Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nipende tu kusema kwamba naunga mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri kwa asilimia mia moja. Kipekee tu napenda kumpongeza sana yeye Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa Hotuba nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la kwanza, kama msimamizi wa Sekta ya Madini nipende tu kutoa shukrani sana kwa Serikali kupitia kwake Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa kukubali kuweza kufuta tozo zilizokuwa zikitozwa katika chumvi, tozo takribani 10 kati ya 16 ambazo kimsingi zilikuwa zimesababisha sana gharama za uzalishaji wa chumvi kuwa kubwa na pia kumsababishia mchimbaji wetu mdogo wa chumvi kutokuweza kupata faida.

Mheshimiwa Spika, ilikuwa kwa takribani gunia la kilo 50 walikuwa wanapata faida ya Sh.150 tu ilikuwa ni faida ndogo. Pia walikuwa wanashindwa kushindana kisoko na matokeo yake ilikuwa chumvi ya kutoka nchi za jirani ilikuwa inaingia kwa wingi zaidi na hatimaye sisi ambao tuna chumvi nyingi humu kutoweza kufanya biashara au kuwa na ushindani. Kwa hiyo nipende tu kusema kwa niaba ya Sekta ya Madini na Wizara tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya Mheshimiwa Musukuma kuhusiana na tozo au kiwango kikubwa cha kodi kinachotozwa katika madini ya dhahabu au kwa wachimbaji wetu wadogo wa dhahabu na alikuwa ameeleza kwamba kuna tozo ya asilimia takribani kumi na nne (14%).

Mheshimiwa Spika, nipende tu kumweleza Mheshimiwa Musukuma kwamba kwa mujibu wa Sheria yetu ya Madini Sura namba 123, wachimbaji wadogo wanatozwa takribani asilimia 12.3 ya kodi ambayo inajumuisha mrabaha wa asilimia sita, inajumuisha kodi ya zuio ya asilimia tano, ada ya ukaguzi wa uzalishaji wa madini asilimia moja, pamoja na ushuru wa huduma au service levy kwa halmashauri kwa asilimia 0.3 ambayo jumla yake ni asilimia 12.3 na kwa upande wa wachimbaji wakubwa na wa kati wao wanatozwa mkokotoo wa asilimia 37.3.

Mheshimiwa Spika, alipendekeza kodi kwa wachimbaji wadogo ziondolewe; nipende tu kumweleza Mheshimiwa Mbunge kwamba tumekuwa tukiliona na kwa kuwa Serikali yetu ni sikivu kama ambavyo tumefanya katika chumvi. Niendelee tu kuwaomba shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo (FEMATA) tukae, tuweze kulizungumza suala hili na kuliona ni kodi zipi au ni tozo zipi ambazo zinaweza zikafikiriwa kuzingatiwa katika punguzo hilo au kuweza kuondolewa.

Mheshimiwa Spika, lengo letu kubwa kama Serikali nikuhakikisha kwamba tunakuwa na uchimbaji mdogo, uchimbaji mdogo ambao utakuwa na faida kwa wachimbaji wetu. Lakini pia sisi kama Serikali bado tunaendelea kuona ni namna gani tunawasaidia kwa upande wa teknolojia,
masuala mazima ya mtaji, mafunzo, kupata masoko lakini zaidi kuwapa teknolojia mpya na waweze pia kujifunza teknolojia ya kisasa katika uchimbaji.

Mheshimiwa Spika, kwa kuanzia kupitia Serikali kupitia bajeti yetu ya Wizara ya Madini katika mwaka ujao wa fedha tutajenga vituo vya mifano vitano katika maeneo ya Chunya, Bukombe, Rwamgasa, Tanga pamoja na Kilwa. Pia tutajenga vituo saba vya umahiri Mpanda, Handeni, Musoma, Songea, Bariadi, Bukoba na kwingineko.

Mheshimiwa Spika, lengo letu kubwa ni kuhakikisha kwamba tunawafundisha kwa mfano ili waweze kuchimba kwa teknolojia ya kisasa kupitia vituo hivyo ambavyo tumeviweka kwa gharama nafuu sana, lakini hatimaye lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunawarasimisha ili waweze kuingia katika mfumo rasmi wa kibiashara pamoja na kikodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho nipende tu kuoa rai kwa Mamlaka zetu za Serikali za Mitaa, kuhakikisha kwamba wanazingatia viwango vya tozo za kodi vilivyoanishwa katika Sheria. Wako wengine unakuta wameenda katika maduara ya uchimbaji wa Madini, unakuta wanaambiwa wakivuna mifuko 10, mifuko labda mitano inaenda kwenye Halmashauri. Niombe sana tuzingatie viwango ambavyo vimeainishwa kisheria ili kuhakikisha kwamba wachimbaji wetu hawa wadogo hatimaye wanaweza kukua.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo Sera yetu ya Wizara ya Madini na Serikali kwa ujumla wachimbaji hawa hadhi yao hii si ya kudumu wanatakiwa tu watumie hadhi ya uchimbaji mdogo kama daraja hatimaye waweze kuwa wachimbaji wa kati na hatimaye pia kuwa wachimbaji wakubwa kama ambavyo wengine kama wakina Busolwa Mining pamoja na akina Mzee wangu Marwa wameweza kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja pia ya zuio la usafirishaji wa carbon, hoja hii nadhani leo nitakuwa nasimama kwa mara ya tatu kuweza kuielezea. Kaka yangu Mheshimiwa Musukuma ameweza kuieleza lakini nipende tu kurudia maelezo ya Serikali kwamba zuio letu la usafirishaji wa carbon liko palepale kama nilivyotoa maelezo yangu tarehe Mosi Juni, kama nilivyotoa maelezo yangu pia tarehe 14 Juni.

