi katika sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano tu kwenye Halmashauri yangu ya Geita tuna upungufu wa wataalam wa afya 200. Ndiyo maana kunatokea changamoto za vifo vya akina mama na watoto wakati wa kujifungua kwa sababu hakuna mtoa huduma katika zahanati au kituo cha afya. Kwa hiyo, napongeza kwa kazi kubwa kwamba tunajenga vituo vya afya na zahanati lakini tuongeze wataalam katika maeneo haya ili waweze kufanya kazi zao kusaidia wananchi, hasa ambao wanapata matatizo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu unakuta kituo cha afya au zahanati kina mtaalam mmoja au wawili, ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo, niombe Serikali kwa kuwa kwenye bajeti huku sijaona hilo, nimejaribu kuangalia lakini sikuweza kuona, nitoe tu msisitizo kwamba mwaka huu wa fedha tuajiri wataalam wa kutosha katika sekta ya afya ili kuwezesha akina mama na watoto waweze kuwa na afya pia waweze kufanya kazi zao vizuri. Unakuta hao hao wachache wanapata shida sana maana watu wanaosubiri huduma ni wengi. Kwa hiyo, wakati mwingine mtu anaweza akawa na majibu hata ambayo hayaeleweki kwa sababu amechoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile sekta ya maji ni muhimu sana hasa vijijini. Niombe tuweze kutekeleza kama ambavyo tumepanga, kwa sababu tulivyopanga hapa mipango ni mizuri sana. Nachoomba utekelezaji uweze kufanyika ili tuweze kuwafikia wananchi wetu katika kuwapa huduma kadri ambavyo Serikali imekusudia, otherwise bajeti iko vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa makusanyo, kuna changamoto kubwa sana. Kwenye matumizi ya vile vifaa vya kielektroniki kwa kweli kuna changamoto kubwa sana na ndiyo maana Serikali haipati mapato ya kutosha kwa sababu vifaa hivi havipatikani. Hata vilivyopo pale havifanyi kazi vizuri, unakuta unakwenda labda kituo cha mafuta lakini hupewi risiti, unaifuatilia risiti unaweza ukatumia nusu saa nzima kuipata. Kwa hiyo, watu wengi wanakata tamaa wanaziacha na mwisho wa siku Serikali haipati mapato yake sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango waangalie jambo hili kwamba namna gani tuweze kuboresha ili utoaji wa risiti na upatikanaji wa mashine hizi uwe mzuri. Kuna nchi nyingi za nje, nimebahatika kusafiri nje pia, kila ukipewa huduma yoyote mahali popote pale lazima utapewa risiti saa hiyo hiyo tena kwa haraka. Katika nchi yetu unapewa huduma labda ya mafuta lakini inakuchukua nusu saa kupata risiti, wakati mwingine unakata tamaa unasema labda niondoke. Niiombe Serikali hapo muendelee kuweka nguvu zaidi katika suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa zaidi tutoe elimu kwa wananchi kuomba risiti. Kwa sasa hivi elimu ipo lakini wanachi hawaombi zile risiti. Nnasema hivyo kwa sababu juzi tu kituo cha mafuta kina risiti nyingi watu hawachukui risiti zao. Kwa hiyo, Serikali iwekeze kwenye elimu ya mlipa kodi, kwa sababu bila ya kodi hatuwezi kupata maendeleo katika nchi yetu. Wananchi wana uelewa mkubwa wakielimishwa wanaelewa vizuri. Kwa hiyo niendelee kuomba Serikali kupitia Wizara husika tuendelee kutoa elimu hii na Wabunge tushirikiane kwa pamoja kuwaambia wananchi na wananchi wana uelewa mkubwa, tusisitize suala la kuomba risiti ni kitu muhimu sana ili kuweza kuchangia katika pato la Taifa.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa miundombinu, naipongeze sana Serikali kwamba imekusudia kujenga mradi mkubwa sana wa umeme Stiegler’s Gorge. Nina uhakika kwamba kupitia mradi huu wananchi tunaweza kupata umeme wa uhakika. Kikubwa zaidi niombe
sasa Serikali iendelee kusambaza umeme kwa kasi hasa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, napongeza sana Serikali na naunga mkono hoja. Ahsante sana.