Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami kabla sijaendelea, nachukua nafasi hii kuunga mkono Azimio lililoletwa na Mheshimiwa George Simbachawene. Ninaunga mkono Azimio hilo na niseme tu kwamba ukweli ni kwamba jambo hili wala siyo jambo la kukurupuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 151 ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi iliielekeza Serikali ndani ya miaka mitano ihakikishe kwamba Serikali imehamisha Makao Makuu ya Serikali kutoka Dar es Salaam kuja Dodoma. Ibara hiyo ya 151 iliweka bayana mambo ambayo hata azimio hili limeyaelekeza. Ilani ilisema la kwanza; Serikali ihakikishe kwamba majengo yote ya Serikali yaanze kujengwa Dodoma kitu ambacho tumeanza kukifanya. Ilani imeelekeza, viwanja vipimwe katika Mji wa Dodoma Makao Makuu kwa ajili ya shughuli za Serikali na wananchi wa Tanzania. Mheshimiwa Jafo, amesema na ndivyo tunavyofanya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ilani imeelekeza itungwe sheria ya kutambua Dodoma kuwa Makao Makuu, ndiyo azimio ambalo linaletwa leo. Kwa hiyo, tuna kila haja ya kuunga mkono Azimio hili lililoletwa na Mheshimiwa George Simbachawene. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme yafuatayo: sisi kama Serikali tunampongeza sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Serikali zote zilizotangulia nakubaliana sana na Mheshimiwa Komu zilitengeneza mazingira wezeshi, lakini maamuzi ya kuhamia Dodoma kulifanya Dodoma kuwa Jiji, kuifanya Dodoma kuwa Makao Makuu yamefanywa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na anastahili kupewa pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kusema tunapohamia hapa Dodoma sasa, tumeweza kutekeleza, tumetekeleza kwa vitendo na tunapotekeleza kwa vitendo na kumuenzi Marehemu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, maneno haya aliyatamka Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na sisi tumeyatekeleza mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niliarifu Bunge hili, mnaposema kwamba kuna mgongano wa wafanyakazi kuhamia hapa Dodoma, ninaomba niwaambie kati ya wafanyakazi 7,440 wa Wizara zote wanaotakiwa kuhamia hapa Dodoma tumebakiza wafanyakazi 909 tu, wengine wote wameshahamia hapa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya wafanyakazi hawa kuhamia hapa Dodoma, Waheshimiwa Wabunge wanafikiri kutakuwa na migongano ya miundombinu, lakini mpaka sasa mmeona Dodoma ni shwari na shughuli za Serikali zinatekelezwa kama inavyotakiwa na hakuna tatizo lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikuthibitishie, kama Serikali tutaendelea kulisimamia agizo hili la Mheshimiwa Rais, kutekeleza matakwa ya Marehemu Baba wa Taifa na azma ya Ilani ya Uchaguzi Ibara ya 151. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiona adui yako anakusifia, ujue umeharibu, lakini ukiona adui hasifii unachokifanya, ujue umefanikiwa. Kwa hiyo, sisi tutaendelea kuifanyia kazi azma hii njema ya kuhamia hapa Dodoma. (Makofi)