Mheshimiwa Spika, nipende tu kwa kweli kuwapongeza sana wamiliki wa Illusion Plants takribani watano kwa Kahama tayari wameshaanza kujenga Illusion Plants hizo. Nipende pia kuwapongeza wawekezaji takribani watatu ambao wameshaanza kuonesha nia ya kuwekeza Shinyanga, vile vile pia niwapongeze sana wawekezaji wengine watatu ambao wameonesha nia ya kuwekeza katika maeneo ya Tabora.

Mheshimiwa Spika, zaidi niwapongeze sana Kampuni ya GEMAAfrica ambao tayari wameshakamilisha kujenga mtambo wa Illusion Plants Wilaya ya Geita. Nipende kuwapongeza Kampuni ya Transco Gold pamoja na Nyamigogo, Nang’ana Group pamoja na Busamu Company ambao nao wameshakamilisha ujenzi wa Illusion Plants katika Wilaya ya Kahama.

Mheshimiwa Spika, kipekee pia niwapongeze Framal Investment ambao tayari nao wameshakamilisha ujenzi wa mitambo yao katika Wilaya ya Musoma pamoja na Deep Mine Service ambayo kwa sasa na wenyewe wanatafuta eneo la kujenga mitambo husika ya Illusion Plants katika Wilaya ya Kahama.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Geita na Tarime bado watu wengi wamekuwa wakionesha nia. Nipende tu kuwakaribisha sana wawekezaji na Watanzania wengine kuona ni namna gani wanatumia fursa hii kuwekeza katika ujenzi wa Illusion Plants katika sehemu ambazo bado wawekezaji hawajenda lakini pia huduma zao zinahitajika. Hata hivyo, nipende kusema kwamba agizo la Serikali bado linasimama palepale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja kuhusiana na Mheshimiwa Ole Millya alieleza kwa kina sana kwamba mapendekezo ya Kamati Maalum ya Mheshimiwa Spika iliyochunguza mnyororo mzima wa biashara ya uchimbaji wa Tanzanite kwamba hayajatekelezwa. Nipende tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu hata siku moja hatuwezi kudharau mapendekezo au maazimio ya Kamati Maalum ya Spika ambayo tunaamini ni mapendekezo ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, vilevile nipende tu kueleza tu kwamba kama ambavyo tulieleza tarehe Mosi, Juni, 2018 katika hotuba yangu ukurasa wa 46, tulieleza namna kabisa masuala mazima ya majadiliano kupitia ubia wa Kampuni ya Tanzanite One pamoja na STAMICO yanavyoendelea na tulieleza katika hotuba yangu ukurasa wa 46 kwa wale ambao watakuwa nayo wanaweza kufuatilia.

Mheshimiwa Spika, tumeotoa maelekezo kwa Kampuni ya Tanzanite One pamoja na STAMICO kurudisha leseni ya uchimbaji ili iweze kuandaliwa utaratibu mpya ambao utaiwezesha Serikali na Taifa kwa ujumla kuweza kunufaika zaidi katika uchimbaji na biashara nzima ya Tanzanite kwa kuzingatia Sheria ya Madini, Sura namba 123.

Mheshimiwa Spika, hayo mengine ya kusema yamegawia, sijui imekuwaje mara imehuishwa, nipende tu kusema kwamba niwaombe Waheshimiwa Wabunge wajikite zaidi katika maelezo ya Mheshimiwa Kabudi aliyoyatoa tarehe Mosi, Juni lakini pia wajikite katika kufanya reference katika hotuba yangu niliyoitoa ya bajeti katika ukurasa ule wa 46. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nipende tu kusema kwamba katika makubaliano yale ambayo Kamati ya Majadiliano ya Taifa kupitia kwa Kiongozi Mheshimiwa Kabudi, makubaliano yaliyoingiwa tarehe 15 Aprili na Kampuni ya Tanzanite One tayari wameshaanza kulipa mkupuo wa kwanza wa fidia ambayo walikuwa wameelekezwa na obviously fidia hii inaingia kwa Taifa na kuna taratibu zake kwa mujibu wa Wizara ya Fedha kwa malipo kama hayo yanalipwa kwa taratibu gani.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru na napenda kusema tu kwamba, naunga mkono hoja.