Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili nami niweze kutoa mchango wangu katika hizi hotuba mbili za Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango. Hotuba zote hizi zilizoletwa mbele yetu ni hotuba nzuri ambazo sisi kama wawakilishi wa wananchi tunao wajibu wa kuziunga mkono na kuhakikisha kwamba zinafanyiwa kazi ili Watanzania waweze kupata manufaa ambayo yamekusudiwa.

Mheshimiwa Spika, Waziri wa Mipango katika hotuba yake ya Uchumi wa Taifa katika mwaka wa fedha 2018/2019 ukurasa wa 28 mpaka 33 ameeleza miradi ya kielelezo. Miradi hii mingine tayari imeshaanza kutekelezwa ikiwemo ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge. Jambo hili ni jambo la muhimu kwa ajili ya ujenzi wa Tanzania ya Viwanda. Viwanda vitakavyokuwa vinazalisha mali au vitendea kazi mbalimbali vitakavyokuwa vinazalishwa kwenye viwanda ambavyo tunavitarajia vitahitaji kusafirishwa na sehemu ya muhimu ya kuweza kusafirisha vitu hivi ni reli.

Mheshimiwa Spika, Tanzania yetu ni Tanzania ambayo ina Watanzania wengi ambao ni wakulima na tunahitaji malighafi za viwandani ambazo zilizo nyingi zinatokana na kilimo. Kwa maana hiyo, ushauri wangu ni kuishauri Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kuhakikisha kwamba sekta hii ya kilimo nayo inapewa kipaumbele, hasa kuhakikisha kwamba mbolea inapatikana kwa wingi na kwa bei ambayo ni ndogo.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali ihakikishe kwamba viwanda vya mbolea vinajengwa hapa nchini kwa kasi kubwa. Kama ambavyo tumeona kiwanda kikubwa cha DANGOTE kimesaidia sana upatikanaji wa cement na kwa maana hiyo ujenzi wa nyumba na shughuli mbalimbali za ujenzi zimekuwa zikienda vizuri kwa sababu saruji inapatikana kwa bei ambayo ni rahisi kidogo.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, niombe tu Serikali iendelee kuhakikisha kwamba viwanda vya mbolea ambavyo tulikushudia vijengwe kutokana na kupatikana kwa gesi hapa Tanzania basi navyo vijengwe na vianze uzalishaji ili kusudi wananchi wetu waweze kuzalisha mazao ya biashara na chakula ili Tanzania ambayo tunaitarajia iwe Tanzania ya viwanda basi iwe na Watanzania ambao wanapata chakula na wanapata malighafi ambazo zinaweza zikafanyiwa kazi katika viwanda ambavyo vinazalishwa hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningeshauri Serikali yangu ni kuhakikisha kwamba viwanda vyetu vya zana za kivita; katika Mkoa wa Morogoro tunavyo vya Mzinga na Nyumbu. Niseme kabisa wazi kwamba Tanzania ya viwanda haiwezekani bila kuwa na Tanzania ambayo imeimarika kiulinzi. Kwa maana hiyo, niombe Serikali ihakikishe kwamba Mashirika yetu ya Nyumbu na Mzinga yanapewa pesa ya kutosha na kwa wakati ili kusudi basi majeshi yetu yaweze kuwa na zana za uhakika pindi hali ya hewa itakapokuwa imebadilika basi tuweze kukabiliana nayo. Ijulikane wazi kwamba katika mataifa yote ambayo yamefanikiwa kiuchumi pia yapo imara kiulinzi. Naishauri tu Serikali ihakikishe kwamba upande huu na wenyewe unafanyiwa kazi na unaeleweka.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali kwa kuja na mpango mwingine kabambe wa uzalishaji wa umeme. Najua kabisa kwamba sekta ya umeme ndiyo sekta mama ambayo inaweza kutusaidia kuhakikisha kwamba Tanzania yetu inakwenda haraka katika suala zima la ujengaji wa viwanda. Kwa hiyo, naunga mkono asilimia 100 ujenzi wa bwawa la uzalishaji wa umeme la Stiegler’s Gorge Serikali iendelee nalo na tuhakikishe kwamba tunakwenda kwa haraka sana ili tuhakikishe kwamba hizo megawatt 2,100 zinaingizwa katika Grid ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo nalo linatakiwa kwa kweli Serikali ilipe kipaumbele ni suala zima la viwanda vya chuma Liganga na Mchuchuma kule. Tumekuwa tukizungumza jambo hili kwa muda mrefu sana na kwamba kwa wale ambao wamekuwa wakiangalia vyombo vya habari wamekuwa wakiona ni jinsi gani ambavyo Watanzania wanapata shida sana ya upatikanaji wa vyuma. Matokeo yake sasa wanaingia hata kwenda kuharibu miundombinu ya barabara, wanaenda wanaokota vyuma vya kwenye barabara hata kwenye reli kwa ajili ya kuuza kama vyuma chakavu. Maana yake ni nini?

Mheshimiwa Spika, maana yake ni kwamba upatikanaji wa vyuma hapa nchini inaonekana ni mdogo na kwa hiyo kama supply inakuwa ni ndogo, matokeo yake sasa watu wanaamua kuchukua sasa scraper na vitu vingine ambavyo wakati mwingine ni vya maana kama alama za barabarani na zenyewe zinachukuliwa na kwenda kuuzwa kama vyuma chakavu ili kusudi viwanda vya vyuma viweze kufanya kazi. Kwa hiyo, niseme tu kwamba Tanzania ya viwanda bila kuwa na upatikanaji wa chuma kule Liganga na Mchuchuma kwa kweli tutakuwa bado ndoto yetu haitafikiwa kwa wepesi. Nije sasa katika suala zima la… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, nashukuru niseme kwamba kwanza naipongeza Serikali tena kwa kuja na mpango wake wa kujenga Makao Makuu ya nchi yetu na kuifanya Dodoma kuwa Mji Mkuu na Mji ambao kwa kweli sasa hivi umepewa hadhi ya kuwa Jiji, niseme tu Serikali iendelee kutoa pesa kwa ajili ya ujenzi wa mji huu ili uendelee kuwa mji wa kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri.