Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuongea siku ya leo kuchangia Hotuba hii ya Waziri wa Fedha. Jambo la kwanza napenda nitoe pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Waziri kwa namna ambavyo amejitahidi kukusanya mapato ya Serikali, mpaka kufikia Aprili amesema amefikisha asilimia 74.3. Kwa kweli amejitahidi sana kwa sababu nyingi ambazo tunaziona na nitazieleza mbele ya safari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo kuna mambo mawili, matatu ambayo inabidi tuyaongelee ili kuweka sawa na kumpa nguvu ili aweze kukusanya zaidi.

Mheshimiwa Spika, ukweli uliokuwepo kama msemaji aliyetangulia alivyosema, vyanzo vingi vya mapato havikusanywi ipasavyo. Kwa mfano mdogo ambao upo kwa kila mmoja, kuna sekta moja ya kodi ambayo kwa asilimia kubwa haikusanywi, kodi hii ni ya withholding tax.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia wakazi wengi wa mijini zaidi ya asilimia 80 pamoja na sisi Wabunge tuliopo humu ndani tunapanga nyumba ambazo tunaishi kwa sasa, lakini ukiangalia kiasi ambacho kinakusanywa kwenye kodi hizi kama withholding tax kwa kweli ni kiasi kidogo sana. Hata wafanyabiashara walio wengi maeneo ya mijini, vibanda vyote vilivyopo mjini vinapangishwa na wafanyabiashara nao bado hawalipi withholding tax.

Mheshimiwa Spika, kwa jambo hili kama kweli TRA wangekuwa very serious wakiwa wana watumishi wengi wa kuwafuatilia kwa kila nyumba ambapo wapangaji wapo, kodi hii ikapatikana, naamini gap kubwa la kodi au mapato lingeweza kuzibwa kutokana na kodi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hiyo, tukiangalia taarifa yake, halmashauri zimeweza kukusanya mapato yake hadi Aprili kwa asilimia 64. Hapa kuna tatizo na tatizo hili ni kwamba usimamizi wa makusanyo ya Halmashauri umekuwa ni mdogo sana. Kwa kuwa makisio ya mapato ya Halmashauri yanatolewa na wao wenyewe, kwa hiyo vyanzo vile ambavyo wanavitoa wana uhakika wa kukusanya, ni kwa nini hawafikii kiwango cha kuridhisha ili kuleta mchango mzuri wa maendeleo katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, jambo hili nilisikia mwaka jana Waziri mmoja alisema kwamba kuanzia mwaka wa fedha ujao halmashauri yoyote ambayo itashindwa kukusanya angalau kwa asilimia 80 ya makisio yake basi halmashauri hizo zijiandae kuondolewa. Je, mpaka sasa mpango huo ukoje, kwa inaonekana wanakisia kitu ambacho wanashindwa kukikusanya?

Mheshimiwa Spika, naomba sana Halmashauri nazo ziangalie wale wanaoshindwa kukusanya basi hatua ile ichukuliwe ili nafasi wapewe halmashauri nyingine zilizo kubwa kama Tunduru ambayo inaweza kukusanya zaidi ya asilimia 100 kutokana na makisio yake.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nitaliongelea kwa uchungu mkubwa sana ni suala lililopo kwenye ukurasa wa 69 wa hotuba yake ambayo naona inahusiana na sheria zinazosimamia bodi za mazao. Naomba kwa ruhusa yako nisome kwa sababu ni mistari michache ili niweze kutoa mchango mzuri wa kuweza kumshauri Mheshimiwa Waziri namna ya kufanya. Amesema:-

“Mheshimiwa Spika, napendekeza kufanya marekebisho kwenye sheria zote zinazosimamia Bodi za Mazao mbalimbali kwa lengo la kuwezesha ushuru wote unaokusanywa na bodi hizo kuingizwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Lengo la hatua hii ni kuhakikisha kwamba mapato yatokanayo na ushuru unaotozwa kwenye mazao mbalimbali yanasimamiwa ipasavyo na kutumika kwa ajili ya shughuli zilizokusudiwa. Aidha, shughuli za kuendeleza pamoja na gharama za uendeshaji wa bodi zitagharamiwa kupitia bajeti ya Serikali.”

