Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, naomba nianze mchango wangu kwenye Wizara hii kwa kuangalia upya Sheria ya Kodi hasa kodi ya wafanyabiashara wadogo. Utaratibu wa kuanza kulipa kodi kabla ya kuanza biashara ni utaratibu usiofaa, kwani mlipa kodi utatakiwa kulipia kodi sehemu ya mapato yake. Sasa kitendo cha kulipa kodi kabla ya kufanya biashara, je, hiyo kodi anaitoa wapi? Iwapo biashara husika ikimpa hasara mfanyabiashara, je, sheria hii haioni kuwa inamuonea huyu mfanyabiashara? Jambo hili limekuwa likilalamikiwa na wananchi wengi sana na wengine kushindwa kuingia kwenye sekta hii ya biashara.

Mheshimiwa Spika, suala la ongezeko la mshahara halipaswi kuachwa bila kuangaliwa upya kwani hali ya wafanyakazi nchini ni mbaya sana, gharama za maisha zinapanda kila siku kukicha, sawa na kushuka kwa shilingi yetu dhidi ya dola. Kuacha kuongeza mishahara ya wafanyakazi kunapunguza sana ari ya wafanyakazi hasa sekta ya afya na sekta ya elimu, kwani hivi sasa wafanyakazi wa sekta hizi wana migomo ya kimoyomoyo. Walio wengi kinachowabakiza kazini ni uhaba tu wa ajira nchini.

Mheshimiwa Spika, kuna malalamiko ya muda mrefu juu ya wafanyakzi wa iliyokuwa NMC na TTCL. Wafanyakazi wa iliyokuwa NMC bado wana kesi mahakamani, lakini Hazina wamekuwa wakipiga chenga kwenda mahakamani, hivyo kuchelewesha haki za watu hao.

Vilevile kuna wafanyakazi wa TTCL, hawa walilipwa kwa makundi. Kuna waliolipwa kwa mkupuo kisha wakarudishwa kwenye pensheni ya kila mwezi na kuna kundi lililolipwa kwa mkupuo lakini hadi leo hawajarudishwa kwenye pensheni ya mwezi. Kitendo hiki ni cha kibaguzi kwa wastaafu hao, nao wanashinda Hazina bila majibu.

Mheshimiwa Spika, lingine ni fedha za mifuko maalum kutumiwa nje ya makusudio ya fedha hizo. Kumekuwa na matumizi yasiyofaa kwenye awamu hii ya tano. Mfano, haiingii akilini miradi ya REA kukwama kwa kukosa fedha wakati vyanzo vya fedha hizi vinajulikana na vinalipa vizuri, lakini wakandarasi wa miradi ya REA nchi nzima wanadai. Mfano mwingine ni fedha za kuendeleza zao la korosho. Pamoja na makusanyo mazuri ya export levy, fedha hizo zimeshindwa kwenda kwenye Bodi ya Korosho. Kutumika hovyo kwa fedha hizi kunaondoa maana ya kuanzishwa kwa mifuko hii.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na utaratibu wa taasisi ya TBS na TFDA kukagua na hatimaye kuteketeza bidhaa fake au zisizoruhusiwa nchini. Jambo hili ni jema, lakini ni kwa nini uteketezaji huu usifanywe kwenye viwanda au kwa waagizaji wakubwa badala ya kwenye maduka ya rejareja? Bidhaa kwa mfano ukienda Kariakoo kwenye maduka ya jumla, zinauzwa bila kificho, lakini ukinunua na kuweka dukani kwako ndipo TBS au TFDA wanakuja kukagua na kusema ni bidhaa fake na kesho yake ukienda Kariakoo bado utazikuta zikiuzwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu taarifa ya TRA na Hazina kukosa uhalisia kwenye maisha ya kawaida ya wananchi wetu, Hazina wanasema umaskini wa watu wetu unapungua wakati hali ya watu wetu inazidi kuwa mbaya. Hali ya lishe ni mbaya, watu wanashindwa kununua mahitaji muhimu. Uwezo wa watu kununua bidhaa umepungua sana kadri ya TRA wanavyotangaza kukusanya mapato zaidi ndiyo hali ya watu inavyozidi kuwa mbaya zaidi na hata fedha za kwenda kwenye miradi ya maendeleo zinashindwa kwenda. Hivyo nini faida ya kuwa na makusanyo mazuri wakati miradi yetu ya maendeleo inakwama siku hadi siku? Wizara zote hazipelekewi fedha za miradi ya maendeleo. Je, takwimu za TRA tuziamini? Kama ndivyo, basi kutakuwa na matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi.

Mheshimiwa Spika, mgawanyo wa fedha za maendeleo nao ni bora ukaangaliwa upya kwani kwenye mikoa au maeneo yenye michango mikubwa kwenye pato la Taifa hakujapewa kipaumbele katika kuimarisha miundombinu ili kuongeza uzalishaji. Mfano, Mikoa ya Lindi na Mtwara bado hali ya miundombinu siyo nzuri. Mfano, Bandari ya Mtwara, Bandari ya Lindi na Kilwa, Barabara ya Nangurukulu – Liwale na kadhalika. Kuacha kuboresha miundombinu ya barabara hizo nilizozitaja hapo juu ni kudumaza uchumi wa maeneo husika na nchi kwa ujumla.