Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na mimi kunipa nafasi nitoe mchango wangu kwenye hii bajeti iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niombe tu kusema kwamba hii bajeti tatizo kubwa haiakisi maisha ya wananchi wetu wa kawaida na ndiyo maana kuna baadhi ya watu wengine wanasema hii bajeti ni bajeti hewa, kwa sababu ukiangalia kwenye vipaumbele vilivyoandikwa hapa haijaakisi kabisa maisha ya wananchi wetu wa chini. Kwa mfano, kwenye miradi hii ya kipaumbele, ukiiangalia hata kwenye bajeti wamesema kwamba hailetewi fedha za kutosha, hakuna fedha ambazo zimeenda huko fedha za kutosha. Kwa mfano, wamesema kwamba miradi ya kipaumbele kama vile Rufiji. Rufiji mwaka jana ilitengewa shilingi bilioni 220 hivi lakini wakaipeleka shilingi bilioni tatu, sasa unashindwa kuoanisha tatizo liko wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo kubwa ambalo naliona bajeti hii inaanza kuharibika tangu kwenye mipango. Mipango tunayopanga na tunapokwenda kutekeleza tunatengeneza vitu tofauti. Niwatolee mfano, kwenye mipango utakuta kuna miradi ya LNG, Mkuza, kuna huo mradi wa Rufiji, kuna Special Economic Zone, kuna makaa ya mawe, kuna General Tyre, mambo ya barabara na kufungamanisha kwamba uchumi na maisha ya wananchi. Lakini tunapokwenda kutekeleza, tunatekeleza vitu vingine ambavyo havimo kwenye mpango.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kwenye bajeti iliyopita hapa nimesikia kuna majengo ya Chuo Kikuu ambayo hayakuwemo kwenye mpango, lakini yamejengwa, kuna ujenzi ule wa Magomeni Quarter umeanza kujengwa lakini kwenye mpango haukuwemo, kwenye ukuta pamoja na kwamba ni jambo zuri kwenye huo ukuta wa Tanzanite, haukuwemo kwenye mpango lakini umejengwa. Kwa hiyo, utakuta kuna miradi ambayo inakamilika ujenzi wake, haimo kwenye mpango, lakini ile miradi ambayo imo kwenye mpango hailetewi fedha. Kwa hiyo, kufeli kwa bajeti hii kunaanzia tangu kwenye mipango yetu kwa sababu tunachokipanga sicho tunachokitekeleza. Tunapanga kama Taasisi, kama mpango, Wachumi wanakaa wanapanga lakini inapokuja kwenye utekelezaji mtu anatoa matamko mengine yanafanyika mambo mengine, matokeo yake zile fedha ambazo zilitakiwa ziende huku, zinaenda huku. Kwa hiyo kwa msingi huu, nasema kabisa kwamba bajeti hii haiwezei kukidhi matakwa ya wananchi wetu.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tunaingia kwenye nchi ya viwanda na uchumi wa kati, hivi kweli kama tunakisahau kilimo, hatutaki kuwekeza kwenye kilimo tuna dhamira kweli ya kwenda kwenye viwanda? Haiwezekani kwenye bajeti ukapanga asilimia 0.4 ziende kwenye kilimo, kilimo ambacho kinaajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania halafu mkasema kweli tuna nia thabiti, mimi siwezi kuunga mkono jambo hili. Kwa mfano, unaona kwamba mifugo imepangiwa 0.1, uvuvi ndiyo kabisa, mmeua mmepangia 0.06 maana yake tuendelee kula wale samaki wa China ambao wanakuja miaka mitatu iliyopita. Sasa tunaposema kwamba hii haiakisi maisha ya wananchi tunamaanisha hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano mimi natoka Liwale, wananchi wangu kule ni wakulima siyo wafugaji, wale ni wakulima lakini sasa naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, wakulima wale mimi nikawaambie nini kwenye bajeti hii? Sisi zao letu la uchumi kule ni zao la korosho, mmeshalihujumu, zile export levy zimeshapotea, mpaka leo hii hatujui mbolea, pembejeo tunapataje! Hivi mimi watakaponiuliza kwamba bwana eeh! umekaa Dodoma miezi mitatu unachangia bajeti, hivi kama wananchi wa Liwale tumeletewa nini wakulima? Sasa hivi hawana uhakika wa ufuta, yaani bei za ufuta hazijulikani, masoko hayajulikani.