Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nitoe mchango kwenye Wizara hii muhimu inayogusa zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niipongeze Serikali hasa kwa zuio la kuuza mahindi nje ya nchi. Nimesoma kitabu hiki kwenye ukurasa wa 61, nafikiri kilio cha Wabunge wengi mwaka jana, tuliolalamika kwamba Serikali isiingilie mfumo wa soko la mahindi, naona Serikali imesikia na mkatekeleze hili kama mlivyopanga. Isije sasa wakulima wanaanza linaanza tena zuio jipya la vibali watu wasiuze. Liacheni soko liwe huru, watu tukauze mahindi mahali popote panapohitajika. Naipongeza sana Serikali kwa ajili ya hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuishauri Serikali hasa kwenye soko la mbaazi. Soko la mbaazi ni gumu sana, wengi wamezungumza, mimi bahati nzuri nilikuwa kwenye kampuni ya wanunuzi wakubwa wa mazao hayo duniani kwa miaka 19 lakini tulifanya miaka mitatu tu, miaka 16 yote hatukununua hata kilo moja na ni kampuni ya Wahindi wenyewe. Changamoto kubwa ni soko lina hatari kubwa sana kwa sababu mnunuzi mkubwa ni mmoja peke yake. Kwa hiyo, siku yoyote akibadilisha sera zake au siku yoyote uzalishaji kwake ukiwa mkubwa ni tatizo kwenye mbaazi kama tulichokiona mwaka jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, mnunuzi mkubwa ni Serikali ya India ni vizuri sana, kwa sababu biashara ni diplomasia, Wizara ya Mambo ya Nje, Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda na Biashara mkae pamoja ili hawa watu wa diplomasia, Waziri wa Mambo ya Nje akae na Serikali ya India, tupate makubaliano ya awali ya kuwauzia mbaazi zetu kama walivyofanya Ethiopia na nchi zingine. Hata kukiwa na uzalishaji mkubwa hawawezi kubadilisha lazima watakuwa wanazingatia makubaliano, zaidi ya hapo, tutakuwa na soko la kubabaisha kwa sababu wao ndiyo wakulima wakubwa, wanunuzi wakubwa na walaji wakubwa wa mbaazi duniani. Lazima tukae na Serikali ya India, tupate ombi maalum la kuturuhusu kwamba mbaazi zetu tuuze kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kuhusu viwanda vya kubangua korosho. Naomba sana kuishaui Serikali, suala la viwanda vya kubangua korosho lilianza tangu mwaka 1978, Mwalimu Nyerere alifungua viwanda 11 na vyote havikubangua korosho na vilikuwa na uwezo wa kubangua zaidi ya tani 100,000. Kama mkikumbuka wakati ule uzalishaji wetu ulikuwa tani 174,000. Viwanda hivi havikununua hata kilo moja kwa sababu ya mabadiliko ya teknolojia, lakini ni kutokana na changamoto nyingi zilizokuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1994 tukafufua makampuni mengi ambayo yalikuja hapa kuwekeza kwa ajili ya ubanguaji wa korosho. Olam Tanzania Limited ilikuwa na uwezo wa kubangua tani zaidi ya 30,000, wamebangua kwa miaka 10 lakini tulipoanza tu stakabadhi ghalani wakahamisha kiwanda chao kwenda Mozambique. Kiwanda cha Mohamed Enterprises kilikuwa na uwezo wa kubangua zaidi ya tani 2,000 kimefungwa, Kiwanda cha Premier Cashew au Fidahussein kilikuwa na uwezo wa kubangua zaidi ya tani 3,000 kimefungwa; Kiwanda cha Masasi Cashewnut kilikuwa na uwezo wa kubangua tani 1,000 kimefungwa; na Kiwanda cha Buko Masasi nacho kimefungwa, hii ni miaka ya 1990 mpaka 2012. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa hivi tuna viwanda vitatu Export Trading Group (ETG) ana uwezo wa kuzalisha zaidi ya tani 5,000 lakini habangui hizo tani 5,000 kwa sababu raw material hapati, anasafirisha nje kama raw material. Sunshine Group pale Lindi kina uwezo wa kuzalisha tani zaidi ya 2,000 lakini raw material kwenye mnada anapata tani 200 tu; Haute ana uwezo wa kubangua tani 2,000 mwaka jana kapata tani 800. Kwa hiyo, unaona kuna shida ya upatikanaji wa raw material kwa viwanda vya ndani. Ni sababu sera zetu wakati mwingine haziruhusu au hazi-favour hawa wabanguaji wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivyo? Hivi viwanda vya ubanguaji vinahitaji hela nyingi sana. Mtu anakuja, anawekeza hela zake anajua kwamba atarudisha baada ya miaka mitano au kumi baada ya miaka miwili sera zimebadilika. Kwa mfano, hapa Tanzania haturuhusiwi kufanya importation ya korosho kutoka nchi zingine. Wakati dunia nzima ubanguaji wa korosho au soko la korosho ni la mzunguko yaani mwaka huu inakuwa miezi mitatu Tanzania, miezi mitatu India, miezi mitatu Nigeria na miezi mitatu Brazil. Kwa hiyo, mtu ananunua miezi mitatu, anabangua baada ya hapo anaenda sehemu nyingine. Kwa hiyo, jambo hilo sera inazuia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwenye sera zetu tuliweka export levy kwa sababu ya kuzuia korosho yetu isiende nje. Ombi, hii ya asilimia 15 inatosha sana, aidha, ibaki hapo au kuwahakikishia wabanguaji iende juu zaidi ili kuzuia hizi korosho zisiende kule. Kwa sababu akija mtu mwingine kesho akishusha hii export levy maana yake mbanguaji wa ndani huyu hawezi kupata raw material, korosho yote itaenda India, itaendelea kwenda Vietnam kwa sababu wana bei kubwa na wana gharama nafuu ya uzalishaji kuliko sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya ushauri huo, naomba sasa niuombee sasa Mkoa wa Morogoro. Serikali ya Awamu ya Tatu iliamua wakati ule Waziri Mkuu akiwa Ndugu Sumaye na Rais Benjamin Mkapa kwamba Mkoa wa Morogoro ndiyo uwe Makao Makuu ya Nane Nane Tanzania na maonesho yote yafanyike pale kwa sababu ya hali ya kijiografia na uwepo wa Chuo cha Kilimo (SUA) pale Morogoro. Baada ya kuondoka, sera hiyo ikabadilishwa, sasa hivi Maonesho ya Nane Nane yanazunguka kila mkoa na kila kanda matokeo yake tunaongeza gharama kwa wadau, kujenga jengo kila mahali, hata yale majengo sehemu nyingi yamebaki magofu. Ombi langu, ni vizuri tuchague sehemu moja tuweke ndiyo Maonesho ya Nane Nane kwa nchi nzima kama tunavyofanya Sabasaba. Yako Maonesho ya Kibiashara Dar es Salaam, kila mtu anajua Dar es Salaam na Maonesho ya Nane Nane yawepo pale Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia kuhusu suala la ushirika. Mheshimiwa Waziri, hizi taarifa za kusema Morogoro tuko tayari kwa ajili ya stakabadhi ghalani mnazitoa wapi? Mimi natoka Morogoro Vijijini, hata kikao cha RCC hatujawahi kukaa Wabunge wa Morogoro, kikao
cha kisheria hatujawahi! Jana unaniambia kwamba Morogoro Mkoa tumekubali stakabadhi ghalani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumwambia Mheshimiwa Waziri aachane na taarifa hizi za kwenye maandishi. Morogoro Vijijini au Morogoro kwa ujumla hatuna vyama vya msingi, hatuna maghala, hatuko tayari na msimu unaanza mwezi ujao (wiki mbili zinazokuja), katika hali kama hiyo tunaanzaje? Huna ghala, huna wataalam, huna vyama, hujavitengeneza, sasa kwa sababu maamuzi yanatoka Serikalini, tunaweza tukakubali kwa sababu Serikali ni chombo kikubwa lakini mngetusikiliza sisi wawakilishi wa wananchi tunaotoka kwa wannachi tunawashauri kwa nia njema, mfumo huu tuanze mwakani badala ya mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kuhusu hizi data kwenye ukurasa wa 65, Mheshimiwa Waziri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)