Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja iliyopo mezani kwetu. Nianze kwa kuwapongeza viongozi wa Wizara hii; Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu kwa kazi nzuri ambayo wameifanya hadi wakaja na Kitabu cha Bajeti. Mchango wangu utajikita kwenye Sekta ya Kilimo na itajikita sana kwenye zao la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge aliyemaliza kuongea sasa hivi, amezungumzia Export Levy na Mheshimiwa Bundala muda fulani alizungumzia Export Levy. Nami nitaendeleza hapo hapo, kwamba kwa miaka mitatu mfululizo, tumeona Serikali ikiufanya uwekezaji mkubwa sana kwenye zao la korosho, kwa hili naipongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilianza kutoa tozo ikaweka matumizi sahihi ya fedha ya Serikali kwenye Mfuko wa Zao la Korosho na Bodi ya Korosho na hata kufikia hatua ya kuvunja Bodi ya Korosho. Mwisho ikatolewa incentive kwa wakulima, mwaka 2017 zikatolewa pembejeo ambazo wakulima walipewa bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji huo ulifanya uzalishaji wa korosho uwe double. Kwa sababu uzalishaji wa korosho nchini, mwaka 2015/2016 ilikuwa tani 155,000. Mwaka 2017 ilikuwa tani 315,000, kwa uwekezaji mdogo tu huo. Nasikitika sana kwamba kinachoendelea mwaka huu ni kudhoofisha Sekta ya Korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulianza majadiliano na Mheshimiwa Waziri wa Fedha atakumbuka, tulienda ofisini kwake kama Wabunge wa Mkoa wa Mtwara na Lindi wanaozalisha zao la korosho, kuhusu upatikanaji wa fedha za pembejeo. Alitujibu vizuri tu kwamba kuna kasoro kwenye ile sheria, kwa sababu Sheria ya Korosho ilisema fedha hizi zitatumiwa baada ya kutengenezwa kanuni. Mheshimiwa Waziri wa Kilimo alitengeneza kanuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake sasa, tunaona ukurasa wa 69 kwamba Serikali inadhamiria kwamba ile Sheria ya Tasnia ya Korosho ambayo ilikuwa inakusanya korosho, asilimia 35 zinakwenda kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali na asilimia 65 zinakwenda kwenye uendelezaji wa zao la korosho. Sasa inakusudiwa kufutwa na nimechungulia kwenye Finance Bill ipo, inafutwa ili fedha zote ziingie kwenye Mfuko Mkuu. Hapa tunaua korosho. Hapo wanafanya siasa ya Mikoa ya Mtwara na Lindi iwe ngumu. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, kwa hili tuungane. Kwa taarifa ya Kituo cha Utafiti Naliendele sasa hivi, wamejikita kwenye Mikoa 17. Kwa hiyo, wale wenzangu wa Chunya, Singida na Tabora, fedha hii ikiondoka hawatawaona wataalam wa Naliendele wanakwenda kwao kwa ajili kuliendeleza zao la korosho. Kwa hiyo, tuungane ili fedha hizi zirejeshwe, Kituo cha Utafiti Naliendele kifanye kazi yake, nao wazalishaji wapya wa korosho wapate hayo matunda ambayo yameonekana kwenye zao la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye hili kuna changamoto nyingi sana, kwa sababu madhara yake, kama nilivyosema kwanza, sasa hivi hakuna kinachoendelea kwenye sulphur. Inasikitisha sana, mwaka 2017 Serikali ilileta tani 28,000 hazikutosha, lakini mwaka huu tuliambiwa kwamba zimetolewa shilingi bilioni 10 kupelekwa TFC ili waagize pembejeo ya sulphur, hakuna hata kilo 50 ambayo imeeingia sasa hivi nchini. Shilingi milioni kumi hizi zimekuwa dana dana. Kwa hiyo, mwaka huu wakulima wamechanganyikiwa kuhusu sulphur. