Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza katika siku ya leo. Napenda kuanza kwa kutoa pongezi za dhati kwa Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Mpango, pamoja na Naibu Waziri, Mheshimiwa Kijaji pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Fedha na Mipango wakiongozwa na Katibu Mkuu Dkt James Doto.

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa nimpongeze kaka yangu Dkt. Philip Mpango, kwa uwasilishaji wa umahiri kabisa wa bajeti hii, alitumia saa moja na dakika arobaini na tano lakini hatukuchoka. Tunampongeza sana na naunga mkono hoja hii kwa sababu bajeti hii imeandaliwa kwa lengo la kutatua kero za Watanzania.

Mheshimiwa Spika, katika mchango wangu nitapenda kuzungumzia masuala machache kwa sababu ya muda na ningeanza na suala ambalo wachangiaji wengi walikuwa wakilizungumzia kwamba Serikali haipeleki fedha kwamba tunakuwa tunapitisha hapa bajeti lakini mwisho wa siku Serikali haipeleki fedha. Pia wengine walienda mbali na wakawa wanasema kwamba hii Serikali inaleta bajeti hewa.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze kwa dhati Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Joseph Pombe Magufuli ambaye kwa kweli ni Raisi shupavu, ni Rais ambaye anafanya vitu kwa vitendo, akiahidi anatekeleza.

Mheshimiwa Spika, pongezi hizi nazitoa kwa sababu kwenye sekta ya elimu fedha zimekuwa zikija kama ambavyo zimepangwa. Wizara ya Elimu ilipangiwa jumla ya trilioni moja na bilioni mia tatu thelathini na sita na mpaka sasa Serikali imeshatoa trilioni moja na bilioni mia moja ishirini na tisa.

Mheshimiwa Spika, Serikali pia imekuwa ikitekeleza ahadi yake ya elimu bila malipo kila mwezi bila kukosa, fedha kwa ajili ya elimu bila malipo zimekuwa zikienda bilioni ishirini kwa wakati. Pia Serikali ilikuwa imetenga bilioni 427.54 kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu na mpaka sasa ninapozungumza tayari Serikali imekwisha pokea shilingi bilioni 427.44 sawa na asilimia mia moja ya fedha zote ambazo zilitengwa.

Mheshimiwa Spika, kutokana na upatikanaji huu wa fedha katika sekta ya elimu Serikali imeweza kufanya mambo mengi. Tumeweza kujenga madarasa kwa ajili ya kuongeza upatikanaji wa nafasi za elimu pamoja na kuboresha mazingira ya elimu ambapo jumla ya madarasa 1907 yamejengwa lakini na matundu ya vyoo elfu nne mia tano na moja.

Mheshimiwa Spika, na nichukue nafsi hii kuwapongeza kwa dhati, umoja wa Wanawake Wabunge kwa uchangishaji wa vyoo bora kwa mtoto wa kike ambao kwa kweli inaungana na juhudi za Serikali katika utoaji wa elimu bora tunashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, pia tumeweza kujenga mabweni 338, tumefanya ukarabati wa shule kongwe 45 na vilevile ukarabati wa vyoo vya walimu 17. Vile vile kutokana na upatikanaji wa fedha hizi Serikali imeweza kuendelea kuimarisha tafiti katika nchi hii. Serikali ilitoa shilingi bilioni 3.2 kwa ajili ya miradi nane ya tafiti na hii miradi imelenga katika kuimarisha viwanda pamoja na kilimo.

Mheshimiwa Spika, jana tulikuwa tunazungumzia masuala ya kilimo, tunajua kwamba kilimo ndio kinabeba Watanzania na kwa hiyo Serikali imetoa bilioni 3.2 ambazo ni kwa ajili ya miradi minane ya utafiti. Kwa mfano na taasisi inayoshughulika na magonjwa ya binadam, (NIMR) imepata fedha kwa ajili ya kutengeneza maabara kwa ajili ya dawa, pia Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS) kimepata fedha pia kwa ajili ya masuala ya dawa.

Mheshimiwa Spika, hatujasahau na hapa Mkoa wa Dodoma Makao Makuu tumetoa fedha kwa ajili ya kuimarisha utafiti wa zao la zabibu. Kwa hiyo tumetoa fedha kwenye hii Taasisi ya Utafiti wa Mifugo ya TALIRI kwa ajili ya kuzalisha mifugo.

