Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Spika, kwanza ni masikitiko makubwa sana kuendelea kuona kwa miaka miwili mfululizo sasa pesa za maendeleo katika sekta ya mifugo – Fungu 99 na sekta ya uvuvi – Fungu 64 hazijapelekwa mpaka sasa. Naiomba sana Serikali kama kweli ina nia thabiti ya kuwasaidia wafugaji wetu na wavuvi wa nchi yetu, basi ipeleke pesa za maendeleo kwenye sekta hizi muhimu ili tuweze kuwakomboa Watanzania wenzetu wanaoteseka sana ndani ya nchi yao.

Mheshimiwa Spika, Ranchi ya Mkata kwa muda mrefu sana imekuwa kama kichaka cha wahalifu na kushindwa kusaidia wafugaji wetu kufuga, kulima, malisho na kukodishia wafugaji na kusababisha wafugaji wengi wa Mkoa wa Morogoro pamoja na Kilosa kukosa njia mbadala ya kupata njia bora ya kufuga mifugo yao. Tunaomba Serikali iangalie sana ranchi hii.

Mheshimiwa Spika, bado kuna migogoro mingi ya wakulima na wafugaji kwenye Wilaya ya Kilosa na hii inatokana na ufinyu wa ardhi bora na wingi wa mifugo. Wafugaji wana mifugo mingi sana hata wanakosa maeneo ya malisho na maji ya kutosha (malambo) na kusababisha kuingiliana sana na mashamba ya wakulima na kusababisha migogoro isiyokwisha ya wafugaji na wakulima. Tunaiomba sana Serikali ipunguze maeneo ya ranchi na maeneo tengefu na kuyagawa kwa wafugaji ili waweze kupata maeneo ya kufugia, malisho, malambo na majosho.

Mheshimiwa Spika, lingine ni mipaka ya vijiji vya ufugaji na maeneo tengefu na hifadhi. Kuna migogoro mikubwa sana kati ya maeneo (vijiji) vya wafugaji kama Mufilisi na Mkaa Endelevu na vijiji vingine kama Kiduhi na mipaka ya Hifadhi ya Mikumi na vijiji vingine vya wafugaji kama Parakwiyo, Mbande na Twatwatwa vilivyopo Wilayani Kilosa na ambavyo vimekuwa na migogoro ya mipaka na hifadhi na baadhi ya vijiji vya wakulima. Tunaomba sana Serikali itupie jicho jambo hili na kumaliza migogoro hii ya muda mrefu sana.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kilosa ina upungufu mkubwa sana wa majosho, malambo na malisho ya mifugo. Kwa hiyo, tunaiomba sana Serikali iweze kuwasaidia wafugaji wetu hao pamoja na madawa ya mifugo yao ambayo mingi inakufa kwa magonjwa mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukiwaomba sana wafugaji wapunguze mifugo yao kwenye Wilaya ya Kilosa lakini hatujawaandalia masoko ya mazao yao ya mifugo. Tunaiomba sana Serikali kujenga viwanda vya mazao ya mifugo kama viwanda vya kusindika nyama, maziwa na viwanda vya ngozi katika Mkoa wa Morogoro na Wilaya ya Kilosa ili kuweka mazingira wezeshi na rahisi kwa wafugaji wetu kuweza kufuga mifugo michache na yenye tija kwa Taifa letu. Ahsante.