Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, napenda kuanza mchango wangu kwa sekta hii kuanza na sekta ya uvuvi. Sekta hii haijapewa msukumo wa kutosha kwani hadi leo bado Taifa linaagiza samaki kutoka nje. Pamoja na kuwa ubora wa samaki wa kutoka nje wanatiliwa mashaka, hadi leo hakuna uwekezaji wa kibiashara katika sekta ya uvuvi kwani hadi sasa hakuna meli kubwa ya uvuvi hasa kwenye bahari kuu wala hakuna kampuni yoyote ya sekta binafsi kuonesha uwezo wa kumudu kuingia kwenye sekta ya uvuvi wa kisasa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa na maji ya kutosha, ya bahari na maziwa makuu, bado tunaagiza samaki na mazao ya samaki toka nje ya nchi. Tumechoka na samaki wabovu kutoka China, samaki vibua.

Mheshimiwa Spika, ni ipi sera ya Serikali ya Awamu ya Tano juu ya Wizara hii? Kama hakuna fedha za maendeleo zinazopelekwa kwenye Wizara hii pamoja na kuonekana kukusanya vizuri maduhuli ya Serikali bado hata hizo fedha wanazokusanya wenyewe Wizara ya Fedha hawataki kurudisha fedha hizo kwenye Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Ni jambo lisiloeleweka kuona Taifa lenye rasilimali za bahari, maziwa na mifugo ya kutosha bado tunaagiza samaki, nyama na maziwa toka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, uvuvi haramu unachangia kwa kiasi kikubwa na utendaji mbovu wa watendaji wa Wizara hii kwani si sawa sawa kunyang’anya nyavu baharini, ziwani badala ya kwenye vyanzo vya vifaa au zana hizo zinazoitwa haramu, je, wavuvi wanapata wapi zana hizo? Kwa nini Serikali inashindwa kusimamia uingizajiwa zana hizo haramu badala ya kuwapa hasara wavuvi kwa kuchomewa zana zao?

Mheshimiwa Spika, mifugo sasa nchini inaelekea kuwa balaa badala ya neema kwani hakuna utaratibu wa kueleweka juu ya namna bora ya ufugaji wala namna bora ya uvunaji wa mazao ya mifugo ikiwemo nyama, maziwa, ngozi na mayai. Wafugaji wetu bado ni wafugaji wa kienyeji wa kuhamahama bila kujali Taifa linapata nini juu ya wingi wa mifugo ambayo kwa uhalisia inatuletea migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Spika, elimu kwa wafugaji juu ya ufugaji bora wenye tija bado ni ndogo sana. Hivyo, Wizara inatakiwa kuwekeza zaidi kwenye elimu ili watu wafuge kwa tija. Hivyo kuweza kujitosheleza kwa kuwa na viwanda vya kutosha katika kuongeza thamani kwenye mazao yanayotokana na mifugo. Hakuna uwekezaji wa kutosha katika sekta ya mifugo juu ya uchakataji wa mazao ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, Wizara haioneshi mipango wala dira ya kutupeleka kwenye ufumbuzi wa changamoto zilizo kwenye Wizara hii, kwa sababu kutokupelekewa fedha za maendeleo kunaonesha wazi kuwa hakuna dhamira ya kutatua changamoto za Wizara.

Mheshimiwa Spika, kutawanya mifugo nchi nzima hakuwezi kuwa ni njia bora ya kukabiliana na changamoto hizo, tumeamua kusambaza mifugo kama tulivyoamua kusambaza mazao ya kilimo, jambo hili tusipolichukulia hatua kwa makini tunakwenda kuifanya Tanzania ya jangwa kwa kuondoa uoto wa asili wa nchi hii.

Mheshimiwa Spika, tunahitaji miradi ya uchimbaji wa malambo, mabwawa na maeneo ya minada hasa kwa mikoa ile ambayo si ya wafugaji kwa asili, mikoa kama ya Lindi na Mtwara bado hakuna malambo, mabwawa wala maeneo ya minada. Jambo hili linafanya mikoa hiyo kutopata faida ya mifugo hiyo kwani hakuna faida ya moja kwa moja kwa jamii kwa kuhamishia mifugo hiyo. Serikali inapaswa kutafuta wawekezaji wa ndani na nje ili kunusuru sekta hii na kukuza pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, maafisa mifugo ni tatizo lingine kwenye sekta ya mifugo, mfano;- Mkoa wa Lindi si Mkoa wa wafugaji. hivyo, idadi ya maafisa mifugo haikuwa kipaumbele, lakini kwa hivi sasa baada ya Serikali kusambaza mifugo nchi nzima hivyo umuhimu wa maafisa mifugo ni mkubwa sana kwa Mkoa wa Lindi hasa katika Jimbo la Liwale ambako hakuna miundombinu yeyote iliyoandaliwa kupokea mifugo. Kwani sasa nyama zinauzwa bila kupima ubora wa nyama na hakuna sehemu maalum kwa ajili ya mnada wa ng’ombe hivyo, Wilaya ya Liwale tunahitaji wataalamu wa mifugo.

Mheshimiwa Spika, kukosekana kwa wataalamu hao kunakuwepo na ufugaji usiotunza mazingira hivyo kuharibu vyanzo vya maji.