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, fedha hizi zingetumika kulipa vikundi vidogo vidogo vya wazalishaji wa miche ya mikorosho. Kwa bahati mbaya sana wakulima hawa au vikundi hivi walishazalisha hiyo miche, miche imeshachukuliwa kwa wakulima, hawajapewa hata shilingi. Kwa hiyo, Mbunge ukionekana kule unazunguka zunguka wanakwambia Mbunge fedha zetu tulizotumia kuzalisha miche ya mikorosho bado hazijatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shughuli ambayo itaenda kuua kabisa tasnia ya korosho ni kwamba asilimia ya fedha hizi zilikuwa zinakwenda Kituo cha Utafiti Naliendele kwa ajili ya utafiti wa zao la korosho. Kule hali ni mbaya. Tulikutana na wataalam wanasema kule hakuna kinachoendelea. Madhara ya kwanza ni upungufu wa mbegu za korosho. Mbegu za korosho lilikuwa jukumu la Kituo cha Utafiti Naliendele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapoondoa fedha hizi na wao wamesimamisha uzalishaji wa mbegu za korosho. Kwa sababu kuna mikoa mipya 17 ambayo imeingia kwenye uzalishaji wa korosho, mahitaji yao wao ni tani 165 za korosho. Kwa hiyo, mwaka huu hizo hazitaingia kwenye tasnia ya korosho. Madhara ya pili ni kwamba watashindwa kuendeleza kilimo cha korosho kwenye maeneo mapya. Kama nilivyosema, Chunya, Kyela, Singida na Tabora, walishaanza uzalishaji. Kwa hiyo, wale hawatawaona tena wataalam kutoka Naliendele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masikitiko yetu makubwa ni kupotea kwa ajira. Kituo cha Utafiti Naliendele kilikuwa kinatumia sehemu ya fedha hizi kwa ajili ya ajira ya watumishi wa pale, takriban watumishi 77 watapoteza ajira na kituo kile sasa hivi kuna ajira za kudumu watumishi wawili tu, madereva. Kwa hiyo, fedha hii inapokosekana, Kituo cha Utafiti cha Naliendele kitapoteza watumishi 77 na kitabaki na madereva wawili tu. Hebu angalia tasnia ya korosho inavyoteketea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Dkt. Mpango asiingie kwenye kumbukumbu mbaya kuua zao la korosho katika nchi yetu. Hebu naomba tutafakari hili turejeshe. Naelewa kwamba lengo lake ni kufanya matumizi mazuri ya fedha hizi, tusimamie, kama udhaifu ni Watendaji wa Bodi ya Korosho, tuwawajibishe, lakini siyo kuchukua fedha shilingi bilioni 211 ambazo zingeingia katika kuendeleza zao la korosho na kuzipeleka kwenye Mfuko Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili ni kuhusu produce cess, ushuru ambao Halmashauri au mamlaka ya Serikali za Mitaa zinatakiwa kulipwa. Sheria inasema kwamba wapewe 3% ya farm gate price. Kumekuwa na upotoshwaji wa sheria hii unaofanywa na Wizara ya Kilimo na Bodi ya Korosho. Wanachaji 3% kwa bei dira, siyo sahihi. Kwa 3% inatakiwa iwe bei ya mnadani, ndiyo ushuru ambao unatakiwa uende Halmashauri na mlipaji sio mkulima, ni mnunuzi wa korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufanye marekebisho hayo, tusimamie vizuri. Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba imefika mpaka Mahakamani. Kwanza ilienda kuomba ushauri Ofisi ya AG Mtwara. Ofisi ya AG Mtwara ikajibu vizuri kabisa kwamba definition ya Farm Gate Price ni bei ya mnadani na siyo bei dira. Kwa hiyo, naomba hii wakati wa kufanya majumuisho, Mheshimiwa Waziri na hususan Waziri wa Kilimo, aiagize Bodi ya Korosho kwa sababu kila msimu huwa anatoa mwongozo; aiagize Bodi ya Korosho msimu ujao watoze ushuru wa Halmashauri kwa bei na mnadani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi fedha zinazoenda kwenye Halmashauri siyo sadaka, zinatumika kwa ajili ya Maendeleo ya Halmashauri zetu. Halmashauri zetu vyanzo vingi tumewanyang’anya. Wamebaki na produce cess tu. Sasa walipwe kile wanachostahili na siyo 3% ya bei dira, iwe 3% ya bei ya mnada. Hii inawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Mheshimiwa Waziri wa Kilimo aiagize Bodi ya Korosho isi-charge hii 3% kwa mkulima, sheria iko wazi kabisa. Anayelipa produce cess ni mnunuzi (buyer). Mkulima akifika sokoni, hatakiwi kuchajiwa hiyo produce cess, anayetakiwa kulipa ni mnunuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi.