Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi uliyonipa ya kuchangia. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya njema aliyonipatia, Muumbaji wa Mbingu na Nchi na vyote vilivyomo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Rais Magufuli kwa kumteua Mfugaji Mheshimiwa Mpina kuwa Waziri wa Wizara hii na kwa kumteua Mheshimiwa Naibu wake ambaye pia ni Mvuvi. Amewateua kwa makusudi maalum akijua kwamba wanajua changamoto za wakulima, wafugaji na wavuvi. Kwa hiyo wavuvi na wafugaji wana matumaini makubwa sana na Mheshimiwa Waziri aliyepo na Naibu wake kwa sababu wanaijua sekta hii vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma kwa haraka sana hotuba ya Mheshimiwa Waziri na jinsi sekta ya mifugo ilivyochangia Pato la Taifa na nimefadhaika na kuhuzunika nilivyosoma taarifa hii jinsi sekta ya mifugo ambayo imetufanya kuwa nchi ya tatu Afrika kwa wingi wa mifugo lakini ikachangia kiasi kidogo sana katika Pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana hatuko makini, inawezekana hatujajali sana sekta hii ya mifugo na uvuvi, kiasi kwamba tungekuwa serious katika sekta hii tungefanya vizuri na sekta ya mifugo ingechangia kama sekta ya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Waziri ukusara wa 25 amesema Wizara ilikusanya bilioni 10.5 tu na kutochangia ipasavyo katika pato la Taifa na wakaorodhesha sababu huku, wakasema zaidi ya asilimia 20 ya maziwa yanaagizwa kutoka nje. Wakasema usafirishaji holela wa ngozi ndani na nje ya nchi, uingizaji mkubwa wa bidhaa za ngozi kutoka nje, kuwepo dawa bandia. Naamini tuna watalaam na naamini wataalam wetu kazi yao ni kusimamia sekta waliyoisomea na waliyopewa kuidhibiti. Nilikuwa na matumaini kwamba wasingeruhusu haya yote yakatokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, napata kigugumizi kuona kwamba sekta ya mifugo inachangia kiasi kidogo namna hiyo. Siyo mwaka huu tu, miaka yote ya nyuma sekta ya mifugo inachangia kidogo sana pato la Taifa. Tumepoteza bilioni 263.95 kwa sababu ya kutosimamia/kutodhibiti sekta ya mifugo na hii iko katika ukurasa wa 28 wa hotuba ya Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukipita vijijini akinamama na vijana wanatembeza maziwa, hawana pa kupeleka kwa sababu hatuna viwanda vya maziwa; viwanda vya maziwa ni vinne tu nchi hii yenye ng’ombe wengi. Havitoshelezi kununua maziwa ya nchi nzima, lakini kama hatuwezi, hatuna viwanda vya kutosheleza tutafute namna ya kusindika haya maziwa yakauzwa nje ya nchi kuliko kutumia Lactogen (maziwa ya kopo) kwa watoto wetu, maofisini na hata mahotelini wakati tuna ng’ombe zaidi ya milioni 20, hatufaidiki na ufugaji tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wafugaji waliopo hawafaidiki na ufugaji kwa sababu hawana namna ya kuuza ng’ombe, hawana namna ya kusafirisha ng’ombe nje ya nchi na hata utaratibu wa dawa za mifugo haueleweki. Wafugaji wananunua hawajui kwamba je, hii ni dawa halisi au dawa hii siyo dawa halisi, mradi kaikuta dukani kama ina jina bandia hajui kwa sababu hata Maafisa Ugani tulionao hawatoshelezi. Hatuna Maafisa Ugani wanaotosheleza mahitaji katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, usafirishaji wa ngozi, hatuna viwanda vya ngozi ndiyo maana tunanunua viatu kutoka China na Kenya, nje ya nchi hatuna viwanda vya ngozi. Viwanda vya ngozi hatuna, viwanda vya maziwa vinne tu, viwanda vya nyama sijui ni vingapi hata ile cha Shinyanga nadhani imeshasimama, Tanganyika Packers ndiyo tulishasahau; kuna nini katika kuanzisha viwanda vya mifugo hapa nchini?(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashindwa kuelewa/ nashindwa kujua tatizo lipo wapi. Mwaka huu au mwaka wa fedha unaoisha Wizara ya Mifugo walipiga chapa ng’ombe wakapata bilioni 14; kazi ndogo kweli lakini walipata bilioni 14. Hizi bilioni 14 hawajarudisha kwa wafugaji, hawajachimba malambo, wafugaji wanahangaika kipindi cha kiangazi, lakini kwa chapa tu wamepata bilioni 14. Wafugaji hawana malambo wakati wa kiangazi wanahama huku na kule, Wizara iwasaidie wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chuo chetu cha LITI kipo Mpwapwa, kile chuo kilishasahaulika siku nyingi, mabweni yamechakaa, hakuna vifaa vya maabara, mabweni yamechakaa, madarasa yamechakaa, bajeti ni finyu lakini wanafunzi Tanzania nzima wanakwenda pale kujifunza. Nimwombe Mheshimiwa Waziri akikumbuke Chuo cha LITI. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme jambo moja tena, wavuvi wameonewa sana katika nchi hii. Nyavu inchi nne na inchi tano ni haramu, timba na kokoro ni haramu, nyavu inchi sita na saba kama ina macho 78 ni haramu, lakini kama ina macho 26 ni halali. Wavuvi wamechomewa nyavu zao waliokopa wengine wamekufa; wamekufa kwa sababu wanatozwa faini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unashikwa na samaki, samaki hao wakati wavuvi wanakwenda ziwani/baharini, Afisa Uvuvi amekagua nyavu lakini wanapotoka kuvua samaki wanakamatwa, nyavu zinachomwa na faini anatozwa milioni 25 au milioni 50 alipe ndani ya masaa 24. hivi ni nani nayeweza kuwa na milioni 50 kwa siku, akiweka pesa yake tayari tu kwa ajili ya kulipa faini kwa sababu ya nyavu ambazo Afisa Uvuvi amezikagua na Mkurugenzi wa Uvuvi alipitisha lakini bado nyavu zikachomwa. Watu wamekufa; Kanda ya Ziwa, Ziwa Tanganyika, Ziwa Nyasa watu wamekufa, Rukwa watu wamekufa kwa mambo ambayo Serikali ingeweza ikakaa na wavuvi na wakaelewana na wavuvi wakapata elimu hiyo na wasirudie makosa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wako waliochomewa kimakosa, hawa waliowachomea kimakosa wanawafanyaje? Nyumba zao zimeuzwa walikopa benki, wanawafanyaje? Tunaambiwa nyama ina cholesterol tule samaki, Dodoma sasa hivi unaweza kutafuta samaki mabucha 20 usipate samaki kwa sababu ya matatizo yaliyopo kwenye maziwa na bahari zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Mwanza kuna mtu mmoja tu anaitwa Naipich ndiye ameruhusiwa kutengeneza nyavu, hivi yeye peke yake anaweza kutengeneza nyavu za Tanzania nzima? Hivi dagaa anavuliwa kwenye nyavu ya aina gani, kule Ziwa Viktoria kuna samaki wanaitwa Furu, Furu hakui hata ukimfuga miaka 20 yupo vilevile anavuliwa kwenye nyavu za aina gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusiwafanye wavuvi wakajiona kwamba wao sio Watanzania, tusiwafanye wavuvi wakatuchukia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba Ranchi zetu pia hazijatumika vizuri.