Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Spika, nami nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili kuweza kutoa mchango wangu kwenye hoja hii iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha, pamoja na Naibu wake pia niwapongeze Watendaji walioko ofisini kwao, Katibu Mkuu pamoja na wote walioko ofisini kwa kufanya kazi kwa juhudi kubwa na hatimaye kutuletea bajeti ambayo ni nzuri kwa kweli na ni bajeti ambayo inaleta matumaini makubwa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, bajeti hii ni nzuri kwa sababu moja imeweka vizuri kodi ambazo zilikuwa zinasumbua hasa wakati huu tunapotaka kujenga uchumi wa viwanda. Hakuna kodi iliyoongezeka kuzidi kiwango hata mahali ambapo kodi zimeongezeka na hasa wazalishaji wetu wa ndani, bajeti hii imewaangalia vizuri kwa kweli. Wasiwasi wangu tu ni huu utambulisho wa electronic tax stamp, sijaelewa sawasawa kama kweli haina matokeo ambayo ni hasi kwa mlaji na wazalishaji. Tutajifunza huko mbele, tutaona pengine haitakuwa na matokeo haya. Lakini vinginevyo kama ina matokeo chanya basi tutakwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuzungumzia mapato yetu ya ndani. Mapato yetu ya ndani yanaendelea kuongezeka lakini ongezeko kubwa liko kwenye kodi. Mapato yasiyotokana na kodi bado ni madogo sana, bajeti iliyopita kutokana na hotuba hizi zilizosomwa hapa, mapato yasiyo ya kodi ilikuwa trilioni 1.7 na mwaka huu ambao bajeti yake tunaijadili mapato yasiyotokana na kodi yanakadiriwa yatakuwa trilioni 2.16. Sasa kitakachokusanywa bado hatuelewi.

Mheshimiwa Spika, mapato haya siyo makubwa sana na mapato haya yanatakiwa kuwa makubwa kwa sababu ni lazima sasa yaweze ku-supplement mapato yanayotokana na kodi. Mapato yanayotokana na kodi bado ni madogo kwa sababu uchumi wetu unatawaliwa na sekta isiyo rasmi kubwa sana, kwa sababu sekta isiyo rasmi ni kubwa basi hatupati kodi ya kutosheleza huko. Sasa lazima tutafute namna ya kongeza mapato yasiyo ya kodi. Tunaweza kuyaongeza kwa namna mbili tu ambazo napendekeza hapa.

Mheshimiwa Spika, moja ni kufanya Ofisi ya TR isimamie vizuri makampuni na taasisi za Serikali ambazo zinazalisha. Kusema ukweli TR anatakiwa awezeshwe kiasi cha kutosha kabisa ili aweze kusimamia vizuri mahali ambapo Serikali ina stake, kwenye kampuni ambazo Serikali ina stake, TR asimamie vizuri kuhakikisha tunapata mapato ya kutosha kule. Pia taasisi zingine na ikiwezekana taasisi ambazo hazizalishi au ni mzigo kwa Serikali basi tuweze kuondokana nazo, kwa nini kuendelea kuzipa ruzuku, kuendelea kuzipa pesa wakati hazizalishi na haziongezi mapato yoyote kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo la pili ambalo kama nchi tumeendelea kulizungumza kwa muda mrefu, suala la uvuvi kwenye Bahari Kuu. Inasemekana tunapoteza shilingi trilioni moja kila mwaka kwa sababu ya kutoweka maanani uvuvi kutoka kwenye Bahari Kuu. Sasa Serikali imekuwa na maelezo tofauti kwamba wanafanya upembuzi yakinifu ili kutengeneza bandari ya uvuvi, lakini huu mwaka ni wa tatu niko kwenye Bunge lako bado upembuzi yakinifu unaendelea.

Mheshimiwa Spika, sasa nadhani umefika wakati kwamba sasa tuanze uvuvi wa Bahari Kuu ili utusaidie kutuongezea mapato yasiyo ya kodi. Vinginevyo tutaendelea kuimba wimbo wa namna hii, bado tutakuwa na mapato chini tutakuwa na mapato duni na hivyo tunapotaka kufika 2020 au 2025 tuwe na uchumi wa kati itatuchelewesha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la pili, suala la maji. Suala la tozo ya maji kwenye mafuta. Suala la maji ni muhimu sana kwenye nchi yetu kwa sababu mbili pia. Kwanza maji tunayataka sisi kama binadamu kwa matumizi yetu mbalimbali, lakini pia maji tunayataka kwa ajili ya kilimo chetu. Kilimo chetu kwa sababu ya kutegemea mvua kimekuwa kilimo cha chini, kimekuwa kilimo ambacho hatuna uhakika hata tukilima kama tunaweza kuvuna. Tukiweka nguvu kubwa kwenye maji tuna uhakika na kilimo na tuna uhakika wa kuwapatia watu wetu maji ambayo wanahangaika usiku na mchana mahali pengi.

Mheshimiwa Spika, mimi natoka kijijini kabisa, kijiji changu tunachota maji kilomita saba kwenda, kilometa saba kurudi. Sasa suala la maji ni suala kubwa na ni suala muhimu sana kwenye nchi yetu. Tuliomba Serikali iongeze shilingi 50 kwenye maji. Serikali inasema haiwezi kuongeza kwa sababu itaongeza mfumuko wa bei. Mfumuko wa bei unaoongezwa na mafuta ni wakati mafuta yamepanda bei huko tunakoyanunua, lakini kwa muda wa miaka miwili sasa na huu ni wa tatu nadhani, mafuta hayajaweza kupanda sana kwenye soko la dunia kiasi kwamba yakipanda, pengine tukiyanunua kwa gharama ya juu kule hapa tutajiletea inflation (mfumuko wa bei) imported inflation, lakini mafuta hayajapanda sana huko kwa wenzetu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja.