Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Kumi na Moja wa Bunge

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Kumi na Moja wa Bunge

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi kuweza kuchangia taarifa hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa the Interpretation of Laws Act, Cap. 1, imeweka masharti maalum ambayo yanalipa Bunge mamlaka ya kuweza kuzisimamia au kufanya udhibiti wa Sheria Ndogo ambazo zinatungwa na Serikali pamoja na taasisi zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge linafanya udhibiti huo baada ya sheria zile ndogo kuwa zimetungwa na Serikali na zimetangazwa katika Gazeti la Serikali, lakini pia zimewasilishwa Bungeni. Katika uchambuzi wa sheria ndogo vitu ambavyo tunajiridhisha ni kwamba, kama sheria ndogo hizo zilizotungwa zinaendana na zinakidhi matakwa na masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pia zinakidhi matakwa na masharti ya sheria mama na sheria nyingine za nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sheria ndogo ya The Mining Local Content Regulation katika kanuni ya 3, kanuni hii inaonekana kwamba ni ultra vires kwa maana ya kwamba, inakwenda kinyume na masharti ya sheria mama, kivipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, ukiangalia kanuni hii yenyewe inatoa tafsiri ya neno kampuni zawa ambayo katika tafsiri yake imeweka kwamba, kampuni zawa itakuwa ni ile kampuni ambayo katika share holders wake au wanahisa 51% ya wenye hisa wawe ni Watanzania. Si hivyo tu, pia 80% katika utendaji wa juu wa kampuni hiyo pia, wawe ni Watanzania. Sasa ukiangalia Sheria ya Makampuni ambayo ndio sheria mahususi kwa masuala ya makampuni kwa Tanzania hii, haijatoa tafsiri hiyo, ambayo imetolewa katika kanuni hii kwa hiyo, maana yake nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kunakuwa na mkanganyiko wa tafsiri na utaratibu wa kutunga kanuni au kutunga sheria ndogo ni lazima sheria mama zizingatiwe. Pale kunapokuwa na mkanganyiko kati ya sheria mama pamoja na kanuni hiyo inaleta changamoto na ninaomba sana marekebisho yaweze kufanywa ili kuondoa mkanganyiko huo kwa sababu ukiangalia kwenye Sheria ya Makampuni yenyewe inatafsiri kampuni zawa ni kampuni ile ambayo imesajiliwa chini ya BRELA. Kwa hiyo matakwa ya shareholding structure hayajawekwa kwenye Sheria ya Makampuni.

Kwa hiyo, ni vizuri Sheria ya Makampuni ifanyiwe mabadiliko ili kuweza kuendana na matakwa ya mabadiliko na kuzuia mkanganyiko wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda pia kwenye The Urban Planning (Appeals), Regulations, 2018 ambayo imetungwa chini ya Sheria ya The Urban Planning Act, Sura ya 355, utaona kwamba kanuni hii imeweka sharti kwamba mahakama mara baada ya kutoa uamuzi, kuwasilisha nakala tatu za hukumu kwa Mamlaka ya Mipango Miji zinazoainisha sababu ya kufikia maamuzi yake. Sasa ukiangalia kanuni hii, utaona kwamba utaratibu uliowekwa na kanuni hii si sawa, kwa nini, kwa sababu hamna chombo au taasisi yoyote ya Serikali…

T A A R I F A . . .

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru kwa taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mahakama ni mhimili unaojitegemea na unaoendeshwa chini ya Ibara 107(b) lakini unapoona kwamba kuna kanuni ambayo inatoa sharti ya kuamuru Mahakama tofauti na utaratibu basi hii kanuni inakuwa ni batili na inakinzana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana gani kwamba Mahakama haiwezi kuamuriwa na Serikali au chombo chochote cha Serikali, bali mahakama inaamuriwa na mahakama iliyo juu yake, si tofauti na hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hii kanuni ambayo inayotoa masharti kwa Mahakama kuleta maelezo na kuleta nakala tatu za hukumu kwa Mipango Miji na kuainisha sababu ya kufikia maamuzi yake ina changamoto na sio sahihi na kuna haja ya kufanya marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, ukiangalia kwenye hii The Urban Planning (Appeals), Regulations, 2018 kanuni ya 4(b) kanuni ya ndogo ya pili na ya tatu utaona kwamba inaweka sharti kwa mtu anayekata rufaa dhidi ya maamuzi ya Mamlaka ya Mipango Miji kutoa nyaraka zote pamoja na zile ambazo hakuwa amezitoa katika usikilizaji wa shauri la awali dhidi ya mamlaka hiyo kuzipeleka kwa Mamlaka ya Mipango Miji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika utaratibu mtu anayetoa rufaa hatakiwi wala hapaswi kisheria kupeleka nyaraka zozote kwa yule mrufaniwa, tofauti na hapo inabidi tu asubiri mashtaka yaanze na atakabidhi nyaraka kwa Mahakama na si kumpelekea yule ambaye yeye anaenda kukata rufaa dhidi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sio hivyo tu hata katika ngazi ya rufaa, rufaa haichukui ushahidi mpya, rufaa inafanya uamuzi kutokana na nyaraka zilizokuwepo kuanzia mwanzo katika mashtaka, lakini kusema kwamba kuletwe nyaraka mpya si utarabu sawa na ni kinyume na tofauti na kanuni hizi zinavyoelekeza. Kwa hiyo, kuna haja ya kufanya marekebisho ili kuendana na sheria zilizowekwa ambazo zinaongoza utaratibu wa kimahakama wa kukata rufaa na wa kimashtaka kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kujielekeza kwenye baadhi ya hizi sheria ndogo, naomba sasa kuishauri Serikali kwamba wakati wa utungaji wa sheria ndogo kwanza wawashirikishe wadau mbalimbali ili hizi sheria ndogo zinapokuja kutungwa kusiwe kuna changamoto wakati wa utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, Serikali pia iongeze rasilimali watu katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali hasa katika vitengo vinavyojihusisha na kupitia sheria ndogo hizi ili kuondoa zile dosari ambazo zinaonekana ambazo hatimaye zinaleta changamoto katika utekelezaji wa sheria husika. Pia wakati wa utunzi wa sheria ndogo mamlaka au Serikali pia ihakikishe kwamba uchambuzi na utunzi wa zile Sheria Ndogo unazingatia misingi ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sheria ndogo na sheria zingine za nchi ili sheria ndogo tunazozitunga zisije zikaleta conflict of Laws na sheria ziwe zinaweza kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante sana.