Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, na mimi nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ili niweze kuhitimisha hoja yangu kwa kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja za Wabunge zipo nyingi, zipo ambazo nitafanikiwa kuzieleza hapa na zipo nyingine ambazo utaturuhusu tuzilete kwa maandishi ili Wabunge wetu waweze kupata hoja mbalimbali walizoziuliza na ziweze kusaidia katika kusukuma hatua hii ya shughuli nzima ya sekta yetu ambayo ni ya mifugo na uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikianza moja kwa moja na eneo ambalo limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge zaidi ya nane ambao wapo hapa ilikuwa ni eneo la malisho ya mifugo ambalo wameliongea kwa hisia kubwa. Wewe mwenyewe najua ni mfugaji pia umeliongea kwa hisia kubwa sana. Pia imezungumzwa kuna migogoro mingi ya wakulima na wafugaji ambayo nayo imo mle, kuna migogoro kati ya wakulima na watumiaji wengine wa ardhi, lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu aliwahi pia kuunda Tume ya watalaam ya kufuatilia suala la migogoro hii kati ya wakulima, wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu kuwa katika mwaka 2017/2018 Wizara kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Tume ya Taifa ya Matumizi ya Ardhi imetenga jumla ya hekta 10,378.53 kwa ajili ya maeneo ya ufugaji kwenye vijiji 13 katika Wilaya za Makete, Kilolo, Tanganyika, Mpanda na Kalambo. Hadi sasa hekta milioni 2.545 katika vijiji 741 zimetengwa kwa ajili ya malisho.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu katika kuangalia hili suala la malisho ya wafugaji imefanya mambo yafuatayo; moja, katika ranchi zote za taifa (ranchi mama) hekta 2,000 zimetengwa kwa ajili ya wafugaji hasa wakati wa ukame na zitasimamiwa na NARCO yenyewe lakini unapofika muda wa ukame, wafugaji waliopo kwenye maeneo hayo watakuwa wanalishia mifugo yao, haya ni mageuzi makubwa hayakuwepo. Jumla ya hekta 7,000 tayari zimetengwa kwa ajili ya shughuli hiyo. Pia hata hapo Kongwa tumetenga hizo hizo hekta 2,000 kwa ajili ya wananchi waweze kupata maeneo ya malisho. Kwa hiyo, katika Wilaya mbalimbali hizi za Kongwa, Longido, Siha, Arumeru na Karagwe kote kule tumetenga hekari hizo. Kwa hiyo, NARCO pamoja na TALIRI yote tunatoa hekta hizo kwa ajili ya malisho.

Mheshimiwa Spika, lingine tuliloamua ni kwamba katika maeneo ya ranchi zetu ambazo kuna watu wamewekeza, wale wawekezaji wote wababaishaji ambao na Waheshimiwa Wabunge mmewazungumza hapa kwa hisia kubwa, tumefanya tathmini wengine hawajawekeza kabisa na wengine hawalipi kodi ya Serikali, wote wale tunawaondoa. Taratibu zimeshakamilika kilichobaki ni kwamba kufikia tarehe 1 Julai, tutakuwa tumeshamaliza kuwaondoa wawekezaji wote wababaishaji na tutabaki na maeneo yetu ambayo tutaweza pia kuwapa baadhi ya wafugaji kwa ajili ya kulishia mifugo yao kwa utaratibu ambao utakuwa umewekwa.

