Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia mawazo yangu na ya Wana-Igalula katika mpango na bajeti ya Serikali ambayo imesomwa na Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nitoe pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kusimamia uchumi wetu na kumshauri Mheshimiwa Rais katika kuhakikisha kwamba uchumi wa nchi hii unakwenda vema na mwisho wa siku maisha ya wananchi wetu yanakwenda sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ya Mipango na Bajeti amezungumzia mambo mengi, lakini nataka nimpongeze ameondoa baadhi ya kodi na tozo ndogo ndogo ambazo zilikuwa kero kubwa kwa wananchi wetu huko vijijini. Naomba nipongeze kazi kubwa ambayo inafanyika, tulishauri katika bajeti zilizopita kwamba uchumi wa nchi yetu unachangiwa sana na ubora na utendaji kazi wa bandari yetu. Sasa tunaona bandari yetu inaboreshwa, ni moja ya sababu itakayosababisha uchumi wa nchi yetu uende sawasawa. Napongeza sana kwa kazi kubwa inayofanyika pale katika bandari yetu ya Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia uanzishaji wa blue print, wafanyabiashara walikuwa wanalalamika taasisi nyingi za kutoza kodi lakini leo tunaenda kuzikusanya katika sehemu moja. Jambo hili litawarahisishia wafanyabiashara wetu kufanya biashara katika maeneo yao mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza pia ununuzi wa ndege. Tunataka kuimarisha uchumi wetu, tunataka tukusanye fedha za kutosha katika eneo la utalii, ni lazima tufanye maamuzi mengine ambayo baadhi ya watu wanayaona ni matatizo lakini huko tunakokwenda yataleta manufaa makubwa sana kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sisi wakazi wa Mkoa wa Tabora ujenzi wa reli ya standard gauge ilikuwa ni kilio chetu kikubwa sana. Kwa sasa usafiri wa reli siyo madhubuti sana, lakini kwa ujenzi wa standard gauge tunaelekea kwenye usafiri wa uhakika sana kwa sisi wakazi wa Mkoa wa Tabora. Hata tumbaku yetu inaposafirishwa kutoka Tabora kwenda sokoni, inatumia barabara na gharama zake zinakuwa kubwa. Kwa hiyo, ujenzi wa standard gauge utatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitoe mawazo haraka haraka kwa sababu najua muda ni mdogo, nianze na nukuu ya Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wa 79. Wakati anafanya hitimisho alisema, kujenga uchumi wa viwanda utachochea ajira na ustawi endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichangie sana hapa hasa kwa sisi tunaotoka vijijini, unapozungumzia uchumi wa viwanda na maisha ya wananchi wetu asilimia kubwa unazungumzia raw material. Raw material za viwanda hivi zinatokana na kilimo na asilimia 85 ya wananchi wetu wanategemea kilimo sasa kisipoboreshwa hata hili suala la kusema kwamba tunataka kukuza uchumi wa viwanda itakuwa ni tatizo. Viwanda vyetu vinategemea tumbaku, katani, mpunga na nyanya. Je, bajeti yetu inasema nini katika kuwawezesha hawa wananchi wetu kuweza kuendesha kilimo cha kisasa ambacho ni kilimo cha umwagiliaji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia bajeti tunayoimaliza sasa, kwa kweli katika eneo la umwagiliaji ni sawasawa na zero, hatujafanya kwa kiasi kikubwa sana. Naomba Mheshimiwa Waziri, tukitaka kuzungumzia uchumi wa viwanda tusiache suala la kusaidia kilimo cha kisasa hasa katika eneo hili la umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya sisi kuzalisha raw material tunatakiwa tusafirishe mazao yetu kwenda sokoni. Ni jambo la msingi sana kuiwezesha TARURA. TARURA inatengeneza barabara zetu za vijijini. Kama barabara za vijijini zitakuwa mbovu, usafirishaji wa mazao kutoka vijijini kuja kwenye soko pia ni tatizo, utaongeza gharama za raw materials hizo na mwisho wa siku itakuja ku-affect viwanda vyetu huko tunakokwenda. Tuiangalie TARURA na tuipatie fedha za kutosha ili iweze kutatua kero ya barabara zetu huko vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia uchumi wa viwanda, uchumi wa vidogo vidogo unaajiri kwa asilimia kubwa sana watu ambao wako katika maeneo yetu ya vijijini. Viwanda vidogo visipowezeshwa na hapa nataka nizunguzie SIDO, SIDO inatengeneza zana ambazo nyingi kati ya hizo zinatumika vijijini kwetu. Kama nilivyosema, viwanda vidogo vingi ndiyo vinatoa ajira ya kutosha. SIDO haijawekewa fedha za kutosha, naomba tuiangalie ili iweze kusaidia viwanda vidogo vidogo katika maeneo yetu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la umeme. Unapozungumzia uchumi wa nchi kama suala la umeme litakuwa ni tatizo, bado tutakuwa tunapiga mark time. Shida moja iliyopo pale ni bajeti tuliyoipitisha kupelekwa ili kutekeleza miradi iliyopo. Miradi mingi ya umeme vijijini kwetu kwa sasa inasuasua kwa sababu Wizara haijawezeshwa fedha za kutosha ili kutekeleza miradi hii. Hapa nataka nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya lakini tuwawezeshe fedha ili waweze kutekeleza miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la maji. Unapozungumzia uchumi maji ni jambo la msingi sana. Mwaka jana tulitenga shilingi bilioni 673 walipelekewa shilingi bilioni 347 tu. Tuli-survive na ile Sh.50 tuliyoipitisha hapa ya tozo ya mafuta, Wabunge wengi walishauri tuongeze Sh.50, hebu naomba tukubali tuongeze ile Sh.50 ili tupate Sh.100 tukatatue tatizo la maji. Tunahitaji tutengeneze miradi mikubwa ya umwagiliaji, tujenge mabwawa ya maji na kulipa wakandarasi wanaofanya kazi kule. Tukiongeza ile Sh.50 nina hakika kabisa miradi mingi ya maji itatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri sana kwamba tunapopitisha bajeti kupanga ni jambo moja na sisi tunatimiza wajibu wetu wa kushauri. Mambo mengi yanashindwa kutekelezeka kwa sababu bajeti tuliyoipanga na kuipitisha mara nyingi haiendi katika zile sekta husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Wizara ya Fedha ijitahidi kupeleka fedha zile ambazo tumezipitisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.