Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Ahmed Mabukhut Shabiby

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Gairo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Leo nitachangia kiasi tu. Kwanza nianze na ile shangwe ya akinamama kwa kuondolewa kodi ya taulo za kike. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kutoa kodi hii, lakini bado tuna wasiwasi na sio wasiwasi kwamba bei itakuwa ipo pale pale. Kwa sababu ametoa kodi kwa nia nzuri, lakini cha msingi lazima aangalie aweke na bei, kwamba itauzwa bei gani? kwa sababu ukitoa kodi yule mwenye duka hawezi akajua hiyo kwamba imetolewa kodi wala haitofahamika na hivyo yeye atauza bei ile ile; kwa hiyo manufaa kwa wananchi hayatakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunaomba aangalie namna ya kurekebisha, kwamba waweke na kiwango cha bei, kwamba hii itauzwa kiasi fulani ili wale wenye maduka wasiweze kujipatia faida hii ya ushuru ambao umetolewa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwenye Viwanda, kwa kweli ameonesha nia nzuri sana ya kuweza kunyanyua viwanda vya nchi hii; na wale watu ambao kweli wana nia ya kuanzisha viwanda huu ndio wakati wao. Nasema hivi kwa sababu bajeti hii imeonesha kabisa na ipo wazi kabisa, kwamba kama unaweza kuanzisha viwanda anzisha na Serikali inakuunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano kwenye mafuta, ameongeza ushuru kwenye crude oil na viwanda vya Tanzania vya ndani ya nchi kama mawese ametoa ushuru. Ila tunamshauri, hata kwenye mashudu nayo hajayaekezea vizuri, nayo atoe ushuru wake ule wa ongezeko la thamani (VAT).

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huu nataka niwaambie wafanyabiashara, wakati huu wa Serikali ya Awamu ya Tano ndio wakati wa kufanya biashara. Kwa sababu bado watu wanadanganyana danganyana hali mbaya, TRA inafilisi, sijui nini, huku na benki nazo ndio zimeshusha Interest. Sasa huu ndio wakati wa kukopa, hela zimejaa, wakati watu wanaogopa sasa ndio wakati watu kukopa na kufanya biashara, ukichelewa hapa ndio biashara imekwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa cha msingi tu, nataka nitoe ushauri na nataka niseme ukweli; kwamba hapa inaonekana kabisa Mawaziri wetu wanafanya kazi lakini ushirikiano haupo, ni zero. Kwa sababu unataka kuanzisha viwanda vya mafuta lakini ushirikiano wa Waziri wa Viwanda na Waziri wa Kilimo uko wapi? Maana unapiga kelele uanzishe kiwanda cha mafuta ya alizeti wakati kwa wakulima hamna lolote wala hakuna support ya aina yoyote ili wazalishe alizeti kwa wingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaanzisha kiwanda, kwa mfano kama hapa Dodoma ukiweka kiwanda inatakiwa kiwe kimoja tu na hata hivyo hakitoshi kwa sababu alizeti yote hii ya Dodoma inakwenda Singida. Kwa hiyo hata ukianzisha kiwanda kingine hawatoweza kupata alizeti za kutosha. Mbegu ya alizeti inayotumika Tanzania inatoa 22 percent ya mafuta wakati South Africa kuna mbegu inatoa 60 percent. Nataka kusema hapa Mawaziri hapa maneno mengi, ushirikiano hakuna, vitendo hakuna; huu ndio ukweli na lazima tuambiane ukweli; tusipoambiana ukweli hapa, tukianza kuogopana, tutasalimiana, tutakunywa chai lakini ukweli ndio huo; wengine ndio maana sasa wanafikia hamna sifa wanaenda kupima samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunafanya tu, ukiangalia ile video inakuangalia hamna kitu. Nataka nimtafute Mheshimiwa Rais kwa wakati wangu, ntamwambia mzee hawakusaidii hawa pangua tena, si dhambi kupangua pangua Mawaziri mara nne, mara tano. Waangalie, maana Mawaziri ukiangalia kwenye nchi hii wanaofanya kazi kwa moyo kabisa hawazidi watano. Wengine nao wamekuwa walalamikaji kama sisi Wabunge, tukikutana humu, aaa’ nchi hii’, mimi naogopa’, yaani hawahawa ndio wanaichafua, halafu mnapiga kelele; hawa ndio wanaomchafua Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bora hata upate adui mpinzani wa chama kuliko mpinzani wa ndani ya Serikali, mbaya zaidi kwa sababu humjui. Kwa hiyo, naomba Wizara hii, Mheshimiwa Dkt. Mpango ana shida sana, ana shida sana kutokana na Mawaziri wengine kutokupa support, huo ndio ukweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine nilisikia kina tajwatajwa hapa, mimi nafanya biashara, kwa hiyo nitakiongelea kila siku kama nitaona kinaenda tofauti. Kuna Mbunge mmoja hapa nilikaa naye hataki yeye TIPER itumike, anataka mafuta yakija yaingie moja kwa moja kwenye madepo ya kampuni binafsi, hicho kitu hakiwezekani. TIPER imejengwa tangu enzi ya Mwalimu Nyerere kwa ajili ya kudhibiti kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mfumo unaotumika sasa hivi ndio mfumo sahihi, wakati ule hizi kampuni nyingi hazikuwepo. Ili Serikali ijue mapato yake lazima mafuta yote yaende sehemu moja, yakitoka kwenye meli moja kwa moja yaende TIPER. Wakati huo ndivyo ilivyokuwa, hizi kampuni nyingine zote; Oryx, Gapco, zote hazikuwepo hizi. Puma zilikuwa hazipo, Oilcom, nani, hawakuwepo hawa. Kwa hiyo wakati ule yakienda TIPER ndio yanaenda Esso,Agip na Shell. Sasa hivi anakuja mtu anasema hiyo italeta leakage, sijui na nini. Yakifika pale TIPER, wewe kama una lita milioni tano utasubiri Milioni tano zako utapata zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikwambie kwa nini wanafanya hivi? Wanafanya hivi kwa sababu kampuni chache hizi zinapanga hata bei, kwamba hawa sasa tuwagonge hivi. Sasa hivi vikampuni vya Watanzania vidogo vidogo hivi ndivyo vinavyoshusha, vinasababisha na wao washuke. Kwa hiyo nia yao ni kuuza kampuni ndogo ndogo ili wabaki wao; na kila mtu akiweka mafuta kwao wanachukua karibu kwa metric tons wanachukua dola ishirini. Kwa hiyo wanajua yakienda kule wao watakosa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)