Mheshimiwa Spika, vilevile tukaweka utaratibu mwingine kwamba kutakuwepo na ardhi ambayo haitakodiwa na mwekezaji wa kudumu. Itakuwa standby kwa ajili ya ku-accommodate kama kunatokea changamoto katika eneo hilo la malisho ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, tukaenda mbali zaidi kwamba wenzetu Wizara ya Maliasili na Utalii walishakuja hapa kutokana na timu hiyo iliyoundwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu ambayo Wabunge wengine wanauliza kwamba matokeo yake yapo wapi, lakini matokeo tayari tulishayaleta Bungeni. Hizi hekta nilizozitaja za watu ambao tunawaondolea ni zaidi ya hekta 65,000. Vilevile Maliasili na Utalii wamekubali kuyaondoa maeneo tengefu ambayo hayana sifa na wanakamilisha tu, wametuambia hapa watakamilisha hivi karibuni ili maeneo hayo yaweze kutolewa kwa wafugaji. Zaidi ya hekta 96,000 nazo zitatolewa ili kwenda kumaliza migogoro ya wafugaji wetu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kubwa ambalo limefanyika hapa leo, nadhani watu wote wamesikia maamuzi ya Serikali dhidi ya malalamiko ya wafugaji ambao mifugo yao ilikuwa imeshikiliwa na hifadhi. Waziri wa Katiba na Sheria hapa ametoa matokeo ambayo ni zaidi ya ng’ombe 500 kesho zitaondoka. Hii inatokana na kikao ambacho nilikutana na wafugaji juzi kabla ya kuwasilisha bajeti yangu hapa. Tukazungumza wakanipa malalamiko yao nikachukua hatua ya kumuomba Waziri Mkuu baadhi ya Wizara tukutane. Tukakutana Wizara yangu, Wizara ya Katiba na Sheria, Mwanasheia Mkuu wa Serikali, Mwendesha Mashtaka wa Serikali na Wizara ya Mambo ya Ndani tukazungumza tukakubaliana na hatua zinaendelea kuchukuliwa kwa ajili ya kupunguza haya malalamiko ya wafugaji hasa wanapokuwa wamekamatwa kwa makosa mbalimbali katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kabla ya hapo nilichokifanya ilikuwa kuwakumbusha pia wenzangu wa Wizara zingine umuhimu wa kuzingatia sheria unapokuwa umekamata mifugo ili kupunguza malalamiko ya mifugo kukamatwa na kufa na kukosa mahitaji muhimu kama ya maji na malisho. Nikaandika Waraka kwa wenzangu wote na unafanya kazi, naamini kabisa kwamba malalamiko ya namna hiyo sasa yameanza kupungua. Nataka niwahakikishie wafugaji wa nchi hii wapo kwenye mikono salama na tutahakikisha kwamba haki zao zinalindwa kwa nguvu zote ili waweze kuzalisha kwa maslahi ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilikuwa ni kuitaka Wizara kuhakikisha kwamba kunakuwa na uwekezaji mkubwa katika viwanda vya nyama, maziwa na kadhalika. Nataka niwahakikishie kwa muda huu mfupi ambao nimekuwepo mimi na Naibu wangu kwenye ofisi ile tumefanya mambo makubwa. Tumefanya tathmini ya mikataba yote na mikataba mingi tumevunja ambayo haina tija kwa Taifa na mingine ambayo haijakamilika tupo kwenye hatua za kuikamilisha hivi karibuni.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano Kiwanda cha Shinyanga kilichukuliwa na kikauzwa kinyemela na hati haikupatikana. Tumesimamia mpaka ile hati imepatikana kwa muda mfupi na sasa Kiwanda cha Shinyanga tathmini imeshakamilika na niwahakikishie kwamba mwezi huu wa sita tunatangaza tender ya kumpata mwekezaji mahiri kwa ajili ya kiwanda hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeenda Kiwanda cha Mbeya kiko vizuri kina ranchi safi. Kiwanda hiki na chenyewe tumehakikisha kwamba kinafanyiwa tathmini sasa ili mwezi huu wa sita na chenyewe kitangazwe ili tuweze kupata mwekezaji mahiri. Kiwanda cha Ngozi cha Mwanza ambacho Wabunge hapa wamekizungumza sana na chenyewe tayari Msajili wa Hazina anaenda kufanya tathmini ya kujua thamani yake ili na chenyewe tuweze kukitangaza ili tuweze kupata mwekezaji mahiri katika kiwanda hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mnaweza kuona kasi ya Wizara katika kuhakikisha kwamba viwanda vinajengwa Tanzania na vinaimarika kwa ajili ya ku-support hili soko la mifugo kwa sababu mifugo yetu tusipohakikisha viwanda hivi vinaanzishwa basi faida yake itakuwa ngumu sana. Kwa hiyo, viwanda hivyo vinaanzishwa na kile cha Utegi, lakini tuna kiwanda kingine kinajengwa Longido cha mtu binafsi, tuna kiwanda kingine kinajengwa Chato, Geita cha mtu binafsi. Kwa hiyo, mtaona kwa muda mfupi mageuzi makubwa ya mifugo yanakuja.

Mheshimiwa Spika, mmezunguzia juu ya uwekezaji katika Ranchi za Taifa (NARCO) na kuna wachangiaji zaidi ya 12. Kuna migogoro ya mipaka imezungumzwa huko na kuna mikataba imevunjwa ambayo haina. Ni kweli kabisa, mkisoma kwenye ripoti yangu mtaona mikataba ambayo tumeamua kuivunja ambayo haina tija. Moja, ni mkataba wa TMC, kiwanda chetu cha nyama hapo ambapo toka tukibinafsishe mpaka leo Serikali haijapata gawio, leo miaka kumi. Tumefanya tathmini katika kiwanda hicho, tukaona madhaifu yalipo na tukakuta kwamba miaka kumi hiyo hawajaweza kufanya malipo ya gawio lolote la kwetu.

Kwa hiyo, tunakamilisha hatua na mkataba huo tutauvunja. Tulipotishia tu kuvunja mkataba wakaja kwetu wakituambia kwamba tayari wana karibu shilingi bilioni 2.8 kwa ajili ya kutoa gawio. Kwa hiyo, mnaweza kuona mambo ambayo yalikuwa yanafanyika, ni mambo ambayo yalikuwa yanahitaji tathmini nyingi ili uweze kufikia maamuzi. Ndiyo maana mtaona kwenye ripoti hii kuna tathmini na operesheni, mambo hayapo sawa ukiona hali imekaa namna ile.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Diodorus Kamala, kaka yangu na kwa kweli nilikuwa mbeba mikoba hata alipokuwa Waziri. Yeye amezungumza suala la mgogoro wa mpaka alionao kati ya wananchi wake na NARCO. Mambo ya mipaka ni ngumu sana kiongozi kuyaamulia mezani, inahitaji nipate muda niende huko nikaone huo mgogoro kati ya NARCO na wananchi wale ukoje, tutatatua hakuna
ambalo litatushinda kwa sababu sheria ipo na nyaraka zipo, tutazipitia tutaona nani yupo sawa na kuna kasoro wapi. Nilishamuahidi Mheshimiwa Diodorus Kamala kwamba nitakwenda huko kwa ajili ya kushughulikia suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa suala la Operation Nzagamba. Operation Nzagamba imekuja baada ya kuona rasilimali zetu zinatoroshwa. Waheshimiwa Wabunge nataka niwaambie, tupo hapa tumekula kiapo kwa ajili ya Taifa hili na kulinda rasilimali hizi za Taifa. Hakuna mtu yeyote mwenye nia yoyote mbaya na Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Watanzania hawa wafugaji na wavuvi, mimi kama Waziri mwenye dhamana ya mifugo ningependa wapate mafanikio makubwa sana na lazima wapate mafanikio makubwa. Rasilimali hizi zinaibiwa, kila mtu anabeba anavyoweza. Kwa mwaka mmoja ng’ombe 1,600,000 wamebebwa, kondoo na mbuzi zaidi ya 1,500,000 wametoroshwa kwenda kuuzwa nje ya nchi bila kulipa chochote. Wanapoenda kuuzwa nje ya nchi sisi hatupati kitu chochote. Ngozi, nyambi, ajira na mapato ya Serikali yanaenda nje, tutaendeshaje? Yaani tuchunge sisi halafu wafaidike watu wengine? Hatukatai rasilimali zetu kwenda nchi jirani hata kidogo na isichukuliwe kwamba kuna Waziri au mtu yeyote anakataa, tunachokataa ni lazima Taifa hili linufaike kwa mujibu wa sheria zilizowekwa.

Mheshimiwa Spika, gharama ya mtu akitaka kuuza ng’ombe nje ya nchi analipia shilingi 20,000 kwa mujibu wa sheria kwa ng’ombe mmoja na kwa mbuzi analipia shilingi 5,000. Haiwezekani ng’ombe wetu wakaenda bila kuzilipa hizo tozo na mimi Waziri nipo hapo kwenye Wizara, haiwezekani. Lazima tuweke utaratibu ambao utalifanya Taifa hili linufaike. Tulikuwa tunakusanya shilingi bilioni 1.1 kwa mwezi kwa maana ya sekta ya mifugo, leo niwaambieni kutoka shilingi bilioni 1.1 hizi operesheni ambazo mmezihoji tunakusanya shilingi bilioni 3.5 kwa kudhibiti fedha ambazo zinaibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaamini wamekuja Mawaziri hapa wa Afya mmewapigia makofi kwa sababu wanajenga vituo vya afya lakini si ndiyo hela zenyewe lazima tusimamie vyanzo vyetu ili tuweze kulijenga Taifa letu. Sasa wewe una mifugo, unatangaza una mifugo milioni 30; mbuzi milioni 18 na kondoo milioni 50, uchunge wewe asubuhi mpaka jioni halafu wakanufaike watu wengine hata kodi kidogo usitoze, halafu ukitoza kidogo iwe lawama tena? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nakubali yapo mambo ambayo tunaweza kushauriana kwa namna ya kuyaweka yawe vizuri zaidi, lakini nataka niwaambie tunaibiwa mno na ndiyo maana nikawapa na hiyo tathmini ya shilingi bilioni 263 zinatoroshwa. Mifugo iliyopo kwenye Taifa hili, Wizara ya Mifugo kwa kodi tunayokusanya haiwezi hata kulipa mishahara ya Wizara labda niwaambieni sasa ndiyo muone wingi wa utoshaji ulivyo. Hata Wizara ya Mifugo yenyewe mapato yanayopatikana hayawezi kulipa mishahara, hatuwezi kukubali ikawa hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumefanya operation hapa, watu wanaingiza maziwa na nyama ambazo hazijalipiwa. Wazalishaji wa nchi hii wanakula hasara kubwa, wenye viwanda vya nyama na maziwa wanapata hasara. Sisi ndiyo Wabunge na ninyi ndiyo muda wote mmetulalamikia kushindwa kusimamia unregulated importation. Sasa unataka Waziri afanye nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitegemea na naomba mnipe nguvu zaidi ya kuhakikisha kwamba tunazilinda hizi rasilimali. Katika miezi sita niliyokaa kwenye Wizara hii makusanyo ambayo tumekusanya pamoja na kodi mwaka jana mlioziondoa nyingi sana Waheshimiwa Wabunge katika Wizara hii lakini tumekusanya mpaka sasa hivi tuna shilingi bilioni 37; zaidi ya shilingi bilioni kumi za mwaka jana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu walisema Wizara hii wanatoza watu kodi kwa ajili ya kubaki na hela, hakuna fedha yoyote inayobaki Wizarani. Fedha hizi zote zipo Hazina na ndizo hizo zinazoenda kwenye miradi yenu ya maji, zahanati na kila kitu. Mimi Mpina na Wizara yangu tunapata mshahara tu uliowekwa, ndiyo tunachopata lakini hakuna maslahi mengine yoyote yale katika kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Taifa hili ni la kwetu, mmetuapisha kwa katiba na kwa sheria tunazisimamia sheria ili Taifa linufaike. Mtaona makusanyo haya, tulikuwa tunakusanya kama shilingi bilioni 32 tu Wizara yote yaani sekta yote ya mifugo na uvuvi unayoijua. Nawaambieni tupo hapa leo mwaka unaokuja wa fedha katika Wizara hii tutavunja rekodi ya kukusanya karibu shilingi bilioni 100. Yote haya ni ili Watanzania wapate fedha wanufaike na rasilimali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wapiga kura wangu wa Kisesa wako hapa wananisikiliza, mimi siyo mnafiki na mpaka naingia kaburini sitakuwa mnafiki. Sekta hii tutaisimamia kwa weledi mkubwa kuhakikisha kwamba Taifa hili linaendelea maana tumechezewa mno. Kama tunachezewa halafu hatujui tunachezewaje tutaingia kwenye mgogoro mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie sekta ya uvuvi. Tumefanya maamuzi, Waheshimiwa Wabunge mmekuwa mkituomba muda wote mnataka Shirika la TAFICO lifufuliwe, nimefanya maamuzi Shirika la TAFICO sasa linafufuliwa tarehe 1 Julai na watendaji watakuwa ofisini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mmezungumzia kuhusu ujenzi wa bandari, ujenzi wa bandari tayari na tumeshapata mpaka na mtu wa kufanya huo upembuzi yakinifu. Miezi nane anakamilisha, Tanzania tunaanza kujenga bandari ya uvuvi. Mungu awape nini kama siyo Mawaziri wenye kuthubutu kama mimi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumefanya maamuzi, wafanyabiashara wetu wengi wanalalamika juu ya importation ya samaki wengi sana. Tuna maziwa haya lakini samaki wanaoingizwa hapa mpaka sato ambao tunaweza tukazalisha sisi, vibua ambao wako wengi tu, kwenda kuvua katika katika Ziwa Victoria, watu wanaingiza. Kuna watu wangependa sisi hapa tusivue hata kidogo.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi hali ya uvuvi haramu ilivyo na nitawapa documents ninazo hapa, nataka niwape taarifa. Kuna Wabunge wengine hapa waliongea mpaka wakalia lakini nadhani kama kweli ni wazalendo, hizo taarifa nitakazozitoa hapa zitawaliza machozi kwa ajili ya Taifa lao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaibiwa kila sehemu, kwenye uvuvi hapa nimeendesha hiyo Operation Sangara inaitwa Operation Sangara 2018. Operation Sangara 2018 ninavyoiendesha mimi na Wizara yangu, kwanza, utaratibu wa muundo wake, tumeunda operation ambayo sio ya wavuvi tu, tulijua hili na mimi najua operation hizi, kila mtu aliyefanya operation, Waziri yeyote aliyefanya operesheni alipata tatizo katika Bunge hili na nilijua toka mwanzo kwamba haya yatajitokeza. Ndiyo nikasema tunapounda operation hii, nikasema Wavuvi, Mazingira, Polisi, Usalama wa Taifa wote wawemo ili tunapokwenda, tunakwenda kama task force kwa ajili ya kwenda kung’oa huu mzizi wa uvuvi haramu ulioshamiri ambapo Taifa linakosa mapato yake. Watanzania wanakula vifaranga, hii nchi siyo ya kula vifaranga, yenye maziwa na bahari kubwa. Halafu Watanzania wanakula vifaranga na wanakula samaki wa kutoka nje na wana furaha kubwa kufanya hivyo wakati samaki wao wanavuliwa kwa shuka, wanavuliwa kwa nyavu zisizoruhusiwa. Kwa hiyo, tukawa tunafanya hivyo.

Vilevile kulikuwa na timu ambayo inaratibu zoezi hili ambayo nayo ilishirikisha Wizara hizo ninazozisema. Tulifanya tathmini za mara kwa mara kuangalia hizi operation zinavyokwenda.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme na Wabunge wanisaidie. Nimeingia kwenye Kamati yangu, ikanieleza kuhusu uvuvi haramu, wakanipongeza kwa kazi nzuri na wakasema niendelee. Nilipokuja kwenye Bunge lako nililieleza kwamba kama kuna changamoto yoyote kuhusu uvuvi haramu, naomba basi hiyo document mimi niishughulikie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wapo Wabunge ambao walikuja ofisini kwangu na malalamiko ya wananchi wao. Mengine yalikuwa ya kutaka tu Waziri aone huruma dhidi yao na nilifanya hivyo na wako wengi. Mimi niliomba nipewe hizo nyaraka lakini mpaka leo ninavyozungumza hakuna nyaraka hata moja niliyoletewa na Mbunge hata mmoja ambayo Wizara yangu ilishindwa kushughulikia. Ndugu zangu uvuvi haramu unaliangusha Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nitoe matokeo, tumefanya operation mara tatu, katika operation ya awali watuhumiwa walikuwa 1,200, tulipokwenda kipindi cha mpito wakafika 610 na tumekwenda kipindi cha pili wakawa 1,474; kwa hiyo wanaongezeka. Zana haramu, kokoro, tulivyoanza zilikuwa 2,661 tulizoziondoa majini, tulipokwenda kipindi cha mpito ikawa 335 na baadae awamu ya pili zikawa 8,007.

Mheshimiwa Spika, kuhusu nyavu haramu awamu ya kwanza ilikuwa 410,213, ya pili 63,757, ya tatu 81,461. Jumla ya nyavu haramu tulizozitoa Ziwa Victoria ni pieces 555,431 ukizidisha mara mita 80 unakuta karibia kilometa 40,000. Kilometa 40,000 ni sawa na kwenda Afrika Kusini karibu mara tano, unaenda unarudi, unaenda unarudi, ndiyo nyavu zilizokuwepo Ziwa Victoria.

Sasa kama una nyavu hizo katika ziwa lako, utafanya nini? Nyavu hizi zote tumeziondoa na sasa kama mnavyoyaona matokeo ni makubwa, samaki wameongezeka katika ziwa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tumekamata samaki wakitoroshwa kwenda nje ambao Taifa lisingenufaika kwa chochote zaidi ya kilo 181,217. Maana yake ni magari 18 ya tani 10 zilikuwa zinatoroshwa tu kwenda Congo, Malawi, Kenya na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, mabondo ambayo yana thamani kubwa, zaidi ya kilo 5,147. Kuhusu pikipiki zinazokamatwa zikibeba samaki wachanga zaidi ya pikipiki 269 zimekamatwa wakibeba samaki wachanga na kwenda kufanya biashara usiku. Magari zaidi ya 564 yakiwa yamebeba samaki wachanga na wasioruhusiwa kwa mujibu wa sheria yalikamatwa.

Mheshimiwa Spika, sasa Ziwa Victoria kama mlivyopata kwenye taarifa katika rasilimali ya tani milioni 2.7 ambazo Taifa hili ndiyo stock yetu ya samaki, tani milioni 2.1 zinatoka Ziwa Victoria. Kwa hiyo, usipo-manage uvuvi haramu kwenye Ziwa Victoria, maana yake sekta au Taifa haliwezi kunufaika kabisa na uchumi wa nchi yake.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na mambo yafuatayo; hii taasisi yetu ya TAFA walikuja ofisini na walikuwa na mambo mawili makubwa waliyoyawasilisha. Moja, ilikuwa ni suala la nyavu za kuunganisha, ndilo lililokuwa tatizo lao kubwa. Walipokuja kwangu nikawaambia nitalifanyia kazi na nikawaagiza TAFIRI kufanya utafiti huo ili tuweze kuja na majawabu ya nini tufanye katika uvuvi huu wa nyavu za kuunganisha.

Mheshimiwa Spika, lakini hata tulipoenda kwenye kikao chetu cha Lake Victoria Fisheries Organization, ndiyo matokeo haya yanatarajiwa yapatikane ili sisi wote kwa pamoja tuweze kuunga lile zoezi la kwamba kama East Africa tutaamua kuvua kwa nyavu za aina gani. Kwa sheria zilizopo zinakataza kufanya uvuvi kwa nyavu zilizoungwa, ndiyo sheria zilizopo na sio Mpina.

Mheshimiwa Spika, vilevile wavuvi hao walivyokuja kwangu baada ya kuachana nao na kuwasihi kwamba waache uvuvi haramu, jioni tu wote walikamatwa, sehemu kubwa wanahusika na uvuvi haramu. Mambo mengine ambayo Waheshimiwa Wabunge walikuwa wakipigiwa simu na wananchi wakiwa kule walikuwa wakiniwasilishia mimi malalamiko. Wanaponiwasilishia malalamiko anaambiwa amekamatwa tu akiwa hana koleo la plastiki, amepigwa faini shilingi milioni tano. Ukienda kufuatilia, ukweli siyo huo na Mbunge mwenyewe mhusika anathibitisha kweli nilidanganywa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hapa nataka niweke hivi, cha kwanza lazima mfahamu, kukamatwa tu kwenyewe ni changamoto, ama umeonewa au umekamatwa kwa haki. Kwa hiyo, taarifa zinaweza zikaletwa zikawa sivyo.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na huyu Mbunge wa Ukerewe Jimboni kwake, tulikuwa na Waziri Mkuu, tumefanya ziara katika eneo la Ukerewe, mabango yote ya Waziri Mkuu yalionesha wanaomba maji na vitu vingine, lilitoka bango moja tu la kulalamikia kuhusu nyavu. Waziri Mkuu ameweza kufanya ziara kule na mimi akaniita. Hakuna mahali ambapo Wizara ililalamikiwa kwa malalamiko ambayo yanazungumzwa hapa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana mimi muda wote niwapo hapa nimekuwa nikiwaomba Waheshimiwa Wabunge kwamba kama kuna tatizo, Mbunge umepewa muda wa kuongea na Mheshimiwa Spika, umepewa dakika 10 zote za kuongea, mpaka unamaliza kuzungumza unasema tu operation hii imejaa uonevu mkubwa, watu wetu wameonewa sana, watu wetu wamedhulumiwa sana lakini kwa nini mimi sijawahi kuambiwa ni wapi, licha ya kuliomba Bunge hili mara kwa mara lituambie ni wapi ambapo wananchi wameonewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Musoma nimekwenda mara nyingi mimi, amezungumza kaka yangu hapa, Mheshimiwa Mathayo kuhusu yale magari ya wafanyabiashara. Amekaguliwa akakutwa na maboksi matatu ya samaki wasioruhusiwa, unataka watendaji wafanye nini? Una samaki maboksi matatu katika gari lako na wanafanya sampling, wakishayapata yale lazima wakukague, wafanye nini sasa, njia mbadala wafanyaje? Unajua kabisa wewe huruhusiwi kununua wala kuuza samaki wasioruhusiwa, alitaka Mheshimiwa Mbunge wafanye nini?

Mheshimiwa Spika, lile gari lingine lililokuwa limekamatwa akanipigia mimi simu, mimi na yeye tunapigiwa simu tu. Yakakutwa maboksi 27 ambayo yana samaki wasioruhusiwa. Sasa ukisharuhusu sheria ya namna hiyo huyu mwenye pikipiki asikamatwe hata akiwa na samaki wasioruhusiwa, huyu mtu wa class hii asiruhusiwe, mtaisimamiaje sheria na hawa watendaji wangu watasimamiaje sheria?

Kwa hiyo, mimi niseme Wizara yangu tuko committed, tuko tayari kuchukua maelekezo ya Waheshimiwa Wabunge, watushauri katika maeneo yote ambayo wao wanaona kwamba hapa kuna kasoro na sisi tunayafanyia kazi. Aliwahi kuja Mheshimiwa Ngeleja ofisini kwangu saa tano usiku akakuta Wizara nzima tuko ofisini. Tunakesha kufanya tathmini hizi lakini kwa shabaha moja tu kuhakikisha kwamba rasilimali za Taifa letu tunazikomboa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza kwamba hawana nia mbaya na operation lakini tunalalamikia kasoro. Sasa mimi kwenye Kamati niliomba kasoro, nikaja hapa Bungeni mwezi Februari nikaomba kasoro na bahati nzuri kuna Wabunge wengine wanasema kabisa tuna ushahidi, huo ushahidi kwa nini hautolewi au kuna tatizo gani? Kwa nini mtu aseme tu nina ushahidi lakini usitolewe? Naweka mezani kwamba sijawahi kuletewa tatizo lolote na Mheshimiwa Mbunge nikashindwa kulitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaeleze jinsi mambo yanavyokuwa na niwape mfano mmoja wa Kisiwa cha Lubili, Bukoba ambapo tulikuta wamevuliwa samaki wachanga kilo 65,000, wameanikwa mpaka hakuna hata pa kukanyaga na yule mtu ni Mkongo ambaye ndiyo anavua. Wanakuja Wacongo na Waganda wanalipa fedha hapa, wana- facilitate uvuvi haramu.