Mheshimiwa Spika, walivyoanzisha bodi hizi na mazao ilitokana na changamoto za uendeshaji wa kuendeleza mazao mbalimbali likiwemo zao la korosho na ndiyo maana zikaanzishwa bodi ili kusimamia mazao haya yaweze kuzalishwa kwa wingi na baadaye tuweze kupata fedha za kigeni kwa ajili ya kuendeleza Pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, nitaenda kwenye zao la korosho; mwaka 2008 wadau wa zao la korosho walikubaliana kuanzisha export levy ambayo katika makubaliano ikaundwa sheria mwaka 2009 na katika sheria ile kama tulivyoeleza siku za nyuma, tulikubaliana kwamba asilimia 35 ya mapato yaende Mfuko Mkuu wa Serikali na asilimia 65 irudi kuendeleza zao la korosho.

Mheshimiwa Spika, huu ndio ulikuwa mkakati wa wakulima wenyewe baada ya kuona kwamba korosho zimekuwa zikiyumba na uzalishaji umepungua na tunamshukuru Mwenyezi Mungu tangu mwaka 2009 tulivyoanza kutumia sheria hii, uzalishaji umeendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka mpaka msimu uliopita tukapata zaidi ya tani 300,000. Katika tani hizo 300,000 Serikali ilikusanya zaidi ya bilioni mia moja hamsini na nne. Kati ya hizo, bilioni mia moja na kumi zilitakiwa zirudi kwenye sekta; nina mashaka na mapendekezo haya.

Mheshimiwa Spika, kama Serikali imeshindwa kurudisha kwa muda wa miaka miwili pesa hii ambayo tayari imezungumzwa kwa sheria kwamba asilimia 65 irudi kuendeleza zao husika la korosho, leo tunachukua pesa hii na tunabadilisha kwamba ziende moja kwa moja kwenye Mfuko Mkuu, nina mashaka kwamba yale yaliyotokea miaka miwili hii ambayo mpaka leo wakulima wa korosho tunalia yataendelea kujitokeza na hatimaye zao la korosho na mazao mengine yatauawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni kwa sababu dhamira na nia ya kuanzisha bodi hizi ilikuwa ni kulisaidia zao lenyewe ili liweze kujiendeleza baada ya kuonekana Serikali kupitia bajeti ya Serikali yenyewe imeshindwa kuendeleza haya mazao. Njia mbadala ilikuwa ni wakulima wenyewe kujinasua kwa kuanzisha hizi bodi na mifuko mbalimbali ambazo walianzisha tozo na ada mbalimbali zilizokubaliana na wakulima wenyewe ili kuendeleza mazao haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiki kilio alichokizungumza Mbunge wa Kilwa ni kikubwa sana maeneo mengi ya Tunduru ambako wanategemea uzalishaji wa korosho kulingana na hii fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba, kwa kuwa haya ni mapendekezo, mapendekezo haya hayana tija kwenye bodi zetu za mazao kwa sababu zinaenda moja kwa moja kuua uzalishaji wa mazao na kama tulivyosema asilimia 20 ya export ya nje, pesa ya kigeni inategemea na mazao yetu.

Mheshimiwa Spika, tukiangalia mwaka jana zao la korosho peke yake liliingiza zaidi ya trilioni 1.2, pesa za Kitanzania kwa ajili ya mauzo yake. Kwa maana hiyo, kama pesa zile hazitaenda kuhudumia zao kwa maana kwamba uzalishaji utapungua na hili lengo linalosema Serikali inaweza kupata fedha nyingi kutokana na hii pesa kupelekwa kwenye Mfuko Mkuu maana yake itashuka.

Mheshimiwa Spika, naomba sana, kwa kuwa dhamira ni nzuri basi haya madeni ya nyuma yaende kuhudumia wakulima ili na sisi wanasiasa twende tukawaeleze wananchi wetu kwamba kuanzia mwaka wa fedha ujao tarehe 1 Julai mfumo utabadilika pesa hii itakuwa inapelekwa moja kwa moja Serikalini na kuamuliwa matumizi kwa njia ambayo amependekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana jambo hilo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Ahsante sana na naunga mkono hoja.