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi hapa mmetangaza kwamba zao la ufuta litanunuliwa kwa stakabadhi ghalani, mmewapa Bodi ya Maghala ndiyo washughulikie hilo, lakini mpaka leo hawajaandaa chochote na ufuta sasa hivi ndiyo uko sokoni, kwa hiyo, mipango hii tuanyopanga haiakisi maisha ya wananchi wetu. Tunaposema hii bajeti siyo rafiki kwa watu wetu tunamaanisha hiyo kwa sababu wengine mipango hii hatunufaiki nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano nakuja kwenye hoja ya kufungamanisha, mnasema kwamba mnaenda kuandaa akaunti moja (collection account) kwamba mapato yote ya nchi hii yakusanywe kwenye akaunti moja halafu Serikali au Hazina ndiyo wagawe. Jambo hili siyo sahihi sana pamoja na kwamba nia yenu ilikuwa ni nzuri. Kwa mwenendo wa upelekaji wa fedha za mafungu haya kwenye Halmashauri zetu au kwenye Taasisi husika na hii sasa mnakwenda kuua. Mmeshaiua Halmashauri, tumejua vyanzo vyote vya Halmashauri mmevichukua mkavipeleka Hazina na hamrudishi, sasa hivi mnaenda kuua mifuko, hii mifuko ambayo ilitengewa fedha maalum.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo sababu juzi nilikuwa nachangia, Waziri wa Fedha nilikuwa nachangia kwamba Serikali hii ya Awamu ya Tano hatuoni fedha zile ambazo zilikuwa za mafungu maalum zamani kiingereza wanaita, kuna fedha ambazo zilikuwa ring fenced, sasa hivi kwenye Awamu ya Tano hizo fedha hazipo tena na sasa hivi ndiyo maana mnaleta hii sera kwamba mnataka kuweka akaunti moja ili muendelee kuua hiyo mifuko na mnapoua hiyo mifuko maana yake, kwanza mlitakiwa mjiulize kwa nini hii mifuko iliundwa, je, yale mahitaji ya hii mifuko imeondoka? Na kama mahitaji ya hiyo mifuko bado ipo kwa nini sasa mnaiondoa? Kuiondoa hii mifuko maana yake sasa mnakwenda kuua malengo yaliyopangwa kwenye hiyo mifuko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kodi ndiyo maana bajeti zetu zinashindwa kutekelezeka, kwa mfano kwenye miradi ya maendeleo hatujawahi kufika asilimia 50 ya utekelezaji wa bajeti yetu. Pamoja na kwamba mmeongeza, walipa kodi wameongezeka mkumbuke kwamba walipakodi wameongezeka lakini kiwango cha kodi kinachokusanywa kinazidi kupungua. Kwa mfano, kwenye page ya tano ya kitabu cha Mwenyekiti amesema; tatizo la kupungua kwa shughuli za uwekezaji nchini ndiyo sababu inayosababisha uchumi wetu kudorora wameeleza
kabisa kwamba shughuli za uwekezaji zimepungua. Sababu nyingine wamesema mitaji inahamishwa na hapa tulishawahi kuwaambia kwamba wafanyabiashara kwa mazingira haya mliyowawekea sasa hivi wafanyabiashara wanahamisha mitaji. Wafanyabiashara wanahama, tukiwaambia mnakataa, matokeo yake ndiyo haya kwamba watu mitaji wanahamisha na mazingira ya uwekezaji bado siyo mazuri, kodi zimekuwa nyingi hazielewekina usumbufu vilevile. Kwa hiyo, haya mambo yote haya tunashindwa kuelewa, mipango yetu hii inatupeleka wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kama mnazo hizo mnazoita Economic Zones, pesa hampeleki! Halafu Economic Zone zingine ambazo tayari watu wamelipwa ili kuacha uwekezaji pale uendelee halafu uwekezaji hakuna, maana yake pale kwanza wamepoteza fedha za kulipa watu fidia halafu hatuna mipango. Hatuna mpango ambao tunaweza kwenda kuutekeleza.

Sasa hii mimi nashindwa kuelewa, hasa mmeshindwaje ninyi kama Serikali kufungamanisha kilimo na viwanda? Msitegemee hizi nyanya ambazo mnazikuta hapo Morogoro, hizi nyanya watu wachache wanaweka pale barabarani ndizo ambazo mnataka kuvijengea viwanda. Hebu fungueni milango watu wawekeze kwenye kilimo, watu wakija kuwekeza kwenye kilimo ndipo mtaweza sasa kuendeleza hivyo viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitolee mfano mmoja, jana Spika alisema hapa anashangaa kwa nini bajeti ya Kenya iko juu kuliko ya kwetu, sababu wenzetu wa Kenya wamejiwekeza kwenye kilimo, sisi tumekataa kuwekeza kwenye kilimo. Asilimia 60 ya nafaka inayosindikwa Kenya ni ya kwao wenyewe lakini sisi asilimia 98 ya nafaka inayosindikwa Tanzania ni kutoka nje. Mfano mzuri mimi nilikuwa msindikaji wa nafaka wa aina ya ngano, asilimia 90 ya ngano inayosindikwa Tanzania ni ya kutoka nje, kwa nini? Ardhi tunayo, tena ardhi nzuri lakini hakuna uwekezaji na wala hamfikirii kutafuta wawekezaji kwenye kilimo cha kisasa, kilimo cha kibiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.(Makofi)