Mheshimiwa Spika, ukienda Uganda, Mheshimiwa Yoweri Museveni ameamua kupeleka jeshi kabisa ziwani kwa ajili ya kupambana na uvuvi haramu. Sisi tunatumia multi-agency yeye anatumia jeshi. Uganda sasa hivi wamepiga hatua kubwa sana katika rasilimali za uvuvi katika Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kueleza kwamba tuliwapa rekodi ya kupungua kwa samaki kutoka tani 50,000 mpaka tani 25,000/26,000 kwa maana ya karibia nusu ya rasilimali zetu zote zilizoko katika Ziwa Victoria zimepungua.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala ambalo limeletwa hapa la uwekezaji wa viwanda katika Ukanda wa Pwani. Tunaomba tuwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba katika Ukanda wa Pwani mipango tuliyonayo sasa uwekezaji utafanyika tu na ndiyo maana nimeamua kwamba TAFICO iwepo pale ili sasa iweze ku-coordinate uwekezaji katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge hapa, kaka yangu sana, Mheshimiwa Alhaji Bulembo, amelalamikia juu ya kumualika mwekezaji mmoja kuja hapa Bungeni na akasema kwamba yule mwekezaji ana tuhuma. Ninachoweza kukisema huyu mwekezaji kwa sasa hapa kwetu katika sekta ya uvuvi, Mafia ana shamba lake ambalo sasa hivi anavuna kwa mwaka tani 300 hadi 400 na ameajiri Watanzania 1,700. Mimi hapa Mpina kumualika kuja Bungeni kama ana tuhuma haimuondoshi kwenye tuhuma zake na wala Mpina hawezi kuingia kwenye mtego huo ambao unazungumzwa, mtego upi sasa? Mimi nimemualika tu kama mwekezaji aje hapa, kama ana matatizo vyombo vya dola si vipo, vitachukua nafasi. Kwa nini nalo hili liletwe liwe kama lawama kwa Waziri kualika mtu kuja hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hebu tupendane, tulijenge Taifa letu kikamilifu. Tulishachelewa mno, ni lazima tuungane sasa kulijenga kwa nguvu zote ili tuweze kufikia mahali ambapo kutaleta matumaini makubwa kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumza dhidi ya nyavu na amefafanua vizuri kwamba tatizo la nyavu tumefanya hivyo baada ya kufanya operation, umekamata kila mtu ana nyavu haramu, isingewezekana muda huohuo tena ukasema kwamba unaweza kuruhusu watu kuingiza nyavu. Sheria inamtaka yule anayetaka kuingiza nyavu ahakikishe kwamba anapata kibali kwanza ndiyo anaagiza nyavu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sisi katika kipindi hiki tulichokuwa tunafanya tathmini na tumemaliza kufanya tathmini, tumeona, kama ni nyavu tutaruhusu za kutoka nje tunataka turuhusu kiasi gani? Si ndiyo Bunge hilihili mnalotaka tuvilinde viwanda vya ndani? Tumetathmini tumeona viwanda vyetu vina uwezo wa kuzalisha karibia asilimia 50 ya nyavu zinazohitajika lakini tumeona bado hawana uwezo wa kumaliza kabisa gap. Kwa hiyo, sasa hivi tutaruhusu kiasi fulani cha nyavu kuingia ili kuweza kuziba gap ambalo watu wetu wanalilalamikia.

Mheshimiwa Spika, nimalizie na hoja nyingine mbili ambazo na zenyewe zimekuwa zikijirudia sana na zimezungumzwa katika maeneo mbalimbali. Wizara iwasaidie wavuvi kupata samaki wengi baharini, hilo Waheshimiwa Wabunge tunalifanya vizuri sana na miradi mingi sana tunapata kwa ajili ya kuwasaidia wavuvi wetu.

Sasa hivi NMB wamekuja na mpango mzuri sana wa kuwatafuta wavuvi wote na kuwaingiza kwenye usajili na kuwafungulia akaunti ili tuanze kuwafahamu wavuvi wetu wako wapi na wanafanya nini. Hili tumelisimamia vizuri sana pale Wizarani na sasa hivi karibu akaunti 20,000 za wavuvi zimefunguliwa nchini na NMB katika maeneo mbalimbali. Tutakwenda kuwafikia wavuvi wote ambao wako takribani 200,000 ili waweze kuingia kwenye mfumo rasmi wa uzalishaji waweze kukopesheka. Kwa sababu watakapokuwa na mikakati hii wavuvi wetu wataweza kukopesheka.

