Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DKT. STEPHEN L. KILUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa niweze kuchangia katika hii hoja ya Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuanza kwa kutanguliza shukrani zangu za dhati kwa Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa jinsi ambavyo inaendesha mambo yake katika kupeleka uchumi wa nchi hii mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa nasoma hiki kitabu cha Hali ya Uchumi wa Taifa nimeona kwamba nchi yetu kweli inaelekea kuzuri maana hakuna jua halijageuzwa katika kupeleka maisha ya Watanzania mbele. Sekta za elimu, madini, maji, barabara, usafiri wa anga, you name them, ziko nyingi; kwa hiyo napenda pongezi zangu za dhati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi pia naomba niipongeze Wizara. Mheshimiwa Waziri jina lake ni Dkt. Mpango na jina linaumba na mipango yake ni safi. Nimesoma hotuba yake imepangiliwa kweli kweli, ushauri wangu ni kwamba haya yaliyoandikwa humu tujipange basi sawasawa katika kuyatekeleza.

Mheshmiwa Mwenyekiti, pia naomba niipongeze Kamati, Kamati ya Bunge imefanya kazi nzuri na mahiri kabisa katika kuandika kitabu chake hiki, na yale mapendekezo yaliyopo nayaunga mkono na naomba yafanyiwe kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo basi naomba nijielekeze katika baadhi ya mambo ambayo na mimi nimeya-note katika hotuba hii na ningeweza kutoa mapendekezo au ushauri wangu. Kwanza naomba pia kuungana na wenzangu ambao wamesifia marekebisho na mapendekezo ya kufutwa kwa kodi mbalimbali, ikiwemo ile ya taulo za kike kwa sababu tunaelewa itawasaidiaje watoto wetu wanaosoma shuleni na wale ambao itawasaidia katika kuzipata kwa bei ambayo naamini itakuwa na punguzo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza pia kuondolewa kwa kodi ya virutubisho kwenye vyakula vya mifugo, isipokuwa nasikitika kwamba hii haitagusa wafugaji wa asili. Sasa huo msamaha usije ukachukuliwa kwamba wafugaji wana kitu kikubwa cha kushangilia hasa wale ambao hawafugi kisasa. Najua dhamira ilikuwa ni kuhamasiha ufugaji bora na wa kisasa, lakini naomba niishauri Serikali kwamba nchi hii kwa asilimia 99.9 bado inategemea mazao ya mifugo ya asili. Nyama inayoliwa ni asilimia 99.9 ya Watanzania ni nyama ya ng’ombe, mbuzi na kondoo
wanaochungwa kiasili. Kwa hiyo bajeti hii ifikirie namna ya kuinua uchumi huo wa mifugo kwa kuiongezea tija na kuiwekea mikakati thabiti ya kuilea hiyo sekta maana bado ni ya muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa sababu wanajitahidi katika kuwawezesha wafugaji wa asili kupata mbegu bora, lakini mbegu bora itakuwa haina maana kama vitu vingine muhimu vipaumbele vya mfugaji havijazingatiwa na vipo vinne nikivitaja kimoja kimoja. Kwanza ni malisho; malisho ni ya muhimu sana na malisho yabainishwe na kutambulika kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ni maji, kukiwa na malisho bila maji bado kutakuwa na mgogoro mkubwa wa jamii zetu za kifugaji kulazimika kuacha hata malisho yenye majani hasa katika yale mapori yetu katika wafugaji waliopo Ngorongoro, Longido, Monduli, Simanjiro, Kiteto wakaenda kwenye maeneo yaliyohifadhiwa na kuleta ile karaha kubwa ambayo tunaona kila siku wakifukuzwa na kupigwa faini kubwa kubwa ambazo zinawadidimiza katika umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, ili kushamirisha hii sekta ya mifugo ni kuhalikisha kwamba wanapatiwa dawa za tiba na