Mheshimiwa Spika, vile vile tumetoa fedha kwa ajlili ya utafiti wa kuboresha mitambo ya kuzalisha mvinyo katika Taasisi ya Utafiti wa Kilimo ya Makutupora. Haya yote nayazungumza kwa uchache tu kuonesha kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ambayo inatenda kwa vitendo na hii yote imetokana na bajeti ambayo imetengwa.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kwenye Taasisi za Elimu ya Juu, Serikali hii imefanya mambo makubwa sana kwenye hizi Taasisi za Elimu ya Juu. Ukienda Chuo Kikuu cha Dar es Salaam sasa hivi inajengwa maktaba ya kisasa na ya kipekee katika Bara la Afrika, ambayo itakuwa na uwezo wa kuweka wanafunzi 2,500 kwa wakati.

Mheshimiwa Spika,ile vile Tume ya Mionzi ya Taifa inajenga Maabara kwa ajili ya kupima mionzi na maabara hiyo ikikamilika kwa kweli itakuwa ni maabara ya kipekee katika Ukanda wa Afrika. Tayari vifaa kwa ajili ya maabara hizo vimekamilika. Nashukuru kwamba Serikali imeshatoa fedha ambazo zilikuwa zimetengwa kwa ajili ya hii Tume na zinaendelea kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, katika suala la kusema kwamba Serikali inatenga fedha haizitoi; kwa sababu ya muda siwezi kumaliza taasisi, lakini niseme kwamba ukienda Mzumbe, ukienda Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine, ukienda Mbeya Chuo cha Utafiti, ukienda Arusha Technical utakuta mambo mengi yanafanyika.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo lilikuwa linazungumziwa katika michango ni namna gani Serikali inaimarisha elimu ya ufundi. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kama ambavyo imeainishwa katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano na ambao umekuwa
ukitekelezwa mwaka hadi mwaka, Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuhakikisha kwamba inaongeza ujuzi kwa wananchi katika nyanja mbalimbali, maana kuna ujuzi wa chini, kuna ujuzi wa kati na ujuzi wa juu.

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyoongea katika Chuo cha Ufundi Arusha Karakana zote zinabadilishiwa vifaa ili ziweze kutoa mafunzo ya kisasa. Kuna kontena kumi na sita ambazo zimefungwa, tayari vifaa vile vipo kwa ajili ya kufungwa, kwa hiyo Serikali inaendelea kuimarisha.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la Walimu, kwa sababu elimu si majengo tu, ni pamoja na Walimu. Serikali imekuwa ikiendelea kuimarisha utoaji wa mafunzo ya ualimu. Sasa hivi tunafanya upanuzi wa vyuo vyetu vya ualimu; ukienda kule Kitangali utakuta Chuo cha Ualimu cha kisasa kimejengwa, nenda Mkuguso, nenda Ndala, nenda Shinyanga utaona kazi nzuri ambayo inafanywa na Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Spika, Serikali hii ambayo Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli ni Rais ambaye anaangalia wanyonge hajasahau wanafunzi wenye mahitaji wenye mahitaji maalum. Kwa hiyo katika mambo ambayo tunafanya tumeendelea pia kuimarisha utoaji wa elimu kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maaalum.

Mheshimiwa Spika, hivi ninavyozungumza ujenzi wa shule maalum kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum inaendelea katika Chuo cha Ualimu Patandi. Sambamba na ujenzi huo lakini Serikali pia imepanga kununua vifaa kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum; na tayari tumeshatoa maelekezo kwamba katika shule zote katika miundombinu yote ya kielimu inayojengwa lazima tuzingatie mahitaji kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niseme tu kwamba niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuiunge mkono bajeti ya Serikali kwa sababu ni bajeti ambayo italeta maendeleo, ni bajeti ambayo inakwenda kutatua kero za wananchi na ni bajeti ambayo inatusaidia hata sisi
Waheshimiwa Wabunge kutekeleza ahadi ambazo tumezitoa kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nategemea kwamba jioni kama ulivyoelekeza Wabunge wote watajitokeza wapige Kura ya Ndiyo katika bajeti hii ili wanafunzi wa elimu ya juu waendelee kupata mikopo ambapo tunategemea kutoa mikopo kwa wanafunzi 123,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naunga mkono hoja, lakini kwa heshima kubwa nawaomba Waheshimiwa Wabunge wote tupige Kura ya ndio. Ahsante sana.