Mheshimiwa Spika, lakini limezungumzwa sana suala la BMUs kwamba zitumike katika kusimamia mambo haya. Katika operation inayoendelea, watendaji na viongozi wengi wa BMUs tumewakamata kwa uvuvi haramu. Kwa hiyo, lazima utathmini kidogo uone mambo ya namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, kaka yangu, Mheshimiwa Kanyasu, yeye kila siku akisimama anazungumzia suala la furu, nembe na gogogo; anazungumzia suala la nyavu ambazo ni double. Nimesema haya mambo jamani ukizungumzia mifugo na samaki, unazungumza sayansi. Waziri au Naibu Waziri hatuwezi kujifungia tu tukasema leo tunaruhusu single, utafiti unakamilika na TAFIRI tumempa fedha alikuwa na upungufu wa shilingi milioni kumi tu kufanya na kuimaliza kazi hiyo ya utafiti. Tutakuja na majibu, Waheshimiwa Wabunge mtuvumilie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hata hawa tuliowapa kazi ya utafiti hawajamaliza swali linaulizwa kila siku lile lile. Suala la nembe na gogogo sheria zilizopo zinakataza kuwavua wale kwa maana ya nyavu zitakazotumika zitakuwa ni haramu Ziwa Victoria. Tayari tumesha mua-sign TAFIRI kufanya hiyo kazi na fedha tumempa; mambo haya yatakamilika tupeni nafasi tunauwezo wa kuleta mageuzi makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninajua, kwamba leo makofi yanaweza kuwa machache sana kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, lakini nitakapokuja mwakani tarehe kama ya leo Bunge lako lote hili watageuka kuwa washangiliaji kutokana na mageuzi ambayo tunaenda kuyafanya. Tumejipanga, hatutashindwa, tupeni imani hiyo ili tuendelee kuwatumikia.

Mheshimiwa Spika, najua ilishagonga ya kwanza, lakini nimalizie tena kwa kuwashukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kunipa imani kubwa ya kuisimamami sekta hii, Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na Baraza zima la Mawaziri. Pia niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Kisesa ambao wanaendelea kunivumilia katika hii kazi ngumu ninayoendelea nao ya kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mhehimiwa Spika, na mwisho Waheshimiwa Wabunge niwaombe, niliwasikia Waheshimiwa Wabunge wakisema kwamba hii bajeti itakuwa ni bajeti ngumu sana kupitishwa na Bunge hili. Mimi naomba iwe bajeti rahisi sana kupitishwa na Bunge kwa pongezi ya kazi kubwa tulizozifanya
kwa mageuzi kama hayo. Mmeona vitu vilivyokamatwa, hawa watu kama wangekuwa sehemu kubwa yao si waaminifu haya mambo tusingeyafanya. Kukusanya bilioni 7.5 katika muda huu za kuuza samaki wanaotoroshwa na faini ambazo zilizokuwa zikipigwa, shilingi bilioni 7.5 si kazi ndogo, wangekuwa wala rushwa hapa tusingefikia kukusanya hayo makokoro yote 555,000 kama wangekuwa watu si waaminifu tusingefikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi ningewaomba kwanza tuwatie moyo Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambao wanasimamiwa kikamilifu ili waendelee kufanya kazi hiyo nzuri ya kulinda rasilimali na ili waweze kulinda Ziwa Victoria na maeneo mengine na maziwa yote na baharini kote. Tumefanya operesheni kule mmeona fani zaidi shilingi bilioni 20, tumekamata ile meli ipo mahakamani tunarajia tutashinda kesi hiyo, tunataifisha hiyo meli. Watu wamegeuza shamba la bibi hapa, wanavuna wao zaidi ya bilioni mia nne na hamsini, sisi tunakusanya kodi shilingi bilioni 3.2; jamani mmekubali haya yaendelee kutokea?

Mheshimiwa Spika, huko kwenye operation Mati nimezungumza suala la yule mwananchi ambaye alikufa. Jambo hili liko kwenye vyombo vya dola kuona mambo yalienda vipi na ndiyo maana Waziri wa Mambo ya Ndani hapa alishatoa majibu ya jambo hilo, linachunguzwa, watendaji hawa wa Serikali wana sheria zinazowaongoza, kama kuna kosa lilifanyika mhusika atachukuliwa hatua.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kuwaomba tena Waheshimiwa Wabunge waunge mkono bajeti hii ili waiwezeshe Serikali kutekeleza majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ninawaomba tena; mimi Mpina na Wizara yangu ni vibarua tu, tuleteeni mapungufu ya maeneo mbalimba hapa hata leo, hata sasa hivi tutaenda kwenye maeneo hayo, kwenye vijiji hivyo kukutana na wananchi hao ili tuweze kumaliza mzizi wa fitina na kuondoa kasoro hizo ambazo wananchi wametendewa isivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba sasa kutoa hoja.