dawa za chanjo na Serikali iiweke ruzuku kama inavyoweka katika mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni masoko ya uhakika ya ndani, maana sisi tunaoishi mipakani kule katika Wilaya yangu kama ile ya Longido wafugaji wale hawana sababu ya kupeleka ng’ombe Kenya, wanakwenda kwa sababu hawapati soko la uhakika la ndani; na wanapata karaha kule. Kuna watu wanaitwa middle men, madalali wanachukua wale ng’ombe ndio wanauza sokoni wewe unakaa unangojea, unapewa kile ambacho kitakachopatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masoko ya ndani yatakapoboreshwa na sisi Watanzania tutaweza kujivunia ufugaji wetu na wafugaji ambao ni jamii kubwa na ambayo inafuga mamilioni ya ng’ombe inayofanya Tanzania iwe nchi ya pili katika ufugaji Afrika hawatakuwa na sababu ya kupeleka ng’ombe nje na watafarijika kuona kwamba Serikali yao inawajali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilipenda kuchangia ni kwenye hili suala la asilimia kumi zinazotakiwa ziende kwenye miradi ya maendeleo ya akinamama, vijana na walemavu katika mapato ya ndani ya halmashauri zetu. Nimesoma hotuba ukurasa wa 40 nikaona kwamba niishauri Serikali kwamba hiyo asilimia kumi, pamoja na kwamba si kiwango kikubwa sana lakini imesaidia na tumeshaona matokeo yake katika Wilaya zetu, zile Wilaya ambazo hazina mapato ya kutosha ya ndani Serikali iwape ruzuku. Hilo ni la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, naomba basi iongezwe asilimia mbili ili iwe ni asilimia kumi na mbili kwa ajili ya kundi muhimu ambalo limesahahulika, kundi la wazee. Sasa fomula itakuwa kwamba, wanawake watapewa asilimia nne, vijana watapewa asilimia nne, walemavu watapewa asilimia mbili na wazee watapewa asilimia mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri hicho kipengele cha wazee ni cha muhimu sana kwa sababu wazee wetu wanaona kama wao wamenyanyapaliwa, wakati wanawake wamebainishwa tofauti na vijana; na najua katika kundi la vijana kuna vijana wa kike na wa kiume. Katika kundi la wazee inaonekana hatujasema wanawake na wazee, tumesema wanawake tu, kwa maana hiyo wazee wamenyanyapaliwa katika hili, kwa hiyo naomba Serikali izingatie hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo napenda kuchangia ni eneo la hii sekta ya utalii. Sekta hii ya utalii ni moja ya sekta muhimu na ni mhimili wa uchumi wa nchi yetu, ukichukulia kwamba ziko tatu za msingi, kilimo chenye mazao na mifugo na uvuvi ndani yake, utalii na
madini; hiyo ndiyo mihimili ya uchumi wetu. Sasa katika hili eneo la utalii ambalo linachangia asilimia 17.7 ya Pato la Taifa na asilimia ishirini na tano ya fedha za kigeni zinaingia katika nchi hii sijaona kwenye bajeti kama wameainishiwa vizuri mikakati iliyowekwa katika kuendelea kuitunza na kuiendeleza zaidi ya kutoa ahueni fulani kwa magari ya kitalii, sijaona mambo mengine ya msingi ambayo nilitegemea kwamba yangeongezwa ili sekta hii iendelee kukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba, ili hii sekta iendelee kuimarika na kuboreka, suala la miundombinu ndani ya parks (National Parks) zetu lipewe kipaumbele. Suala la kutangaza utalii ndani na nje lipewe kipaumbele, suala la kutanganza utalii wa fukwe zetu na liendelezwa lipewe kipaumbele, mambo ya kale, uwindaji, utalii wa kitamaduni, utalii wa usiku...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie pia kwa kusema kuna kero za kodi mbalimbali ambazo wawekezaji wa utalii wanalalamika.