Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja iliyopo mbele yetu. Awali ya yote nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa uwasilisho wa bajeti nzuri ambayo tunaiona inatekelezeka.

Mheshimiwa Spika, nianze na suala la TRA. Katika Mji wa Njombe iko Ofisi ya TRA. Tunaposema kwamba ulipaji kodi unatakiwa uwe rafiki nadhani ni pamoja na mazingira ya kulipia kodi. Katika Ofisi ya TRA Njombe mazingira ni mabaya sana, jengo lile lina vyumba sita, limechakaa, linavuja lakini lina watumishi wachache sana. Matokeo yake ni kwamba kunakuwa na msongamano mkubwa sana, watu wanakwenda kulipa kodi siku mbili mfululizo anakaa TRA kulipa kodi.

Mheshimiwa Spika,Hii nayo inawavunja nguvu sana walipa kodi, niombe sana Serikali ilione hilo na itujengee jengo lingine lenye nafasi. Tuliambiwa kwamba kuna mpango wa kuhamisha TRA pale, lakini hatuoni kama kuna dalili ya kuhama leo wala kesho na makusanyo ya TRA Njombe ni zaidi ya bilioni 12 kwa mwaka. Kwa hiyo, haya ni makusanyo makubwa ukilinganisha na mikoa mingi ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nikiacha suala la TRA niende kwenye suala la kilimo. Njombe ni wakulima na katika kilimo yako mambo ambayo ni msingi sana yakatekelezwa kwa wakati. Jambo la kwanza kabisa ni suala la miundombinu inayowahusu wakulima, wakulima wanahitaji miundombinu ya barabara ili waweze kusafirisha mazao kutoka katika mashamba kwenda katika masoko.

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la pembejeo, pembejeo zimekuwa zikifika kwa kuchelewa sana kwa wakulima, hali ya barabara ni mbaya sana kwa wakulima. Niombe sana Serikali iangalie kwamba ni kwa namna gani sasa itaweza kuwawezesha wakulima wa mazao ya chakula na biashara waliopo katika Jimbo la Njombe Mjini ili kusudi waweze kufanya kazi yao vizuri, msimu wa mavuno waweze kusafirisha mazao vizuri.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kuna Kiwanda kipya cha Chai kimejengwa pale Rwangu, Njombe. Kiwanda kile kinahitaji chai nyingi sana na ile chai inalimwa maeneo mbalimbali sana ambayo hayana hata barabara. Kwa hiyo, ni jukumu sasa la Serikali kuona ni namna gani inawezesha kupeleka fedha za kutosha katika Jimbo la Njombe Mjini, kutengeneza barabara kwa ajili ya mashamba ya chai katika eneo lile.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia kilimo tunazungumzia na masoko, sasa hivi Njombe tumeanza kulima zao la parachichi na zao la parachichi linaiingizia fedha ya kigeni nchi. Sasa hivi tuna-export parachichi kwa wingi sana kutoka Njombe, lakini miundombinu yetu siyo rafiki. Kwa hiyo, inasababisha bei ya lile zao isiwe na ushindani, kwa sababu anatokeza mtu mmoja na kwa kuwa miundombinu inayotakiwa ni ile yenye ubaridi. Niiombe sana Serikali ilione hilo.

Mheshimiwa Spika, siyo hilo tu nikikumbuka huko nyumba wakati uwanja wa Ndege wa Songwe unajengwa tuliambiwa uwanja huu unajengwa Kusini kwa lengo kwamba uweze kusaidia kusafirisha mazao ya matunda na maua kwenda masoko ya Ulaya. Uwanja umekamilika, mazao yanalimwa lakini mpaka leo yanasafirishwa kwa malori. Wafanyabiashara wanasema mazao ya Njombe hayapati bei nzuri kwenye soko la dunia kwa sababu gharama ya usafiri iko juu sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wanasafirisha kwa malori kutoka Njombe mpaka Dar es Salaam, hebu tuone sasa hivi tumetengeneza wale wanaitwa white elephant au ni nini. Kwa sababu uwanja ule uko tayari, mazao yako tayari lakini hatuoni dalili ya kuona kwamba sasa tunaanza kuutumia ule uwanja. Tunakwenda na miradi mingi mikubwa, kama tunashindwa hii miradi ambayo ipo ilishakamilika ikiwemo TAZARA hakuna hata dalili ya kusafirisha mizigo kutoka Nyanda za Juu Kusini kupeleka kwenye masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaweza tukajikuta tunafanya miradi mikubwa mingine lakini bado ikawa haifanyi kazi. Sasa hivi tunakwenda kuhamasisha kuna soko kubwa sana ya njegere changa huko Ulaya na mahindi machanga yanahitajika yakiwa fresh, tunahitaji miundombinu ambayo itatusaidia kusafirisha haya mazao kwa ajili ya masoko ya huko Ulaya na haya mazao yanaleta fedha ya kigeni moja kwa moja. Naomba sana hilo jambo liweze kutiliwa maanani kwamba Uwanja wa Ndege Songwe na TAZARA - Makambako wawekewe miundombinu yenye ubaridi ili kusudi waweze kusafirisha haya mazao fresh kwa ajili ya masoko ya nje na wafanyabiashara hawa wapate unafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la maji. Katika Jimbo la Njombe suala la maji limekuwa gumu sana.

Nimeshangaa sana kuona kwamba inaonekana suluhisho la maji kwenye Mji wa Njombe na miji mingine ni kutungwa kwa sheria inayompa idhini Waziri wa Fedha kutoa msamaha wa kodi. Jambo hili tumelizungumza miaka mitatu, miaka mitatu yote kwenye bajeti fedha inaoneshwa kwamba kuna miradi ya maji, kuna mkopo nafuu toka India. Kumbe tatizo ni sheria ilikuwa inagomba miaka mitatu!

Mheshimiwa Spika, nasikitika sana nikiangalia jinsi Baraza la Mawaziri na Serikali yetu ilivyosheheni wasomi jambo kama hili linachukua miaka mitatu kupata ufumbuzi, je, huo utekelezaji utakuwaje sasa? Sasa tunapitisha hii ili kusudi Waziri apate hiyo idhini, niombe sasa watekelezaji watakapoanza kutekeleza hii miradi, ikiwemo mradi wa maji wa Njombe Mjini waone kwamba mradi huu wananchi wamekosa huduma kwa miaka mitatu. Kwa hiyo, waende na kasi ya kufidia hiyo miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la fedha za maendeleo. Fedha za maendeleo kwenye Halmashauri zetu haziletwi na sisi ambao vyanzo vyetu kama vile vyanzo vya kodi ya majengo vimechukuliwa inatuumiza sana. Tumejenga zahanati, tunashindwa kuezeka, tumebaki na mapagale. Sasa nashindwa kuelewa kwamba ikiwa Serikali imechukua vyanzo vya mapato kama vya kodi ya majengo ikidai kwamba itafidia halafu haitufidii, tumejenga zahanati katika Kijiji cha Mamongolo, Kata ya Makoo; tumejenga zahanati Kifanyo, tumejenga zahanati Luponde, tumejenga zahanati Magoda tunashindwa kumalizia zahanati hizi kwa sababu tu hatuna fedha na Serikali fedha za maendeleo haituletei.

Mheshimiwa Spika, hebu niombe basi Serikali ione kwamba ili twende sawa kwa sisi ambao vyanzo vya mapato ambavyo ni haki yetu kabisa, vyanzo vya mapato vya kodi ya majengo vimechukuliwa, tupewe basi hizo pesa tuweze kumalizia hayo majengo. Kuna wakati wameita Wakurugenzi wa kila Halmashauri wamefika hapa wamepewa maelekezo, wameandika na kila kitu lakini mpaka leo fedha haitoki. Niombe sana jambo hili lifanyike ili kusaidia maendeleo ya maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la elimu. Ukiangalia kwenye kitabu cha Bajeti cha Mheshimiwa Waziri anasema nchi hii inawahitimu laki laki nane kila mwaka, lakini wanaopata bahati ya kuajiriwa ni wahitimu 40,000. Kwa hiyo, watu zaidi ya laki saba wanabaki bila ajira na watu hawa hawana ujuzi wowote zaidi ya kujua kusoma na kuandika. Kila wakati nasimama hapa naelezea kwamba hebu tusaidie nchi hii tuweke shule za ufundi katika shule za Kata ziwemo shule za ufundi.

Mheshimiwa Spika, watu wote hapa wang’ang’ana VETA, hatuna uwezo wa kujenga Vocational Schools leo zikatosheleza nchi hii, lakini njia rahisi ya kufanya tubadili baadhi ya shule za Kata ziwe shule za ufundi ili kusudi tuokoe kundi kubwa la vijana. Tutawasaidia vijana hawa watakuwa wamepata elimu ya ufundi ili waweze kujitegemea hivi hapa ugumu uko wapi au ni nani atamke? Naomba sana jambo hili lifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtazamo wa walio wengi wanaona kabisa kwamba kitu cha ufundi ni kitu kikubwa sana lazima kuwe na ma-workshop kuwe na mashine za ajabu ajabu, lakini nimekuwa nikieleza hapa mara zote kwamba jambo hili wala siyo kubwa kiasi hicho. Hebu twende turudi chini tuangalie tulifanyie kazi, tuweke mpango ambao utasaidia angalau kila Halmashauri iwe na fani angalau moja mbili katika shule zake za Kata kuzifanya kuwa za ufundi ili ziweze kufundisha vijana wapate maarifa na baadaye waweze kujitegemea.

Mheshimiwa Spika, tusipofanya hivyo, tatizo la kujiajiri kwa vijana halitakaa lipate suluhisho, italeta shida sana kwa maana ya kwamba wanaomaliza elimu ya msingi na wanaomaliza elimu ya sekondari ni wengi sana. Kwa hiyo, elimu ya ufundi ndiyo ukombozi na elimu ya ufundi siyo inapatikana kwenye Vyuo vya Ufundi tu kwa maana ya VETA, tunaweza kabisa kuzifanya shule zetu za sekondari zikawa sehemu ya mafunzo ya ufundi na ikawa imesaidia vijana wengi kupata hayo maarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.