Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Maida Hamad Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais na Baraza la Mawaziri. Sekta ya Kilimo inayojumuisha uzalishaji wa mazao ya Kilimo, Mifugo, Uvuvi na mazao ya misitu ndiyo tegemeo la maisha ya Watanzania walio wengi.
Hata hivyo, ukuaji wa sekta hii siyo wa kuridhisha sana kutokana na matumizi ya teknolojia isiyoendana na wakati na pia tunategemea majaliwa ya Mwenyezi Mungu katika hali ya hewa. Hata hivyo, tunashukuru hali ya hewa haijawa mbaya sana, kwa zaidi ya miaka kumi tunapata mvua za kutosha na chakula kinapatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu kwa kipindi hiki imedhamiria kuwekeza zaidi katika uchumi huu wa viwanda, uchumi wa viwanda utategemea sana kilimo chetu kwa namna tutakavyojipanga vizuri na mikakati endelevu ya kilimo kwa mazao yetu yenye ubora unaostahili. Kwa kipindi kirefu Mkoani Lindi tumekuwa na mbegu za mazao ya mahindi, muhogo, mpunga, korosho, ufuta, zisizo na ubora. Wakulima wetu wanajitahidi sana kulima mazao haya lakini mavuno yake hayaleti tija kutokana na mbegu isiyo bora lakini na namna ya kilimo cha jembe la mkono.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji sasa Serikali ya Awamu ya Tano kuleta mapinduzi ya kilimo na kuondokana na kilimo cha jembe la mkono, kuwa na mbegu bora na kuwa na kilimo endelevu kwa kutumia pia skimu zetu na mabanio. Tunahitaji Maafisa wa Kilimo watusaidie kutoa elimu ya kilimo bora cha kisasa cha mazao ya biashara, kilimo ni biashara lazima sasa tuondoke tulipo tusonge mbele.
Wakulima wetu wanahitaji kupewa elimu, kupata mbegu bora na pembejeo za kilimo kwa wakati, Serikali ni vema ikajipanga kujua mahitaji ili vijana wetu na wanawake waweze kupata ajira na kuweza kukuza vipato vyao kupitia kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Lindi Manispaa tunalo banio limejengwa kwa pesa nyingi sana lakini bado halijawanufaisha wakazi wa Kata ya Ng‟ape, sasa lina zaidi ya miaka mitatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu korosho; korosho ndiyo zao la biashara katika Mkoa wa Lindi, kumekuwa na tatizo kubwa la upatikanaji wa fedha wakati wa mauzo ya korosho, Vyama vya Ushirika vinawakandamiza sana wakulima hata kama bei elekezi inatolewa. Tunaiomba sana Serikali kutusaidia kusimamia Vyama vya Ushirika, wakulima wetu wamekuwa maskini kwa kipindi kirefu na hawana msaada wowote.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yangu ina dhamira njema ya mfumo wa stakabadhi ghalani, lakini kwa namna unavyoendeshwa wakulima wanapata kero ya kutopata fedha zao kwa wakati na wapo watu wanatajirika kwa mfumo huu hasa wanaoendesha Vyama vya Ushirika na wakulima wanaendelea kuwa maskini na kukatishwa tamaa na Serikali yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Sekta ya Uvuvi; Mkoa wa Lindi wakazi walio wengi ni wavuvi, maeneo ya Kilwa, Lindi Vijijini na Lindi Manispaa uvuvi uliopo hauna tija. Changamoto kubwa ni pamoja na:-
(i) Kutokuwa na zana bora za uvuvi;
(ii) Kutokuwa na elimu ya uvuvi;
(iii) Kutokuwa na boti zenye engine wakaweza kwenda masafa marefu kwa ajili ya kuvua; na
(iv) Masoko ya uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri ni kwamba, tunaiomba Serikali kutusaidia Mkoa wa Lindi, vijana wetu wakaandaliwa katika vikundi na wakawezeshwa kufanya shughuli za uvuvi ili kuleta ajira kwa vijana na kuleta ustawi wa wananchi wa Lindi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa kazi nzuri anazofanya na naunga mkono hoja.