Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja iliyoko mezani. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na wakati huo huo nawashukuru wapiga kura wa Urambo wanaoendelea kunipa ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali na hasa Wizara inayohusika, Mawaziri wote na watendaji wote kwa kazi nzuri waliyoifanya na hasa kwa bajeti hii ambayo inalenga kujenga uchumi wa viwanda utakaochochea ajira na ustawi endelevu wa jamii.

Mheshimiwa Spika, nimeangalia ukurasa wa 40 ambako kumetolewa maelezo wazi kabisa kwamba bajeti hii itaangalia suala la upatikanaji wa maji vijijini kama walivyopendekeza pia Kamati inayohusika, pia itazingatia suala ala afya. Hapa naomba niikumbushe Serikali kwa upande wa afya, pamoja na jitihada nzuri zinazofanywa na Serikali, bado tuna tatizo kubwa sana la uhaba wa wafanyakazi. Tunaomba suala la wafanyakazi lipewe kipaumbele; na pia uendelezaji wa ujenzi wa Vituo vya Afya ambavyo bado vinahitajika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa elimu pia imeelezewa, lakini nielezee tu kwamba, kuna kifungu hiki kimoja katika ukurasa wa 40 ambacho nimekipenda sana, ila naomba Mheshimiwa Waziri wakati wa kuhitimisha afafanue. Kinasema: “Aidha, mahitaji ya makundi maalum katika jamii yetu; wanawake, vijana, watoto, watu wenye ulemavu na wazee wataendelea kuangaliwa kipekee.’ (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha, atueleze ‘kipekee’ maana yake ni nini? Je, wenzetu wenye ulemavu wa ngozi wategemee mafuta wanayotumia pengine yatapunguzwa bei? Je, wenzetu wasioona watapata pengine fimbo za kutembelea? Tunaomba aneo hili liwekwe wazi ili watu waendelea kuishi kwa matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Wabunge Wanawake na Wabunge Wanaume wanaotuunga mkono katika kutetea haki za wanawake na watoto wa kike, naipongeza sana Serikali kwa ukurasa wake wa 46 ambapo wametamka wazi kabisa kwamba wanaondoa kodi katika taulo za kike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe ni shahidi, hii ajenda ni ya wanawake wote chini ya Chama chetu au Umoja wetu unaoitwa TWPG. Tumekuwa tukilizungumzia suala hili kwa muda mrefu na nachukua nafasi hii pia kuishukuru Serikali, imekuwa ikikubali kuwaleta Wawakilishi wao katika vikao mbalimbali ambavyo tumekaa pamoja ili kuhakikisha kwamba hili leo walilolitamka linafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kwa niaba ya wanawake wa Bungeni wote kuishukuru sana Serikali kwa ukurasa wake wa 46 ambao umekubali kupunguza kodi ya ongezeko la thamani. Nimefanya hesabu hapa, nimeona kwamba VAT asilimia 18 kwa taulo za kike zinazouzwa Sh.2,000/= zitakuwa zimepungua kwa Sh.360/= na kwa taulo za kike ambazo zitauzwa kwa Sh.3,500/= gharama itapungua kwa Sh.630/=.

Mheshimiwa Spika, tumechukua hili kwa uzito wake kwamba angalau Serikali imefikiria. Ndugu zangu akinamama na akinababa mnaotuunga mkono, tuipongeze Serikali kwa hatua hii. Kwa sababu kwa watoto wa kike wanaoshindwa kwenda shuleni kila mwezi kutokana na kukosekana kwa taulo za kike, wanapoteza siyo chini ya siku nne au tano. Kwa hiyo, kwa nusu muhula wanapunguza karibu wiki tatu wanashindwa kwenda shuleni na ukichukulia kwa muhula mzima wanashindwa kwenda shuleni kwa wiki sita na kwa miaka minne kuanzia form one mpaka form four, wanapoteza wiki 24 za kutokwenda shule.

Mheshimiwa Spika, tumezungumzia sana habari za utoro kwa watoto wa kike na kwa taarifa au utafiti uliofanywa na UNESCO umeonesha wazi kwamba katika watoro wa kike 10, mmoja anashindwa kwenda shule kutokana na ukosefu wa taulo za kike. Kwa hiyo, hii hatua ya Serikali tunaipongeza sana nikiamini kwamba pengine itachukua hatua zifuatazo ili huu msamaha huu wa kodi uwe na manufaa zaidi:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, tunaiomba Serikali iwashawishi wawekezaji wa viwanda wengi zaidi wawekeze katika eneo hili. Viwanda vikijengwa vingi, hizi taulo zitapatikana kwa wingi zitasaidia pia hata kushusha bei zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, tunaiomba Serikali sasa, katika malighafi zitakazotumika kutengeneza taulo za kike, VAT pia iondolewe, yaani wapate msamaha wa kodi ili malighafi zipatikane kwa bei nafuu ili wengi zaidi watengeneze taulo hizo. Tunaiomba Serikali, siyo iwaombe tu wafanyabiashara kupunguza bei, hapana; tunaomba hata ikiwezekana itoe bei elekezi ili angalau hizi taulo za kike zipatikane. Naamini, ndugu zangu kwamba hizi taulo za kike kupunguziwa kodi ni hatua ya kwanza. Tunaiomba kwa heshima Serikali tukitegemea kwamba iko siku itafikiria kutoa hizi taulo za kike bure kwa kadri ya uwezo wa bajeti utakavyowezesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kuja na uamuzi wa kuondoa riba katika mikopo inayotolewa kwa akinamama na vijana. Tunaomba hili suala liendelee, sheria itakapowekwa vizuri, basi kusiwe na riba yoyote katika mikopo.

Mheshimiwa Spika, itakuwa sikutenda haki kama sikukutaja wewe siku ya leo kwamba umekuwa mstari wa mbele kutuunga mkono akinamama tunapoangalia vipingamizi vya watoto wa kike kuhudhuria shule. Moja ilikuwa ni hili la taulo za kike ambalo Serikali imelifikiria, lakini la pili ni uhaba wa vyoo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vyoo vingi karibu asilimia 52 vinavyotumiwa na watoto wa kike havina milango. Kwa hiyo, tunakupongeza wewe kwa kutuunga mkono kwa fund raising tunayoitegemea tarehe 22 Juni, 2018, ili tuchangie upatikanaji wa vyoo vya kike, tutoe vyoo vya mfano ili vyoo vitakapojengwa sasa viweze kumsitiri mtoto wa kike na wa kiume pamoja na walemavu. Tunakushukuru sana kwa kutuunga mkono kwa suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nililotaka kuzungumzia ni suala la kodi za mazao. Tumbaku ifikiriwe pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nakupongeza wewe kwa kutuunga mkono.