Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Nishati

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Nishati

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitoe shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri anayehudumu kwenye Wizara hii, kwa kuiweka Mikoa ya Lindi na Mtwara kwenye Gridi ya Taifa. Tunashukuru sana kwa jambo hili kwa sababu mara nyingi sisi watu wa Kusini tulikuwa tunalalamika mara nyingi mnatusahau sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile na suala la kupeleka meli ya mafuta katika Bandari ya Mtwara na Lindi, tunashukuru mmefanya jambo zuri sana. Hata hivyo, mradi huu nina wasiwasi nao kwa sababu Mikoa mingi ambayo imepitiwa na hii Gridi ya Taifa nimeona nguzo kubwa za chuma ipo lakini kuanzia Mbagala mpaka Mtwara sijaona nguzo ya chuma. Isije tukapigwa changa la macho kwa hizi nguzo za magogo, kama ndiyo hivyo basi tutashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nataka niongelee REA. REA awamu ya I na II haijafanya vizuri katika nchi hii, kwa sababu sehemu nyingi za taasisi za umma umeme huu haukuzingatiwa lakini kwenye hii awamu ya III naona imezingatiwa. Je, zile sehemu ambazo zilipitiwa na awamu ya I na II kuna utaratibu gani sasa wa kufikisha umeme kwenye hizi taasisi za umma? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya III ya REA nayo ina ukakasi wake. Mkoa mzima wa Lindi tumepata mkandarasi mmoja. Mpaka leo mkandarasi wa REA Mkoa wa Lindi bado yuko Ruangwa hajui Liwale ataenda lini, hajui Nachingwea ataenda lini na awamu ya III sehemu ya kwanza mnasema inakamilika mwezi Juni mwakani, lakini hatuelewi awamu hii ya kwanza huyu mkandarasi atafikia wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile walituambia kwamba maeneo ambayo yako mbali na vyanzo vya umeme yatapatiwa na umeme jua. Katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Liwale kuna vijiji ambavyo viko umbali mfupi, kutoka Halmashauri ya Wilaya ni kama kilomita 70 au kilomita 50 kutoka kwenye vyanzo vya umeme,Vijiji kama vya Ndapata, Mpigamiti, Kimambi, Mdunyungu, Milui, Kikuyungu, Lilombe, Mlombwe, Ngongowele, Kipelele, Naujombo, najua kwamba hakuna uwezekano wa kujenga nguzo za umeme kutoka Liwale mjini mpaka kufikia vijiji hivi, naomba nipate ufafanuzi umeme jua katika vijiji hivi utakuja lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachogomba hapa mambo ya Stiegler’s Gorge hii ni kwa sababu ya falsafa moja kwamba ukiwa muongo lazima usiwe msahaulifu. Serikali hii mlishatuaminisha kwamba gesi ya Mtwara ndiyo muarobaini wa umeme nchi hii, matokeo yake haikuwa hivyo, ndiyo maana watu wanavyoingia kwenye Stigler’s Gorge pamoja na madhara yote haya ambayo tunaenda kuyapata, je, haitakuwa sawa na yale yaliyokuwa kwenye gesi? Maana tuliambiwa kwamba gesi itashusha bei ya umeme, bei ya umeme bado iko juu. Tuliambiwa gesi itakuwa mwarubani wa umeme nchi hii na kuuza nchi za nje, lakini mpaka leo pesa nyingi zimepotea, hatujui hatima ya mradi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana sasa tunapoingia kwenye Stiegler’s Gorge ambako tunajua madhara ni makubwa, kwa madhara haya kama kweli hili jambo lililokusudiwa litakwenda kufanyika tunaweza tukavumili haya madhara, lakini kwa kuona matatizo yale yaliyojitokeza kwenye mradi wa gesi ndiyo maana leo hii wananchi wengi na Wabunge wengi wanalilalamikia suala hili. Wanakuwa waoga kwa sababu tusije tukatumbukia kwenye tope kama tulivyotumbukia kwenye gesi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la gharama za umeme nchini. Suala hili Mheshimiwa Waziri inabidi alitupie macho sana kwa sababu linatugharimu kwa kiwango kikubwa sana. Ndiyo maana hata viwanda vyetu vinazalisha bidhaa ambazo zinashindwa kuingia kwenye soko la Kimataifa kwa sababu gharama ya uzalishaji nchini ni kubwa. Leo hii mtu aki-import sukari kutoka nje ya nchi inauzwa rahisi kuliko ya ndani ya nchi. Kwa hiyo, suala la gharama ya umeme linatakiwa liangaliwe kwa makini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.